Thursday, March 29, 2018

SIMIYU, TANTRADE KUSHIRIKIANA KUANDAA MAONESHO YA WAKULIMA NANENANE KITAIFA MWAKA 2018



Mkoa wa Simiyu na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania(TanTrade) wamesema watashirikiana kwa pamoja kuandaa Maonesho ya Kilimo NaneNane mwaka 2018 ambayo Kitaifa  yatafanyika Mkoa wa Simiyu.

Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) Bw. Edwin Rutageruka katika Mkutano wao na Waandishi wa Habari uliofanyika katika makao makuu ya Mamlaka hiyo Jijini Dar es Salaam.

Akiongea na waandishi wa habari Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amesema kuwa Mkoa utatoa dira ya kuyafanya Maonesho ya Kilimo NaneNane kuwa ni Maonesho ya Kilimo Biashara ili Watanzania wapate fursa ya kuona teknolojia mbalimbali kwenye eneo la kilimo, mifugo na uvuvi.

“Sisi kama Mkoa tungehitaji tutoe dira ya kuyafanya maonesho ya Wakulima NaneNane yawe ni maonesho ya Kilimo Biashara, mahali ambapo Watanzania watapata Fursa ya kuona teknolojia mbalimbali kwenye eneo la Kilimo, eneo la mifugo, eneo la uvuvi na yote haya yabebebwe na dhana ya Kilimo Biashara” alisema Mtaka

“Matarajio yetu kama mkoa kwa kushirikiana na TanTrade ni kuona kwamba tunaingiza Maonesho ya Kilimo NaneNane kuwa tukio ambalo litawakaribisha watu wenye teknolojia mbalimbali Kitaifa na Kimataifa kwenye kuwezesha mageuzi ya kilimo,uvuvi na ufugaji wa nchi kwa kuonesha ni kwa namna gani wanaweza kumfikia mkulima, mvuvi na mfugaji kwenye teknolojia ya kisasa ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi ili Maonesho ya Kilimo NaneNane yawekwe kwenye ramani ya dunia” alisisitiza  Mtaka

Aidha, Mtaka ameziomba Balozi za Tanzania katika nchi mbalimbali kuyatangaza Maonesho haya kwa kuyatumia kukaribisha makampuni yenye teknolojia kuja kuonesha mkoani Simiyu na akatumia fursa hiyo kuwakaribisha wawekezaji kwa makundi yote kutoka ndani na nje ya nchi kuja kuwekeza katika eneo litakalofanyika Maonesho ya Kilimo Biashara ili uwekezaji huo uendane na viwango vya Kimataifa.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) Bw. Edwin Rutageruka ameeleza kuwa Mkoa wa Simiyu na TanTrade wamekubaliana kuwa na maonesho endelevu ya Kisekta katika Mkoa wa Simiyu

Rutageruka ameongeza kuwa TanTrade ni taasisi pekee iliyopewa jukumu la kusimamia masuala ya Maonesho ndani na nje ya nchi kisheria, hivyo kutokana na uzoefu wa uandaaji wa Maonesho mbalimbali,  kwa mwaka 2018 Maonesho ya Kilimo Biashara yatakuwa ni Maonesho bora kwasababu watawaandaa washiriki wote Kisekta,  kuweka miundo mbinu ya kisasa na kuyafanya Maonesho haya kuwa ya Kimataifa.

“Mkoa wa Simiyu una kiu ya kuona Maonesho ya Kilimo Biashara  yanakuwa ya kisasa  kama ilivyo Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam ambayo kwa Afrika Mashariki ndiyo Maonesho yanayoongoza kwa ubora na Maonesho haya ya Kilimo tutayafikisha huko” aliongeza Bw Rutageruka.

Hivi karibu Serikali imetangaza Kanda Mpya ya Maonesho ya Kilimo na Sherehe za Wakulima NaneNane  inayojumuisha mikoa ya Simiyu, Mara na Shinyanga ambayo inatambulika kama Kanda ya Ziwa Mashariki na Maonesho hayo kwa kanda hiyo  yatakuwa yanafanyika Mkoani Simiyu.
 
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka (kushoto) akizungumza na Waandishi wa Habari katika Makao Makuu  ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) jijini Dar es Salaam juu ya Maonesho ya Kilimo na Sherehe za Wakulima NaneNane yanayotarajiwa kufanyika Kitaifa Mkoani humo mwaka 2018, (kulia) Mkurugenzi Mkuu Mamlaka hiyo, Bw. Edwin Rutageruka.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!