Sunday, April 24, 2016

RC SIMIYU: WATENDAJI MWIBA HOLDINGS LIMITED, MARUFUKU KUWAHOJI WANANCHI KATIKA OFISI ZAO





Mkuu  wa mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony J. Mtaka amepiga marufuku tabia ya askari na watendaji  wengine wa  mwekezaji MWIBA Holdings  Limited wa Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori (WMA) Makao wilayani Meatu, ya kuwakamata wananchi na kuwafanyia mahojiano katika Ofisi zao , na kuwataka kufuata sheria na kukitumia kituo cha polisi cha Makao kufanya mahojiano.

Mwenyekiti wa kijiji cha Makao na Diwani wa kata ya Mwangudo Mhe. .Anthony Philipo (kushoto) akiwasilisha malalamiko yake dhidi ya Mwekezaji MWIBA Holdings kwa Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony J. Mtaka (kulia) katika mkutano wa hadhara ambao ulifanyika katika kijiji cha Makao  hivi karibuni. Picha na Stella Kalinga
Mkuu wa Mkoa aliyasema hayo jana alipozungumza na wananchi wa kijiji cha Makao kata ya Mwangudo wilayani Meatu katika mkutano wa hadhara, mara baada ya kusikiliza malalamiko ya wananchi hao dhidi ya Mwekezaji MWIBA Holdings Limited, ikiwemo unyanyasaji wa wananchi, kukiukwa kwa makubaliano ya mikataba ya utwaaji ardhi na mkataba wa uanzishwaji wa Lanchi.

Akiwasilisha malalamiko yake kwa Mkuu wa Mkoa mmoja wa wananchi wanaodaiwa  kupigwa na kufanyiwa vitendo vya unyanyasaji  katika ofisi za MWIBA Holdings Limited, Bibi. Asteria Godson mkazi wa kijiji cha Makao alisema, alichukuliwa nyumbani kwake na kupelekwa katika moja ya ofisi za mwekezaji huyo ambako alipigwa na kusababishiwa maumivu makali na kuvunjika mkono wa kulia ambao hadi sasa hata baada ya kupata matibabu, bado hauwezi kufanya kazi sawasawa.

“Mimi nilikuwa nimelala ndani kwangu wakaingia watu ambao sikuweza kuwatambua wakitaka niwaeleze mahali alipo mume wangu, nikawaambia mume wangu hayupo wakaanza kunipiga, walinipiga baadae wakanichukua mpaka ofisi za MWIBA huko nako walinipiga na kunifanyia vitendo vingi vya unyanyasaji. Kutokana na kile kipigo sasa hivi mkono wangu mmoja haufanyi kazi”alisema Asteria.

 Akipokea maelekezo ya Mkuu wa Mkoa, Afisa  Uhusiano wa MWIBA Holdings Limited Bwana Msafiri Clarenes alisema wamekubali na watatekeleza kama ilivyoelekezwa, ambapo alimuomba Mkuu wa Mkoa atoe maelekezo kwa wananchi wa Mako kuacha kuchungia mifugo katika eneo la uwekezaji.

Katika kukabiliana na tatizo la eneo la malisho ya mifugo, Mtaka alisema Serikali iliweka mpango wa matumizi bora ya ardhi ambao unaeleza kuwa litatengwa eneo maalum kwa ajili ya machungo ambalo litatumika kipindi ambacho majani yatakuwa yamepungua kuanzia mwezi Julai hadi mvua zitakapoanza kunyesha.

Akitoa ufafanuzi juu ya eneo la kulishia mifugo Afisa Ardhi wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu Bwana Emmanuel Lugamila alisema, eneo hilo lipo ndani ya Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori (WMA) Makao na linatarajiwa kuwekewa alama za kudumu mwezi Juni,2016 ili wananchi waweze kulitambua.

Wakati huo huo Mkuu wa Mkoa amewaasa wananchi kuachana na tabia ya kupangisha mifugo ambayo ni maarufu katika Maeneo hayo kama LUBAGA, kwa kuwa ni chanzo cha migogoro kati ya wafugaji, badala yake viongozi wa vijiji wawatambue watu wenye mifugo katika maeneo yao na kuepuka kwenda katika maeneo ambayo hawaruhusiwi kuchungia.

Wananchi wa kijiji cha Makao wamekuwa na Mgogoro wa kimkataba na Mwekezaji MWIBA Holdings Limited ambao  unaendelea kutafutiwa suluhu kwa mujibu wa sheria.   

Tuesday, April 12, 2016

ASKARI POLISI WANAOKIUKA MAADILI YA JESHI WAWAJIBISHWE




Viongozi wa jeshi la Polisi Mkoa wa Simiyu wameaswa kuwawajibisha askari polisi watakaokiuka maadili ya kazi yao ikiwemo kutoa siri za jeshi la polisi kwa wahalifu.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony John Mtaka alipozungumza na Viongozi na Askari wa Jeshi la Polisi Mkoani Simiyu jana,  katika Ukumbi wa Shule ya Sekondari Bariadi Mjini Bariadi, katika kikao cha kujitambulisha na kutoa maelekezo ya Serikali kwa Jeshi la polisi.

Mtaka amesema viongozi hao wasisite kuwawajibisha askari watakaoonekana kuvujisha siri za jeshi hilo kwa kuwa kufanya hivyo kunalifedhehesha Jeshi la Polisi.

“Hatuwezi kukukubali kudhalilisha taaluma ya jeshi la polisi, hivi askari anayetoa siri za jeshi OCD unamwangalia wa nini, hii ni fedheha. Jeshi la Polisi linaonekana la ovyo kwa sababu ya askari wachache wasiotaka kutii  na kufuata maadili; raia anashindwa kutoa taarifa katika chombo cha dola kwa sababu anaogopa chombo cha dola kitamuuza, aibu hii haivumiliki wachukulieni hatua” alisema Mtaka.

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa  amewataka viongozi wa Jeshi la Polisi kufanya kazi kwa bidii na kusimamia haki ili askari watekeleze majukumu yao  sawa sawa.

Pamoja na kuwaasa Mtaka alitoa pongezi kwa jeshi la polisi kwa kazi nzuri inayoendelea kufanyika katika maeneo tofauti ya mkoa wa Simiyu ikiwa ni pamoja na kufanikiwa kuwakamata majangili waliotungua helikopta wilayani Meatu ,kufanya oparesheni za kuteketeza mashamba ya bangi na kazi nyingine za ulinzi na usalama wa raia na mali zao.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Simiyu, ASP. Onesmo Lyanga, alisema hatasita kuwachukulia hatua viongozi  na askari wa jeshi la polisi wababaishaji, hivyo akawataka wafanye kazi zao kwa bidii.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mh. Anthony J. Mtaka (wa pili Kushoto) akizungumza na viongozi na Askari wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Simiyu (hawapo pichani) jana mjini Bariadi, kulia kwake (wa kwanza) ni Kamanda wa Polisi Mkoa. Onesmo Lyanga.




Thursday, April 7, 2016

BARAZA LA USHAURI LA WATUMIA HUDUMA ZA EWURA LAZINDULIWA RASMI MKOANI SIMIYU


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony J.  Mtaka  jana amezindua  Kamati ya Mkoa ya Baraza la  Ushauri  la Watumiaji wa Huduma zinazodhibitiwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Maji na Nishati (EWURA) ya mkoa huo.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony John Mtaka (wa pili kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Wadau wa Huduma za Nishati , Viongozi wa Serikali na Wajumbe wa Kamati ya Baraza la Ushauri la Watumia huduma za Nishati na Maji la Mkoa wa Simiyu iliyozinduliwa Aprili 06,2016. ( wa kwanza kulia ) ni Katibu Tawala Mkoa, Bibi Mwamvua A. Jilumbi. Picha na Stella Kalinga

Akizungumza na wajumbe wa Kamati ya Baraza hilo na wadau walioshiriki katika hafla ya uzinduzi , iliyofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Mtaka alisema kamati ya baraza hilo inapaswa kuhakikisha inakuwa mstari wa mbele katika kutetea maslahi ya watumiaji wa huduma za nishati na maji, hasa upatikanaji  na uboreshaji  ili huduma hizo ziendane na thamani ya fedha wanazotoa watumiaji.

Mtaka alisema wajumbe wa kamati ya baraza la ushauri la watumia huduma za EWURA, wanao wajibu wa kuelimisha na kusambaza taarifa sahihi kwa watumiaji wa huduma za nishati na maji ili wajue masuala yanayowahusu hususani haki na wajibu wao.
“Mwenyekiti kamati yako itoe taarifa za mara kwa mara kwa watumiaji wa huduma za nishati na maji hasa yanapotokea mabadiliko kama kupanda au kushuka kwa bei ya maji , mafuta na umeme, kukatika kwa maji au umeme na taarifa nyingine muhimu kwa watumiaji wa huduma hizi ili wawe na ufahamu wa kutosha”, alisema Mtaka.

 Aliahidi kuwa Serikali ya Mkoa na vyombo vyake itashirikiana na Kamati ya baraza hili la Mkoa katika kuwajengea mazingira mazuri ya kufanya kazi ikiwa ni pamoja na kutoa ushirikiano na kuhakikisha malengo ya kuanzishwa kwake yanafanikiwa.

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa aliwataka wafanyabiashara wa mafuta kuwashushia bei wananchi pale inapotokea bei za bidhaa hiyo kupungua katika soko badala ya kuendelea kuwaumiza kwa kisingizio cha kutopunguza bei kwa kuwa walichukua mzigo wakati bei ikiwa juu.


Kamati ya Mkoa ya Baraza la Ushauri la Watumia huduma zinazodhibitiwa na EWURA Mkoa wa Simiyu inaundwa na wajumbe watano: Suzan Sabuni (Mwenyekiti), Kubagwa Madabila(Katibu), Kulwa Mtebe (Mtunza Hazina), Magreth Kayanda (Mjumbe) na Martha Zongo (Mjumbe).

SIMIYU KUPATA MASAFA YA UTANGAZAJI


Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Nape Nnauye ameahidi kushughulikia na kuhakikisha Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA)  inatoa masafa kwa ajili ya utangazaji kwa  Mkoa wa Simiyu.
Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Bibi.. Mwamvua Jilumbi (kulia) akisoma taarifa ya Mkoa kwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Nape M. Nnauye (kushoto) wakati wa ziara yake mkoani Simiyu jana, (katikati) Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony J. Mtaka.


Mhe. Nape aliyasema hayo jana wakati alipozungumza na wadau wa Habari, Utamaduni ,Sanaa na Michezo wa Mkoa wa Simiyu katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, wakati wa Ziara yake ya siku moja Mkoani humo.

Nape alisema  mara masafa hayo yatakapotangazwa katika Mkoa wa Simiyu, Wakurugenzi wa Halmashauri za mkoa huo wanzishe redio zao ili kuwawezesha kutoa taarifa mbalimbali za utendaji wa Serikali na kuzifanya kuwa vyanzo vya mapato katika Halmashauri zao.

“Katibu Tawala Mkoa wahamasishe wakurugenzi wa Halmashauri zako kuanzisha vituo vya redio, kila nilipopita nikakuta Halmashauri ina kituo cha redio wako mbali sana”, alisema Nape.

Akisoma taarifa ya Mkoa kwa Mhe. Waziri, Katibu tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bibi. Mwamvua Jilumbi alisema Mkoa wa Simiyu una kituo kimoja cha Redio SIBUKA ambacho hurusha matangazo yake kutoka wilayani Maswa.

Wakati huo huo Waziri Nape Nnauye aliagiza Halmashauri ambazo hazina Maafisa Habari waajiri na wale walio nao wahakikishe Maafisa Habari wanaingia katika vikao vya maamuzi ili wawe na taarifa za kutosha hali itakayowajengea uwezo wa kuzisemea Halmashauri na Mkoa kwa usahihi.

Aidha, amesisitiza uongozi wa Mkoa kupitia kwa Katibu Tawala wa Mkoa ambaye ni mwenyekiti wa Kamati ya Michezo ya Mkoa, kuimaarisha vyama vya  michezo na kuvisaidia kupata viongozi bora watakaosaidia kuendeleza michezo yote ndani ya mkoa.

Sambamba na kuimarisha vyama vya michezo Mhe. Nape alieleza azma ya Serikali katika kurasimisha shughuli za sanaa, ambapo kwa kufanya hivyo kutawasaidia wasanii kupata kipato.


Waziri Nape alifanya ziara ya siku moja mkoani Simiyu akitokea Mkoani Geita, ikiwa ni mwendelezo wa ziara yake ya kutembelea mikoa mipya na mikoa ya pembezoni ili kujionea changamoto mbalimbali za sekta ya Habari Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!