Saturday, May 8, 2021

TMDA YATOA MSAADA TAULO ZA KIKE ZENYE THAMANI YA SHILINGI MILIONI 6 SIMIYU

Mamlaka ya Dawa na Vifaa tiba (TMDA) imetoa msaada wa taulo za kike zenye thamani ya shilingi milioni 6 lengo likiwa kuunga mkono maandalizi ya kambi za kitaaluma kwa wanafunzi wa kidato cha nne zinazotarajiwa kuanza mwenzi Agosti, 2021 mkoani Simiyu. 

Akikabidhi taulo hizo meneja wa TMDA kanda ya ziwa Sofia Mziray amesema msaada huo ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za serikali katika elimu ambayo ni kipaumbe cha mkoa wa Simiyu huku akiwataka amewataka wanafunzi kusoma kwa bidii ili lengo la mkoa huo ya kushika  nafasi ya kwanza  kitaifa. 

“Tumetoa msaada huu kuunga mkono serikali ya mkoa lakini pia tumeona tuwasaidie watoto wa kike waweze kuwepo wakati wote shule, tunataka kusiwe na kisingizio chochote mtoto wa kike kushindwa kuwepo shuleni katika kipindi fulani cha mwezi, sehemu yetu tumefanya tumewaachia ninyi, wito wangu kwenu msome kwa bidii mtimize malengo ya mkoa,” alisema Mziray. 

Naye Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka ameishukuru TMDA kwa msaada huo kuku akitoa rai kwa wazazi kutowatuma wanafunzi katika minada kwa lengo la kuuza bidhaa mbalimbali badala yake kila mzazi aone umuhimu wa elimu na kuifanya elimu kuwa kipaumbele chake kwa kuhakikisha watoto wanahudhuria masomo. 

Aidha, Mtaka amesisitiza wazazi wenye watoto walio katika madarasa ya mitihani kuwapunguzia kazi ili waweze kupata muda mwingi wa kujisomea kwa ajili ya maandalizi ya mitihani ya Taifa kwa lengo la kufikia azma ya mkoa ya kushika nafasi ya kwanza katika mitihani yote ya Kitaifa.

 

 

Afisa Elimu mkoa wa Simiyu, Mwl. Ernest Hinju amesema misaada inayoendelea kutolewa na wadau mbalimbali wakiwemo TMDA inarahisisha kazi kwa wataalamu wa elimu wanaokuwa na wanafunzi katika kambi za kitaaluma na inachangia kuongeza ari ya kusoma kwa wanafunzi na hivyo kuwawezesha kufanya vizuri katika mitihani yao. 

Hinju ameomngeza kuwa maandalizi ya kambi za kitaaluma  kwa wanafunzi wa kidato cha nne mkoani hapo zinazotarajia kuanza Agosti, 2021 yameshaanza. 

Akiongea kwa niaba ya wanafunzi wa kike Jackline Sonda amewashukuru TMDA kwa msaada wataulo za kike na amesema wameupokea msaada huo  kwa mikono miwili huku akiahidi kuwa watasoma kwa bidii kwani miongoni mwa sababu iliyokuwa ikiwafanya baadhi ya wasichana wasihudhurie kikamilifu siku zilizopangwa za kuwepo darasani tayari imepatiwa ufumbuzi.

MWISHO

Baadhi ya wanafunzi wa kike wa Shule ya Sekondari Simiyu wakipokea msaada wa taulo za kike kutoka TMDA, wengine ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka(katikati ya waanfunzi), Kaimu Meneja wa TMDA Kanda ya Ziwa, Bi. Sophia Mziray (mwenye skafu) na viongozi wengine wa mkoa wa Simiyu. Makabidhiano hayo yamefanyika Mei 7, katika Shule ya Sekondari Simiyu.

TAZAMA PICHA MBALIMBALI KATIKA TUKIO HILO












 

WAZAZI WENYE WATOTO WALIO MADARASA YA MITIHANI WAPUNGUZIENI KAZI: RC MTAKA

 Mkuu wa mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka ametoa rai kwa wazazi na walezi wenye watoto walio katika madarasa ya mitihani ya Taifa kuwapunguzia kazi ili wanafunzi hao waweze kupata muda wa kujiandaa na mitihani hiyo na hatimaye waweze kufanya vizuri katika mitihani yao. 

Mtaka ameyasema hayo Mei 06, 2021 Mjini Bariadi wakati wa futari maalum iliyoandaliwa na ofisi yake kwa ajili ya waumini wa dini na Kiislamu walio katika mwezi mtukufu wa Ramadhani ambayo pia iliwahusisha viongozi na watendaji mbalimbali wa Serikali mkoani  Simiyu.

“Matarajio yangu ni kuhakikisha kuwa mkoa huu unabaki kuwa miongoni mwa mikoa mitano inayofanya vizuri kwenye elimu nchini, kwenye malengo yetu ya mwaka huu ni kuona tunatoka kwenye nafasi ya tano, kwenda nafasi ya tatu na kufikia nafasi ya kwanza ili kufikia hapo tuna kazi ya kufanya; niwaombe wazazi na walezi wote wa mkoa wa Simiyu wenye watoto wa madarasa ya mitihani wawapunguzie kazi ili wapate muda wa kujisomea na kufanya matayarisho ya mitihani yao ya Taifa,” alisema Mtaka.

Aidha, Mtaka amewataka wazazi kutowaruhusu wanafunzi kwenda katika minada kufanya biashara badala yake wahakikishe wanafunzi wote wanahudhuria masomo, “ Hii habari ya kuona watoto (wanafunzi) minadani hapana, kila mmoja awe mzazi na mlezi minada ni kwa ajili ya wazazi kufanya biashara siyo mahala kwa watoto kupeleka bidhaa maana minada yetu mingi inafanyika siku za kazi”

Kwa upande wake Sheikh wa Mkoa wa Simiyu Mahamudu Kalokola amemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Simiyu kwa futari na kushiriki katika shughuli mbalimbali zinasowahusu Waislamu ikiwa ni pamoja na kushiriki katika ujenzi wa msikiti mkuu wa Bariadi , huku akiwataka Waislamu wote mkoani Simiyu kuendelea kuiombea nchi na kudumisha amani iliyopo.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Amani ya mkoa wa Simiyu,Askofu Marco Maduhu ametoa rai kwa wananchi mkoani Simiyu kuendelea kushirikiana na kuthaminiana bila kujali tofauti za dini zao.

Naye Katibu wa CCM mkoa wa Simiyu, Bi. Haula Kachwamba amewatakia heri Waislamu wote walio katika mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani na kuwaombea waweze kumaliza mfungo huo salama.

MWISHO

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akizungumza na baadhi ya waislamu, viongozi na wananchi wa mkoa wa Simiyu, Mei 06, 2021 Mjini Bariadi katika futari maalum aliyoiandaa kwa ajili ya Waislamu waliofunga na baadhi ya makundi ya watu mkoani hapa.

Baadhi ya Waislamu wakiwa katika hafla maalum ya futari Mei 06, 2021 Mjini Bariadi, iliyoandaliwa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka  kwa ajili ya Waislamu waliofunga na baadhi ya makundi ya watu mkoani hapa.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka( wa pili kulia) akisalimiana na Sheikh wa Mkoa wa Simiyu Mahamudu Kalokola Mei 06, 2021 Mjini Bariadi katika futari maalum aliyoiandaa kwa ajili ya Waislamu waliofunga na baadhi ya makundi ya watu mkoani hapa.

Muimbaji maarufu wa Kaswida Bi. Arafa Abdillah Salum akiimba katika hafla maalum ya futari Mei 06, 2021 Mjini Bariadi, iliyoandaliwa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka  kwa ajili ya Waislamu waliofunga na baadhi ya makundi ya watu mkoani hapa.



TAZAMA PICHA MBALIMBALI KATIKA HAFLA MAALUM YA FUTARI MEI 06, 2021 MJINI BARIADI, ILIYOANDALIWA NA MKUU WA MKOA WA SIMIYU, MHE. ANTHONY MTAKA  KWA AJILI YA WAISLAMU WALIOFUNGA NA BAADHI YA MAKUNDI YA WATU MKOANI HAPA. 













 

USIMAMIZI WA TMDA, ELIMU KWA UMMA ZATAJWA KUSAIDIA KUPUNGUZA BIDHAA BANDIA SOKONI

 Usimamizi shirikishi, elimu kwa umma zimetajwa kuwa ni miongozi mwa sababu zilizochangia kupunguza uwepo wa dawa bandia katika mikoa ya kanda ya ziwa, jambo ambalo limechangia soko la bidhaa hizo (dawa) kuwa soko salama. 

Hayo yamebainishwa na Kaimu Meneja wa Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba, Bi. Sophia Mziray Mei 06, 2021 wakati akizungumza katika ufunguzi wa kikao kazi cha wataalam wa afya na mifugo pamoja na wakaguzi wa dawa , kilichofanyika Mjini Bariadi Mkoani Simiyu.

“Tumeza kulisimamia vizuri soko hili la kanda ya ziwa siyo kama miaka ile ya nyuma kwa sasa hivi soko hili naweza kusema ni soko salama kwa bidhaa hizi, hata zikikutwa sokoni ni chache sana, pamoja na hilo tunawaeleimisha wananchi, suala la udhibiti siyo la taasisi tu, hata wananchi ni wadau wakubwa katika udhibiti na huwa tunapata taarifa kutoka kwa rai wema juu ya wafanyabiashara wasio waaminifu wanaofanya biashara haramu za dawa, tumewabaini na tumewachukulia hatua,” alisema Mziray.

Akifungua kikao kazi hicho Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa, Bw. Ekwabi Mujungu amesema kufanya kazi bila taarifa (kumbukumbu) ni tatizo ambalo linahitaji ufumbuzi wa haraka huku akiwataka kupitia kikao kazi hicho kuja na suluhisho la kudumu.

“Mnaohusika si lazima mpaka watu  watoke Dar es salaam kuja kuona dawa bandia fanyeni kazi kwa viapo vyenu,” alisema Mujungu

Kwa upande wao baadhi ya washiriki wa kikao kazi hicho wameishukuru TMDA kutoa mafunzo ambayo yatawaongezea maarifa na kuwawezesha kutekeleza majukumu yao hususani ya ukaguzi kwa ufanisi.

“Elimu niliyoipata leo itanisaidia sana katika kufanya kaguzi mbalimbali pia imenisaidia kujua kuwa ni jukumu letu wataalam kuwapa elimu wamiliki wa maduka ili wauze bidhaa zilizosajiliwa na wajenge utamaduni wa kukagua bidhaa zao (dawa) na kubaini dawa zilizoisha muda wake ili watumiaji wa mwisho au walaji wasiumizwe kwa kuuziwa dawa zisizofaa” alisema Linah Kirumbi Daktari wa Mifugo Halmashauri ya Mji wa Bariadi.

MWISHO





RC MTAKA ASHAURI PPRA KUFANYA TATHMINI YA MIRADI ILIYOTEKELEZWA KWA ‘FORCE ACCOUNT’

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka ametoa rai kwa Mamlaka ya Udhibiti wa Ununuzi wa Umma(PPRA) kufanya tathmini ya miradi iliyotekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano kupitia mfumo wa ‘Force Account’ (Mfumo usiotumia wakandarasi/ wakandarasi katika ujenzi) na baadaye ije na usahauri kwa serikali juu ya namna ya kuboresha matumizi ya mfumo huo hususani katika suala la ubora. 

Mtaka ametoa rai hiyo jana Mei 06, 2021 wakati akifungua mafunzo yaliyoandaliwa na mamlaka hiyo yakiwashirikisha wataalam wa Ununuzi na ugavi, maafisa masuuli na baadhi ya watendaji ili kuwajengea uwezo ili waweze kufanya kazi ya ununuzi wa umma kwa ufanisi ambayo yamefanyika Mjini Bariadi.

“Tusije tukawa na miradi hapa lakini miaka kumi inayokuja tukajikuta kwenye tatizo kubwa, kwa hiyo PPRA ije na ushauri kwa miaka mitano ya ‘Force Account’ pengine mfumo huo ni mzuri zaidi kwenye ujenzi wa miradi ya aina gani,” alisema Mtaka.

Kwa upande wake Afisa mtendaji Mkuu wa PPRA, Mhandisi. Leonard Kapongo amesema katika mafunzo hayo wataalam hao watapata naasi ya kujifunza zaidi kuhusu mfumo huo, utekelezaji wake na ikiwa kuna changamoto walizozibaini wakati wa utekelezaji wa miradi kwenye maeneo yao ili zijadiliwe kwa pamoja na kubainisha kuwa PPRA iko tayari kupokea ushauri.

Aidha, Mhandisi Kapongo amesema wameamua kutoa mafunzo ya masuala ya ununuzi wa ummakwa wataalam hao kwa lengo la kuwafundisho Sheria ya Ununuzi wa Umma ya mwaka sura namba 410 ambayo ni sheria mama ya mwaka 2010 pamoja na marekebisho yake ya mwaka 2016 ili waweze kufanya kazi za ununuzi kwa ufanisi.

Mhandisi Mpongo amesema pamoja na mkoa wa Simiyu mafunzo hayo yameshatolewa katika mikoa mingine  14 ambayo ni Ruvuma, Njombe, Iringa, Kagera, Shinyanga, Kigoma, Geita, Rukwa, Katavi, Tabora, Mbeya, Songwe, Dodoma na Mara.

 

Naye Mkurugenzi wa Kujenga Uwezo na ushauri wa PPRA, Mhandisi Mary Swai amesema mafunzo hayo yatawasaidia wataalam kuzingatia sheria ya ununuzi wa umma na kuzingatia taratibu katika ununuzi ikiwa ni pamoja na kusimamia mfumo wa ‘force account’ waweze kuhakikisha ubora unaotakiwa unapatikana na thamani ya fedha inaonekana.

MWISHO













Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!