Sunday, December 31, 2017

ZOEZI LA UPIGAJI CHAPA MIFUGO LAONGEZEWA MUDA WA MWEZI MMOJA

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina ameongeza muda wa mwezi mmoja kwa Halmashauri hapa nchini kukamilisha zoezi la upigaji chapa mifugo na kuwataka watendaji wote wa Serikali wanaohusika kuhakikisha mifugo yote inapigwa chapa.

Waziri Mpina ameyasema hayo leo wakati wa kuhitimisha zoezi la upigaji chapa Kitaifa katika Kijiji cha Migato wilaya ya Itilima mkoani Simiyu, zoezi ambalo lilianza rasmi Kitaifa mwezi Desemba, 2016 na kupangwa kukamilika Desemba 31, 2017.

“Kwa kuwa hadi sasa zoezi hili limetekelezwa kwa asilimia 38.5 kutokana na sababu mbalimbali, Mimi Luhaga Mpina Waziri wa Mifugo na Uvuvi kwa Mamlaka niliyopewa chini ya sheria ya Utambuzi, Usajili na ufuatiliaji wa mifugo ya mwaka 2010 na kanuni yake, ninaongeza muda wa kupiga chapa mifugo kutoka tarehe 01/01/ 2018 hadi 31/01/2018”alisititiza.

Mpina amesema miongoni mwa changamoto zilizopelekea Halmashauri nyingi kushindwa kutekeleza zoezi hilo kwa asilimia 100 ni baadhi ya halmashauri kutokutenga fedha kwa ajili ya zoezi hilo, kubaini mifugo kutoka nje ya nchi, baadhi ya wafugaji kushindwa kutaja idadi halisi ya mifugo yao na baadhi ya Halmashauri kuwatoza wafugaji zaidi ya shilingi 500 ambayo ndiyo bei elekezi, ambapo ameagiza wafugaji hao waliotozwa zaidi ya shilingi 500 warejeshewe fedha zao.

Ameongeza kuwa hadi kufikia Desemba 31, 2017  Halmashauri 30 hapa nchini hazijapiga kabisa chapa mifugo, halmashauri 23 zimeendesha zoezi hilo chini ya asilimia 10 na akaongeza kuwa orodha ya majina ya viongozi wa wilaya hizo walioshindwa kutekeleza agizo hilo la Serikali ameyawasilisha kwa Waziri Mkuu wa Tanzania Mhe.Kassim Majaliwa.

“Halmashauri 30 ambazo hazijapiga chapa kabisa hata ng’ombe mmoja na zile 23 ambazo zimepiga chini ya asilimia 10 majina  ya viongozi wote na Halmashauri husika nimekabidhi orodha hiyo kwa Waziri Mkuu, hatuwezi kuendekeza ukaidi wa maagizo ya Viongozi Wakuu wa Nchi” alisema Mpina.

Akiwasilisha taarifa ya zoezi la Upigaji Chapa katika Mkoa wa Simiyu, Mwakilishi wa Katibu Tawala Mkoa, Ndg.Elias Kasuka amesema zoezi hilo mkoani humo lilianza rasmi mwezi Aprili 2017 ambapo hadi sasa ng’ombe zaidi ya 764, 933 wameshapigwa chapa kati ya ng’ombe 1,500,000.

Akitoa maoni yake baada ya kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo, Paulo Mabula mfugaji kutoka Migato Itilima amesema wafugaji wamelipokea kwa furaha agizo la Waziri wa Mifugo na Uvuvi kuongeza siku za kwa ajili ya kupiga chapa kwani litawasaidia wafugaji ambao bado hawajakamilisha ili kuondokana na changamoto ya wizi wa mifugo.

Naye Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Itilima, Mhe.Mahamoud Mabula amemuomba Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe.Luhaga Mpina kuwasaidia wafugaji wa Wilaya hiyo na maeneo mengine ya Mkoa huo kufanya vikao vya ujirani mwema na wale wa mikoa jirani ili kujadiliana namna ya kuondoa changamoto ya wizi wa mifugo.


Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Itilima Mhe.Benson Kilangi amesema viongozi na wataalam wa wilaya hiyo wamekuwa wakiwahamasisha wafugaji kupanga matumizi bora ya ardhi ili waweze kutenga maeneo kwa ajili ya malisho na kuyawekea miundombinu muhimu kwa ajili ya mifugo ikiwemo maji, majosho pamoja malisho.
Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina(wa pili kushoto) akipiga chapa ng’ombe katika hitimisho la zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa katika Kijiji cha Migato, Wilaya ya Itilima Mkoani Simiyu.
Vijana wa Skauti wilaya ya Itilima wakimvisha skafu Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina alipowasili wilayani humo kwa ajili ya kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo kitaifa, mkoani Simiyu.

Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina akisalimiana na Afisa Mifugo kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Ndg.Ally Mzee mara baada ya kuwasili mkoani humo kwa ajili ya kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa, lililofanyika katika kijiji cha Migato wilayani Itilima.
Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Mhe.Benson Kilangi (wa tatu kushoto) akipiga chapa ng’ombe katika hitimisho la zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa katika Kijiji cha Migato, Wilaya ya Itilima Mkoani Simiyu ambalo limehitimishwa na Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Itilima, Daudi Nyalamu akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Migato na vijiji jirani  mara baada ya Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa lililofanyika kijijini hapo leo.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe.Luhaga Mpina akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Migato na vijiji jirani  mara baada ya kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa lililofanyika kijijini hapo leo.
Mbunge wa Jimbo la Itilima, Mhe.Njalu Silanga akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Migato na vijiji jirani  mara baada ya Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa lililofanyika kijijini hapo leo.
Ndg.Paulo Mabula akitoa maoni yake mara baada ya Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina kuhitimisha zoezi la upigaji chapa Kitaifa katika Kijiji cha Migato wilaya ya Itilima Mkoani Simiyu.
Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina akisalimiana na Mwakilishi wa Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg.Elias Kasuka mara baada ya kuwasili Mkoani humo kwa ajili ya kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa, lililofanyika katika kijiji cha Migato wilayani Itilima.
Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Mhe. Luhaga Mpina akipokelewa na Viongozi wa Wilaya ya Itilima mkoani Simiyu mara baada ya kuwasili wilayani humo kwa ajili ya kuhitimisha zoezi la upigaji chapa mifugo Kitaifa, lililofanyika katika kijiji cha Migato wilayani Itilima.

Friday, December 29, 2017

NAIBU WAZIRI WA MADINI AFANYA ZIARA MKOANI SIMIYU

Naibu Waziri wa Madini Mhe.Stanslaus Nyongo amefanya ziara yake ya kikazi leo Mkoani Simiyu.

Katika ziara hiyo Mhe.Nyongo amekutana na baadhi ya viongozi wa Mkoa wa Simiyu pamoja na watumishi wa Ofisi ya Madini ya Mkoa huo, lengo likiwa ni kuzungumza masuala mbalimbali kuhusu usimamizi wa Sekta ya madini katika Mkoa wa Simiyu, ili kuleta tija kwa wanachi na Taifa kwa ujumla.

Mhe.Nyongo pia amepata fursa ya kutembelea na kuona Jengo la sasa la Ofisi ya Afisa Madini Mkazi na kuahidi kuwa Wizara yake ina mpango wa kujenga jengo la jipya la Ofisi hiyo.

Aidha, amesema atahakikisha tafiti juu ya ubora wa chumvi inayozalishwa wilaya ya Meatu zinafanyika ili kuweza kujua ikiwa inakidhi ubora unaotakiwa kwa matumizi ya binadamu iweze kuongezewa thamani na kutangazwa.

“Tutahakikisha tafiti hizi zinafanyika na mpango wetu ni kwamba zifanyike kwa haraka ili chumvi ya Meatu tuweze kuitangaza, kwa sababu Simiyu tumeshaitangaza vizuri kupitia Chaki sasa tuitangaze tena kwa chumvi yetu” amesisitiza.

Kwa upande wake Afisa Madini Mkazi wa mkoa wa Simiyu, Fabian Mshai amesema wachimbaji wa chumvi wako tayari na wanaomba Mamlaka ya Chakula na Dawa(TFDA) kufanya utafiti kwenye chumvi hiyo  na kushauri namna bora ya kufanya chumvi hiyo iwe bora, ili iweze kupata soko zuri ndani na nje ya nchi.

Naye Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg.Jumanne Sagini amesema ni vema Watendaji wa Ofisi ya Madini Mkoa wakasaidiwa kwa kuwezeshwa vitendea kazi pamoja na mahitaji mengine ili waweze kutekeleza vizuri majukumu yao, ikiwa ni pamoja na kuwafikia wachimbaji kwenye maeneo yanayochimbwa madini na Serikali iweze ipate stahili yake.


Naibu Waziri wa Madini, Mhe.Stanslaus Nyongo akizungumza na viongozi wa Mkoa wa Simiyu (baadhi hawapo pichani) mara baada ya kuwasili mkoani humo kwa ziara ya siku moja (kushoto) Katibu Tawala Mkoa huo, Ndg.Jumanne Sagini(katikati) Mkuu wa Wilaya ya Bariadi.
 Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg.Jumanne Sagini akizungumza wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Madini, Mhe.Stanslaus Nyongo aliyoifanya mkoani humo leo.


 Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Simiyu, Fabian Mshai akiwasilisha taarifa ya Mkoa huo kwa Naibu Waziri wa Madini, Mhe.Stanslaus Nyongo wakati akiwa katika ziara yake mkoani humo. 

Baadhi ya viongozi wa Mkoa wa Simiyu na Watendaji katika Wizara ya Madini wakimsikiliza Naibu Waziri wa Madini, Mhe.Stanslaus Nyongo wakati Wizara yake Mkoani Simiyu leo.

Naibu Waziri wa Madini, Mhe.Stanslaus Nyongo akiagana na viongozi wa Mkoa wa Simiyu mara baada ya kukamilisha ziara yake Mkoani humo.
Naibu Waziri wa Madini, Mhe.Stanslaus Nyongo akisaini kitabu cha Wageni katika Ofisi ya Afisa Madini Mkazi Mkoa wa Simiyu alipokuwa Mkoani humo leo kwa ziara ya siku moja

 Naibu Waziri wa Madini, Mhe.Stanslaus Nyongo akizungumza na watumishi wa Ofisi ya Afisa Madini Mkazi Mkoa wa Simiyu na baadhi ya viongozi wa Mkoa huo wakati wa Ziara yake mkoani humo.
  

Thursday, December 28, 2017

PROFESA NDALICHAKO: WIZARA YA ELIMU HAINA URASIMU KUSAJILI SHULE IKIWA VIGEZO VIMEZINGATIWA

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amesema Wizara yake haina urasimu wowote katika usajili wa shule ikiwa vigezo vyote vinavyotakiwa vimezingatiwa katika uanzishwaji wa shule hizo.

Waziri Ndalichako ametoa kauli hiyo jana wakati alipokwenda kuweka jiwe la msingi katika Shule Shikizi/tarajali ya Njalu iliyopo Habiya Wilayani Itilima na alipotembelea shule ya Sekondari ya Chegeni inayoendelea kujengwa Kijiji cha Bulima wilayani Busega,  zote zikiwa zinajengwa kwa nguvu ya wananchi.

 “Lengo la Serikali ni kuwa na shule nyingi lakini ni lazima vigezo na masharti yaliyowekwa na Wizara yazingatiwe; Kuna watu ambao siyo waaminifu, zamani ilikuwa hata mtu akiwa na madarasa matatu akiomba usajili anaruhusiwa na shule inasajiliwa lakini wakisharuhusiwa wanabweteka na matokeo yake wanaleta shida kwa watoto wetu” alisema Profesa Ndalichako.

Ameongeza kuwa Wadhibiti ubora wapewe nafasi ya kushiriki katika vikao vya Mabaraza ya madiwani ili waweze kutoa elimu na mwongozo kwa madiwani juu ya mambo muhimu yanayotakiwa kuzingatiwa wanapotaka kuanzisha shule katika maeneo yao na wataalam wa elimu wasaidie katika kutoa elimu juu ya miongozo na vigezo vyote.

Aidha, amewapongeza wananchi wa Habiya Itilima na Bulima Busega kwa kuchangia nguvu na michango yao katika  kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.John Pombe Magufuli kwenye ujenzi wa shule hizo na akawataka wazazi na walezi kuhakikisha watoto wote wenye umri wa kwenda shule wanakwenda wasiwape majukumu mengine.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti Mbunge wa Itilima Mhe.Njalu Silanga na Mbunge wa Busega, Mhe.Dkt.Raphael Chegeni wamesema wananchi katika maeneo zilizopo shule hizo wako tayari kuunga mkono Juhudi za Serikali katika ujenzi wa shule,  hivyo wakaomba watakapokamilisha ujenzi wa miundombinu kulingana na miongozo waliyopewa wasajiliwe shule hizo ili kutoa nafasi kwa watoto kupata mahali pa kujifunzia.

“Mhe.Waziri tunakubali kufuata maelekezo yako na tunaomba tutakapo kamilisha mahitaji tunaomba shule hii iweze kusajiliwa na katika Jimbo langu kuna shule 22 za aina hii ambazo zimejengwa kwa nguvu za wananchi” alisema Njalu Silanga Mbunge wa Itilima.

Pamoja kutoa maelekezo na mwongozo kwa wananchi Mhe. Waziri wa Elimu ameahidi kuchangia ujenzi wa shule hizo kwa kutoa saruji mifuko 100 kwa Shule ya Njalu(Itilima) na Mifuko 150 kwa Shule yaChegeni (Busega) na kuwataka Wakurugenzi wa Halmashauri hizo kuhakikisha kuwa wanatafuta vifaa vingine ili kukamilisha miundombinu inayotakiwa kwa kushirikiana na wananchi.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka amesema Serikali ya Mkoa na Wilaya ya Itilima itachangia  saruji mifuko 100 kwa shule ya Msingi (shikizi) Njalu (Itilima) na Serikali ya Mkoa na Wilaya ya Busega itachangia mifuko 50 kwa Shule ya Sekondari Chegeni(Busega) .

Shule ya Msingi Njalu (Shikizi) hadi sasa ina vyumba vya madarasa vitano, ofisi moja ya walimu  na ina upungufu wa chumba kimoja cha darasa, ofisi ya walimu 01 pamoja na matundu ya vyoo matano (05) na mpaka sasa Mbunge wa Jimbo la Itilima ametoa zaidi ya milioni 26.


Kwa upande wa   Shule ya Sekondari ya Chegeni inayoendelea kujengwa mpaka sasa  ina vyumba viwili vya madarasa, ofisi moja ya walimu, ina upungufu wa vyumba viwili vya madarasa, vyumba vitatu vya maabara, matundu 10 ya vyoo, maktaba, jengo la utawala na nyumba mbili za walimu ambapo hadi sasa Mbunge wa Busega Dkt.Raphael Chegeni ameshangia jumla ya shilingi  milioni 10 katika kuwaunga mkono wananchi. 
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa.Joyce Ndalichako akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Bulima Kata ya Nayashimo Wilayani Busega Mkoa waSimiyu wakati wa ziara yake mkoani humo.
Mbunge wa Jimbo la Busega Mhe.Dkt.Raphael Chegeni akizungumza na wananchi wa Bulima wakati Waziri wa Elimu , Sayansi na Teknolojia Profesa.Joyce Ndalichako alipotembelea shule ya Sekondari inayojengwa kwa nguvu za wananchi ambayo imepewa jina la Mbunge huyo (Chegeni Sekondari) jana.
 Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa.Joyce Ndalichako(kulia) akiweka Jiwe la Msingi Vyumba vya Madarasa  vya Shule ya Msingi iliyojengwa kwa nguvu za wananchi na kupewa jina la Mbunge Njalu(Shule ya msingi Njalu) iliyopo Habiya wilayani Itilima wakati wa ziara yake jana.
Mbunge wa Jimbo la Itilima, Mhe.Njalu Silanga akizungumza katika uwekaji wa Jiwe la Msingi la Vyumba vya Madarasa Shule ya Msingi Njalu (Shule shikizi) iliyoko Habiya wilaya ya Itilima wakati wa Ziara ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa.Joyce Ndalichako wilayani humo jana
Diwani ya Kata ya Nyashimo na Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega akizungumza na wananchi wa Bulima wakati Waziri wa Elimu , Sayansi na Teknolojia Profesa.Joyce Ndalichako alipotembelea shule ya Sekondari inayojengwa kwa nguvu za wananchi ambayo imepewa jina la Mbunge wa Busega Dkt.Raphael Chegeni (Chegeni Sekondari) jana.
Baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Bulima Kata ya Nyashimo wakimsikiliza Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa.Joyce Ndalichako wakati alipopita kuona ujenzi wa shule ya sekondari Chegeni ambayo inajengwa kwa nguvu ya wananchi hao wilayani Busega.
Kutoka kushoto Mkuu wa Wilaya ya Busega, Mhe.Tano Mwera, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa.Joyce Ndalichako, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka, Diwani ya Kata ya Nyashimo na Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega, Mickness Mahela, Mkurugenzi Busega na Kaimu Afisa Elimu Mkoa wa Simiyu wakifurahia jambo wakati wa Ziara ya Waziri wa Elimu wilayani Busega.
Kutoka kushoto Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Mhe.Benson Kilangi, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa.Joyce Ndalichako wakiteta jambo wakati wa ziara ya Mhe.Waziri wa Elimu wilayani Itilima jana.
Kutoka kushoto Mbunge wa Jimbo la Busega Mhe.Dkt.Raphael Chegeni, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa.Joyce Ndalichako, Mkuu wa Wilaya ya Busega, Mhe.Tano Mwera, Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega, Mickness Mahela, Mkurugenzi wa Busega Anderson Njiginya wakifurahia jambo  wakati wa Ziara ya Waziri wa Elimu wilayani Busega.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Habiya mara baada ya kukwa nguvu ya wananchi  katika Shule ya msingi Njalu(Shule shikizi) wakati wa ziara yake wilayani Itilima Mkoa wa Simiyu.

Wednesday, December 27, 2017

UJENZI WA CHUO CHA VETA MKOA WA SIMIYU KUANZA MWEZI MACHI 2018

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako amesema Serikali inatarajia kuanza ujenzi wa Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi(VETA) cha Mkoa wa Simiyu kuanzia mwezi Machi, 2018.

Waziri Ndalichako ameyasema  hayo leo wakati alipokuwa akizungumza na viongozi wa Mkoa wa Simiyu wakati wa ziara yake ya siku moja Mkoani humo.

“Kesho tarehe 28/12/2017 kwenye magazeti kutatoka tangazo la zabuni ya ujenzi wa VETA ya Mkoa wa Simiyu na tunategemea kujenga VETA ya Kisasa itakayohudumia Mkoa na inayoendana na mahitaji ya sasa; tukitangaza zabuni kesho itachukua siku 30 kupokea zabuni unahitajika mwezi mmoja kufanya tathmini, nawaahidi kuwa ujenzi utaanza mwezi Machi” alifafanua Profesa Ndalichako.

Ameongeza kuwa Serikali ya Awamu ya Tano ambayo inasisitiza juu ya ujenzi wa Uchumi wa Viwanda inatambua umuhimu wa Vyuo vya Mafunzo ya Ufundi Stadi ndiyo maana imejipanga kujenga vyuo hivyo pamoja na kuimarisha Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi.

Aidha, Profesa Ndalichako amepongeza ongezeko la wanafunzi walioandikishwa kuanza darasa la kwanza Mkoani Simiyu na akasisitiza kuwa Wizara ya Elimu ambayo ndiyo inayotunga Sera itahakikisha inasimamia kikamilifu ili  wanafunzi wote wanaoanza darasa la kwanza wamalize masoma yao.

Amesema ongezeko hilo ambalo limesababishwa na mwamko chanya wa wazazi baada ya kuanza kutekelezwa kwa  mpango wa elimu bila malipo limepelekea upungufu wa miundombinu shule na ndiyo maana Serikali kuu inashirikiana na Halmashauri pamoja na wananchi katika ujenzi wa miundombinu ili kukabiliana na upungufu kupitia Mradi wa Lipa kulingana na Matokeo(P4R).

“Kupitia mradi wa Lipa kulingana na Matokeo tumeshajenga jumla ya vyumba vya madarasa 1104, matundu ya vyoo 3396, mabweni 261. Tunaendelea pia kuimarisha miundombinu katika sekta ya elimu kwa ujumla, kwa maana ya ukarabati katika vyuo vya Ualimu ambapo tumeshakarabati vyuo 17 na shule kongwe 46 kati ya shule 88 zimeshakarabatiwa” alisema Waziri.

Profesa Ndalichako amepongeza Uongozi wa Wilaya ya Itilima kwa kutumia vizuri jumla ya shilingi bilioni 2.177 za Mradi wa Lipa Kulingana na matokeo(P4R) ambazo zimetumka kujenga vyumba vya madarasa, mabweni na matundu ya vyoo  wilayani humo.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe.Anthony Mtaka amesema katika kipindi cha mwaka 2018-2020 Mkoa huo umejiwekea mpango wa kujenga mabweni kwa wanafunzi wa kike katika kila shule ili kuwaondolea adha ya kutembea mwendo mrefu na changamoto nyingine.

Akimshukuru Waziri wa Elimu kwa kupeleka fedha za Mradi wa Lipa kulingana na matokeo (P4R) katika Wilaya ya Itilima ambazo zimesaidia upatikanaji wa Mbunge wa Jimbo la Itilima Mhe.Njalu Silanga amesema Wilaya hiyo imetekelezaji wa mradi huo kwa kufuata taratibu na miongozo yote  ya Serikali kwa kushirikiana na wananchi.

Hii ni ziara ya kwanza kwa Waziri Ndalichako Mkoani Simiyu ambayo imempa nafasi ya kutembelea, kuweka mawe ya msingi, kukagua na kufungua vyumba vya madarasa, mabweni katika maeneo tofauti Wilayani Itilima ikiwemo Kijiji cha Habiya, Lagangabilili, Itilima, Mahembe na baadaye kufanya mkutano wa hadhara katika kata ya Luguru.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Lagangabilili mara baada ya kufungua vyumba vya madarasa vilivyojengwa kupitia Mradi wa Lipa Kulingana na Matokeo (P4R) katika Shule ya msingi Lagangabilili wilayani Itilima Mkoa wa Simiyu.  
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako(kulia) akiweka Jiwe la Msingi katika Mabweni ya Wasichana yaliyojengwa kupitia Mradi wa Lipa Kulingana na Matokeo (P4R) katika Shule ya Sekondari Itilima wilayani Itilima Mkoa wa Simiyu,(kushoto) Mkuu wa Mkoa huo, mhe Anthony Mtaka.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako( wa tatu kushoto) na baadhi ya viongozi wa Wilaya ya Itilima na Mkoa wa Simiyu wakielekea kukagua vyumba vya madarasa katika Shule ya Sekondari Lagangabili, wakati wa ziara yake mkoani humo.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako(kushoto) akipokea maelezo kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Mhe.Benson Kilangi (kulia) wakati akikagua vyumba vya madarasa katika Shule ya Sekondari Lagangabili, wakati wa ziara yake mkoani Simiyu.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako(aliyekaa) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa Wilaya ya Itilima na Mkoa wa Simiyu mara baada ya kukagua vyumba vya madarasa vilivyojengwa kupitia Mradi wa Lipa Kulingana na Matokeo(P4R) katika Shule ya Sekondari Lagangabilili wilayani Itilima.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako(kulia) akisaini kitabu cha Wageni katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu mara baada ya kuwasili mkoani kwa ajili ya ziara ya siku moja(katikati) Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka(kushoto) Katibu Tawala Mkoa, Ndg.Jumanne Sagini.

Mbunge wa Itilima, Mhe.Njalu Silanga(kulia) akizungumza jambo wakati wa Ziara ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako (kushoto) aliyoifanya wilayani Itilima.
Baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Habiya na Wanafunzi wa Shule tarajali/shikizi ya Njalu iliyopo wilayani Itilima mkoani Simiyu, wakimsikiliza Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako(hayupo pichani) wakati wa ziara yake wilayani humo.
Baadhi ya Viongozi wa Wilaya ya Itilima na Mkoa wa Simiyu wakifurahia jambo wakati ziara ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako(hayupo pichani) mkoani humo.
:- Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako akizungumza na wananchi wa Kata ya Luguru wilayani Itilima (hawapo pichani) wakati wa Ziara yake mkoani Simiyu.
Vijana wa Skauti wilaya ya Itilima wakivisha Skafu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako mara baada ya kuwasili wilayani humo kwa ziara ya siku moja.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako akipokelewa na viongozi wa Wilaya ya Itilima mara baada ya kuwasili wilayani humo kwa ziara ya siku moja.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa. Joyce Ndalichako(mbele kushoto) akiwa na baadhi ya viongozi wa Wilaya ya Itilima na Mkoa wa Simiyu mara baada ya kukagua jengo la Bweni linalojengwa kwa ya wanafunzi wa kidato cha Tano na sita watakapoanza kusoma shuleni hapo

Friday, December 8, 2017

WANAFUNZI 19,242 WACHAGULIWA KUJIUNGA KIDATO CHA KWANZA MWAKA 2018 SIMIYU

Jumla ya wanafunzi 19,242 mkoani Simiyu sawa na asilimia 92.5 wamechaguliwa kujiunga na shule za sekondari katika awamu ya kwanza kwa mwaka 2018.

Hayo yamesemwa na Katibu Tawala wa Mkoa huo, Ndg.Jumanne Sagini katika kikao cha kutangaza matokeo ya uchaguzi wa wanafunzi wa kidato cha  kwanza mwaka 2018 kilichofanyika leo Mjini Bariadi.

Sagini amesema jumla ya wanafunzi 20,818 sawa na asilimia 67.73 ya wanafunzi waliofanya mtihani wa darasa la saba walifaulu, ambapo kati yao 1576 sawa na asilimia 7.5 ya waliofaulu hawakupata nafasi ya kuanza kidato cha kwanza kutokana na uhaba wa vyumba vya madarasa na madawati katika baadhi ya Halmashauri.

“Wanafunzi waliokosa nafasi Halmashauri ya Mji wa Bariadi ni wale waliopaswa kwenda Shule ya Sekondari Kidinda(207) na Biashara(162), Halmashauri ya Wilaya ya Busega walipaswa kwenda shule za Lamadi (486), Nasa (358) na Sogesca (363). Ni wajibu wa Halmashauri hizi kushirikiana na wananchi kuhakikisha miundombinu pungufu imekamilishwa haraka ili ifikapo Februari 15, 2018  wanafunzi hao waripoti kwenye shule walizopaswa kwenda” amefafanua Sagini.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega na Halmashauri ya Mji Bariadi wamesema Halmashauri zao zinaendelea na ujenzi wa vyumba vya madarasa katika shule hizo na wataendelea kufanya jitihada mbalimbali kwa kushirikiana na wananchi kuhakikisha kuwa miundombinu hiyo pungufu inakamilika haraka, ili kufikia Februari 05 mwakani wanafunzi wote waliokosa nafasi awamu ya kwanza waweze kwenda shule.

Wakati huo huo Sagini amezitaka Halmashauri kuendelea kushirikiana na wadau wote wa elimu kukamilisha majengo na kuandaa mazingira ya kuwapokea wanafunzi wote waliochaguliwa kuanza kidato cha kwanza mwaka 2018 bila vikwazo vya aina yoyote.

Ameongeza kuwa wazazi, walezi na jamii kwa ujumla washirikiane na uongozi wa wilaya, halmashauri na shule  kuhakikisha kwamba wanafunzi wote waliochaguliwa wanaandikishwa, wanaripoti shuleni na kuendelea na masomo yao kwa bidii hadi watakapomaliza elimu yao ya sekondari mwaka 2021.

Akielezea hali ya ufaulu kwa wanafunzi wa darasa la saba  kwa mwaka 2017, Afisa Elimu Mkoa, Mwl. Julius Nestory amesema kwa mara ya kwanza mwanafunzi aliyeongoza katika Mkoa ambaye ni (msichana) Hoka Lyaganda Saguda ametoka katika Shule ya Serikali ambayo ni Shule ya Msingi Sima B iliyopo Mjini Bariadi.

Amesema ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa elimu na kuinua kiwango cha ufaulu mkoani humo Mikakati ya kuinua ufaulu ya kila wilaya isimamiwe kikamilifu,  Ofisi za Wilaya, Halmashauri, Kata na Wakuu wa Shule zifanye ufuatiliaji kuhusu ufundishaji na ujifunzaji na  Ukaguzi wa shule ufanyike kwa kiwango kisichopungua asilimia 50 kwa mwaka na Wakurugenzi watenge fedha kwa ajili ya ukaguzi wa shule.

Naye Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Itilima, Mhe.Mahamoud Mabula ameshauri kuwa ili kuinua ufaulu suala la maendeleo ya Elimu liwe agenda ya kudumu katika vikao vyote muhimu vya Halmashauri mkoani humo, ili kutoa nafasi ya kujadili changamoto mbalimbali za sekta ya elimu na kuzitafutia ufumbuzi.


Idadi ya wanafunzi waliochaguliwa kujiunga kidato cha kwanza mwaka 2018 Mkoani Simiyu imeongezeka kutoka wanafunzi 16,620 mwaka 2017 hadi wanafunzi 19,242.
Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg. Jumanne Sagini akifungua kikao cha kutangaza matokeo ya Uchaguzi wa Wanafunzi wa Kujiunga Kidato cha Kwanza mwaka 2018 Mkoani humo, kilichofanyika leo Mjini Bariadi.
Afisa Elimu Mkoa, Mwl. Julius Nestory akiwasilisha taarifa ya hali ya ufaulu wa wanafunzi wa darasa la saba kwa mwaka 2017, katika  kikao cha kutangaza matokeo ya Uchaguzi wa Wanafunzi wa Kujiunga Kidato cha Kwanza mwaka 2018 Mkoani Simiyu, kilichofanyika leo Mjini Bariadi.
Mkuu wa Wiayaya Bariadi, Mhe.Festo Kiswaga akichangia hoja katika katika  kikao cha kutangaza matokeo ya Uchaguzi wa Wanafunzi wa Kujiunga Kidato cha Kwanza mwaka 2018 Mkoani Simiyu, kilichofanyika Mjini Bariadi.
Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Meatu, Mhe.Juma Mwiburi akichangia hoja katika  kikao cha kutangaza matokeo ya Uchaguzi wa Wanafunzi wa Kujiunga Kidato cha Kwanza mwaka 2018 Mkoani Simiyu, kilichofanyika leo Mjini Bariadi.
Mkuu wa Wilaya ya Busega, Mhe.Tano Mwera akichangia hoja katika  kikao cha kutangaza matokeo ya Uchaguzi wa Wanafunzi wa Kujiunga Kidato cha Kwanza mwaka 2018 Mkoani Simiyu, kilichofanyika leo  Mjini Bariadi.
Katibu Tawala Wilaya ya Meatu, Veronica Kinyemi akichangia hoja katika  kikao cha kutangaza matokeo ya Uchaguzi wa Wanafunzi wa Kujiunga Kidato cha Kwanza mwaka 2018 Mkoani Simiyu, kilichofanyika leo  Mjini Bariadi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega, Ndg.Anderson Njiginya, akichangia hoja katika  kikao cha kutangaza matokeo ya Uchaguzi wa Wanafunzi wa Kujiunga Kidato cha Kwanza mwaka 2018 Mkoani Simiyu, kilichofanyika leo Mjini Bariadi.
Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Maswa, Mhandisi Paul Jidayi akichangia hoja katika  kikao cha kutangaza matokeo ya Uchaguzi wa Wanafunzi wa Kujiunga Kidato cha Kwanza mwaka 2018 Mkoani Simiyu, kilichofanyika leo Mjini Bariadi.
Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Itilima, Mahamoud Mabula akichangia hoja katika  kikao cha kutangaza matokeo ya Uchaguzi wa Wanafunzi wa Kujiunga Kidato cha Kwanza mwaka 2018 Mkoaani Simiyu, kilichofanyika leo Mjini Bariadi.
Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Mhe.Benson Kilangi akichangia hoja katika  kikao cha kutangaza matokeo ya Uchaguzi wa Wanafunzi wa Kujiunga Kidato cha Kwanza mwaka 2018 Mkoani Simiyu, kilichofanyika leo Mjini Bariadi.
Mkurugenzi wa Mji wa Bariadi, Ndg.Melkezedeck Humbe akichangia hoja katika  kikao cha kutangaza matokeo ya Uchaguzi wa Wanafunzi wa Kujiunga Kidato cha Kwanza mwaka 2018, Mkoani Simiyu kilichofanyika leo Mjini Bariadi.
Baadhi ya Wajumbe wa Kikao cha Kamati ya kutangaza matokeo ya Uchaguzi wa wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2018 mkoani Simiyu, kilichofanyika leo Mjini Bariadi

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!