Sunday, November 17, 2019

WADAU WA ELIMU TIMIZENI WAJIBU SIMIYU IENDELEE KUNG'ARA KIELIMU: RAS SIMIYU

Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini ametoa wito kwa viongozi, wataalam wa Elimu, jamii na wadau wote wa elimu kila mmoja kutimiza wajibu wake, ili mkoa wa Simiyu uendelee kufanya ya vizuri kielimu na uwe miongoni mwa mikoa mitatu bora inayofanya vizuri katika ufaulu wa mitihani yote ya Taifa.


Sagini ameyasema hayo Novemba 16, 2019 wakati akizungumza na viongozi, wataalam na wadau wengine wa elimu mkoani Simiyu katika kikao cha kutangaza mkakati wa kuboresha taaluma mwaka 2020  kilichofanyika Mjini Bariadi.

"Tukitoka hapa kila mtu akitimiza wajibu wake nina uhakika tutautekeleza mkakati huu wa kuboresha taaluma, matarajio yetu ni kusonga mbele si kurudi nyuma, dhamira yetu iwe kuwa namba moja, mbili na tatu," alisema Sagini.

Aidha, Sagini amesema ni vema walimu wakaboresha mfumo wa ufundishaji kwa wanafunzi wao ambao utawaandaa kwa umahiri katika mitihani yao ikiwa ni pamoja na kuwapa majaribio na mitihani ya mara kwa mara.

Afisa Elimu wa Mkoa wa Simiyu, Mwl. Ernest Hinju amesema azma ya viongozi, wataalam na wadau wa elimu mkoa wa Simiyu ni kuufanya mkoa kuwa miongoni mwa mikoa yenye mafanikio kielimu, ambapo azma  hii imeonekana kutimizwa kupitia matokeo ya mitihani ya Kitaifa ya mwaka 2017, 2018 na 2019 ambayo ufaulu wake ulikuwa mzuri.

"Kidato cha nne 2017 mkoa ulikuwa wa 11 kati ya mikoa 31 mwaka 2018 ukawa wa 9 kati ya mikoa 31; kidato cha sita mwaka 2018 mkoa ulikuwa wa 10 na mwaka 2019 umeshika nafasi hiyo hiyo ya 10 kati ya mikoa 31, darasa la saba mwaka 2018 mkoa ulikuwa wa 22 na mwaka 2019 mkoa umeshika nafasi ya 8 kati ya mikoa 31 na ufaulu umekuwa ukipanda pia kila mwaka," alisema Hinju.

Naye Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Simiyu, Mhe. Enock Yakobo amewapongeza walimu kwa kazi nzuri wanayofanya ambayo imechangia kwa kiasi kikubwa kuongeza ufaulu na kuuweka
mkoa katika nafasi nzuri kielimu.

Mwl. Milembe Mange kutoka Shule ya Msingi Sangida Bariadi amesema,  Mkakati wa taaluma umetoa dira katika maeneo mengi ya kuboresha elimu ikiwemo ushirikishaji wadau hususani wazazi, ambapo kupitia ushirikishwaji huo, wazazi wataendelea kushirikishwa katika kuchangia ujenzi wa madarasa yatakayosaidia kupunguza idadi ya wanafunzi darasani na kuboresha mazingira ya kujifunzia.

Kwa upande wake, Mdhibiti Ubora wa Shule katika Halmashauri ya Mji wa Bariadi, Mwl. John Magwila amesema wadhibiti ubora wote wa Mkoa wa Simiyu watahakikisha wanakagua katika shule zote kujiridhisha utekelezaji wa masuala yote muhimu yaliyoainishwa katika mkakati wa kuboresha taaluma, ili kufikia lengo la kuongeza ufaulu na kuufikisha mkoa katika nafasi tatu bora kitaifa kwenye mitihani yote ya Kitaifa.

Mkakati huu Simiyu umezingatia vipaumbele kadhaa baadhi ya hivyo ni uwajibikaji wa maafisa elimu kata na mfumo mzima wa utawala, huduma bora na mawasiliano kubalika kwa walimu na wadau wa elimu, utoaji wa motisha na zawadi kwa wadau wanaofanya vizuri, ufuatiliaji kambambe wa ufundishaji na ujifunzaji,  upimaji, mafunzo kazini na kambi za kitaaluma.
MWISHO



Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini akizungumza na viongozi na wataalam wa elimu kuanzia ngazi ya shule, kata, wilaya na Mkoa pamoja na wadau  wengine mkoani Simiyu katika kikao cha kutangaza mkakati wa kuboresha Taaluma mwaka 2020 Mkoa wa Simiyu, kilichofanyika Novemba 16, 2019 Mjini Bariadi.
 Baadhi ya viongozi na wataalam wa elimu kuanzia ngazi ya shule, kata, wilaya na Mkoa pamoja na wadau  wengine  wa elimu mkoani Simiyu, wakimsikiliza Karibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini wakati akifungua kikao cha kutangaza mkakati wa kuboresha Taaluma mwaka 2020 Mkoa wa Simiyu, kilichofanyika Novemba 16, 2019 Mjini Bariadi.

Afisa Elimu wa Mkoa wa Simiyu, Mwl. Ernest Hinju akiwasilisha taarifa ya Maendeleo ya Elimu mkoani humo, katika kikao cha kutangaza mkakati wa kuboresha Taaluma mwaka 2020 Mkoa wa Simiyu , kilichofanyika Novemba 16, 2019 Mjini Bariadi.




Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Simiyu, Mhe. Enock Yakobo akizungumza na viongozi na wataalam wa elimu kuanzia ngazi ya shule, kata, wilaya na Mkoa pamoja na wadau  wengine mkoani Simiyu katika kikao cha kutangaza mkakati wa Mkoa wa kuboresha Taaluma mwaka 2020, kilichofanyika Novemba 16, 2019 Mjini Bariadi.



Baadhi ya viongozi na wataalam wa elimu kuanzia ngazi ya shule, kata, wilaya na Mkoa pamoja na wadau  wengine  wa elimu mkoani Simiyu, wakimsikiliza Karibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini wakati akifungua kikao cha kutangaza mkakati wa kuboresha Taaluma mwaka 2020, kilichofanyika Novemba 16, 2019 Mjini Bariadi.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!