Saturday, May 21, 2016

SAGINI: WAKUU WA IDARA ZINGATIENI USHAURI WA WAKAGUZI WA NDANI HALMASHAURI ZIPATE HATI SAFI




Wakuu wa Idara wametakiwa kuzingatia ushauri wa Wakaguzi wa Ndani wa kujibu hoja inavyotakiwa ili Halmashauri zao zisipate hati zenye masahaka au hati chafu..

Hayo yalisemwa na Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne A.Sagini wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya usimamizi wa fedha, mipango na bajeti, uwekezaji, uimarishaji ukusanyaji wa mapato, taratibu za ukaguzi wa ndani na manunuzi ya umma kwa wahasibu, wakaguzi wa ndani, maafisa ugavi na maafisa mipango wa Halmashauri zote za Mkoa wa Simiyu, yaliyofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya wilaya ya Meatu.

Mbali kuzisaidia Halmashauri  kutopata hati za mashaka au chafu kutoka kwa mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) taarifa za mkaguzi wa ndani zinasaidia menejimenti kutambua kasoro za mfumo wa usimamizi wa fedha ndani ya taasisi na kuziondoa kwa kuzingatia sheria na kanuni za umma.

“Mkaguzi wa Ndani ni Jicho la Afisa Masuuli kumwezesha kujua kama matumizi ya fedha za Umma yanafuata taratibu na miongozo ya usimamizi wa fedha za Umma iliyopo na anawakumbusha wakuu wa Idara na Vitengo kujibu Hoja za Mkaguzi wa Ndani ya siku saba kama sheria inavyotaka, ” , alisema Sagini

Sagini alisema kuwa mafunzo hayo yamelenga katika umuhimu wa usimamizi wa rasilimali fedha ikiwa kama kiungo cha kuwezesha kutoa huduma bora kwa wananchi, ambapo wataongeza utambuzi, namna ya kuanzisha wazo la uwekezaji na namna ya kupata fedha za miradi katika kufanya uwekekezaji katika sekta ya umma.

Kwa upande wake Thomas Magambo ambaye ni mtaalamu mshauri wa mradi wa PFMRP IV Mkoa wa Mara na Simiyu amesema kuwa mafunzo hayo yanalenga kuboresha mfumo wa manunuzi ya umma, ukusanyaji mapato na uwekezaji ndani ya halmashauri ili kuongeza ukusanyaji mapato na kuwezesha kupata hati safi.

Naye  Donatus Wegina, Katibu Tawala Msaidizi wa Mipango na Uratibu katika Sekretarieti ya Mkoa wa Simiyu, alisema kuwa mafunzo hayo yamefanyika ili kuwajengea uwezo wasimamizi wa fedha za ndani, ukaguzi wa ndani, manunuzi, mipango na bajeti ili mipango inayoandaliwa iweze kusaidia Halmashauri kupata hati safi na kuhakikisha kuwa fedha za Umma zinatumika kwa kufuata miongozo na taratibu za kibajeti kwa manufaa ya wananchi na Taifa kwa ujumla.

Katika ukaguzi uliofanywa na Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa hesabu za mwaka 2014/2015 Halmashauri za Itilima, Bariadi Mji na Busega zimepata hati safi wakati huo Halmashauri za Meatu, Maswa na Bariadi vijini  zimepata hati zenye mashaka.


Katibu Tawala Mkoa Simiyu, Jumanne A. Sagini akizungumza na wahasibu, wakaguzi wa ndani, maafisa ugavi na maafisa mipango wa Halmashauri za Mkoa wa Simiyu (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya usimamizi wa fedha, mipango na bajeti, uwekezaji, ukusanyaji mapato na taratibu a ukaguzi wa ndani na manunuzi ya umma. Picha na Stella A. Kalinga
Katibu Tawala Mkoa Simiyu, Jumanne A. Sagini (wa nne kulia) akiwa katika picha ya pamoja na wahasibu, wakaguzi wa ndani, maafisa ugavi na maafisa mipango wa Halmashauri za Mkoa wa Simiyu na wawezeshaji , mara baada ya ufunguzi wa mafunzo ya usimamizi wa fedha, mipango na bajeti, uwekezaji, ukusanyaji mapato na taratibu na ukaguzi wa ndani na manunuzi ya umma,(wa nne kushoto ) Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, Godfrey Machumu Picha. Stella A. Kalinga


Katibu Tawala Mkoa, Jumanne A. Sagini akiangalia vifaa vilivyowekwa na Halmashauri ya Wilaya ya Meatu kwa ajili ya kuwekea taka ikiwa ni njia mojawapo ya kuweka safi mji wa Mwanhuzi na mkakati wa usafi na utunzaji wa mazingira Wilyani humo (wa kwanza kushoto) ni Katibu Tawala Wilaya ya Meatu, Chele Ndaki. Picha Na Stella A. Kalinga

 
Katibu Tawala Mkoa, Jumanne A. Sagini akizungumza na mafundi wanaotengeneza madawati katika moja ya karakana kwa ajili ya shule za msingi na Sekondari wilayani Meatu, ikiwa ni utekelezaji wa agizo la Rais, John Pombe Magufuli la kuhakikisha kuwa hakuna mwanafunzi anayekaa chini ifikapo Juni 30, 2016. Picha Na Stella A. Kalinga









Sunday, May 15, 2016

RC SIMIYU AMPA SIKU TANO MTAALAM MSHAURI MRADI WA BARABARA BARIADI MJINI KUWASILISHA MAPITIO YA GHARAMA ZA MRADI(BOQ)



Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtaka,  ametoa siku tano kwa Mtaalam Mshauri wa Mradi wa Ujenzi wa Barabara za Halmashauri ya Mji wa Bariadi (NOR PLAN) kuwasilisha mapitio ya Mchanganuo wa Gharama (BOQ) ya Ujenzi wa barabara hizo katika Ofisi yake.

Mtaka alitoa agizo hilo jana wakati wa ziara yake ya ukaguzi wa miradi ya ujenzi wa barabara aliyoifanya katika Halmashauri ya Mji Bariadi, akiambatana na Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Bariadi.

 Mtaka alisema ipo haja kwa Uongozi wa Mkoa kuona mapitio hayo ili Ofisi ya Mkoa na watendaji wengine wayapitie na kuona kama kuna vitu ambavyo si vya msingi au vyenye gharama kubwa wamshauri Mtaalam mshauri na Mkandarasi kuviondoa ili kupunguza gharama ya mradi huo uliopangwa kutekelezwa kwa shilingi bilioni 9.1 kwa kilomita 6.

“Katibu Mkuu TAMISEMI alipokuja alikuagiza ufanye review ya BOQ na akataka uanishe kiasi gani cha fedha kitaokolewa . Nakala hiyo tunapaswa tuipate sisi kama viongozi wa mkoa, naagiza uilete hiyo review Ijumaa saa 4:00 asubuhi, halafu  Katibu Tawala Mkoa atakaa na Wataalam wa Sekretarieti  na wadau wengine ambao kwa pamoja watashauri nini kifanyike”alisema Mtaka.

Aidha, baada ya Mhandisi wa Mkandari wa Mradi, Jassie And Company Ltd (JASCO), Ndg. Daniel Nila kueleza kuwa gharama za ujenzi wa barabara hizo zilipangwa kuwa shilingi bilioni 1.3 kwa kilomita moja,  kutokana na barabara hiyo kupangwa kujengwa kwa hadhi ya barabara ya uwanja wa ndege; Mkuu wa mkoa aliwashauri kuangalia mazingira ya Mji wa Bariadi na kujenga barabara inayoendana na mazingira ili kupunguza gharama zisizo za lazima.

Sanjari na hilo Mkuu wa mkoa alitoa wito kwa Wakandarasi wazawa wanaopewa dhamana ya kutekeleza miradi ya Serikali, kuweka uzalendo mbele na kutekeleza miradi kwa kiwango.

Kwa upande wake Mhandisi Victor Malya kutoka Kampuni ya NOR PLAN (Mtaalam Mshauri wa Mradi), alisema tangu Mradi wa ujenzi wa barabara za Mji Bariadi uanze kutekelezwa mwezi Agosti, 2015 hadi sasa umetekelezwa kwa asilimia 50, ulitarajiwa kukamilishwa mwezi Agosti 2016  lakini kutokana na sababu mbalimbali ikiwepo mvua kubwa iliyonyesha mwezi Novemba na Desemba mradi huo hautaweza kukamilika ndani ya muda uliopangwa katika mkataba.

Pamoja na maelezo hayo kutoka kwa Mhandisi Malya, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu alimtaka Mkandarasi wa mradi huo  (JASCO) kuongeza kasi ya utekelezaji  kufikia mwezi Oktoba mradi uwe umetekelezwa kwa asilimia kubwa ili barabara hizo zikatumiwe na viongozi na wananchi wakati wa maadhimisho ya Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2016, kwa sababu kama zitakuwa  zimefungwa kama ilivyo sasa  zitasababisha usumbufu.
Mkuu wa mkoa wa Simiyu Mhe. Anhony J. Mtaka (wa kwanza kulia) akimsikiliza Mhandisi wa Ujenzi wa Sekretarieti ya Mkoa, Deusdedit Mshuga akitoa maelezo na kuonesha mapungufu aliyoyaona katika barabara ya Muungano-Malambo iliyojengwa na Mkandarasi Mzawa GAT Engineering, wakati wa ziara yake ya kukagua miradi ya Barabara mjini Bariadi.




Tuesday, May 10, 2016

RC SIMIYU APIGA MARUFUKU DAGA SHIDA



Mkuu wa Simiyu Mhe. Anthony J. Mtaka amepiga marufuku tabia ya viongozi wa kimila kuwaadhibu wananchi  wanaobanika kuwa kuwa na makosa kupita mabaraza ya kimila maaarufu  kama DAGA SHIDA na badala yake amewataka  watumie vyombo vya Serikali vinavyotambulika kisheria.

Mtaka alitoa agizo hilo alipozungumza na wananchi wa kijiji cha Ikindilo kata ya Ikindilo tarafa ya Bumela wilayani Itilima, ambapo ameitaka Kamati ya Ulinzi na Usalama wilayani Itilima, kulisimamia suala hilo kwa kuwa limekuwa likiwadharirisha wananchi na wale watakaobainika kukaidi agizo hilo, wafikishwe kwenye vyombo vya sheria na kuchukuliwa hatua.

“Mkuu wa Wilaya na wajumbe wako kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya, simamieni suala hili na mhakikishe linakomeshwa kabisa. Naagiza  hili kwa mkoa mzima sitaki kusikia kitu kinachoitwa daga shida. Hatuwezi kuacha wananchi wanateseka, watumishi wetu tunaowaleta kuwatumikia wananchi nao wanateseka na mifumo kandamizi kama hii wakati vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vipo”alisema Mtaka 

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa aliwataka wananchi watakaoitwa kwa ajili ya kwenda kuadhibiwa na viongozi wa mabaraza ya kimila maarufu kama Sumbantale wasikubali na wawatake viongozi hao wa kimila kuwashtaki  katika ofisi za Serikali au katika Vituo vya polisi ikiwa watajiridhisha kuwa wana makosa.
Mfumo wa daga shida umekuwa ukitumwa katika maeneo mengi mkoani Simiyu, ambapo wananchi  hususani watumishi wa umma wamekuwa wakiadhibiwa na viongozi wa kimila kwa kuwataka kulipa faini ya fedha , mazao, wanyama  na kupigwa pale wanapoonekana kwenda kinyume na matakwa yao ya kimila na wakati mwingine wamekuwa wakizushiwa .

Wakati huo huo Mtaka amewataka  wazazi na walezi kuacha mara moja tabia ya  kuwakatisha masomo watoto wao wa kike na kuwaozesha kwa kuwa wakiendelea kufanya hivyo watachukuliwa hatua kali za kisheria.

“Ole wake mzazi au mlezi atakayemtoa mtoto shule  na akaenda kumuozesha,ajue ameamua kuhamishia maisha yake toka nyumbani kwenda jela, hilo halina mjadala. Mtoto wa shule ni wako kwa kuwa umemzaa lakini akiwa shule toka darasa la kwanza  mpaka kidato cha sita ni mali ya serikali” alisema Mtaka.

WAKAZI WA ITILIMA WAISHUKURU LIFE MINISTRY KUWACHIMBIA KISIMA



Wakazi wa kijiji cha Ikindilo wilayani Itilima wamelishukuru Shirika la dini la Life Minisry kwa kuwatoa katika adha ya maji iliyokuwa ikiwakabili kwa kuwachimbia kisima kirefu chenye thamani ya shilingi milioni 50.

Akizungumza mara baada ya uzinduzi wa kisima hicho uliofanywa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony . J. Mtaka , mkazi wa kijiji cha Ikindilo bibi . Monica Malugu alisema kisima hicho kimewasadia kuondokana na ashida ya kufuata maji kwa mwendo mrefu.

“Nawashukuru sana wafadhili kwa kutukumbuka wana Ikindilo kwa kutuchimbia kisima hiki, tulikuwa tunafuata mbali yaani tulikuwa tunatembea zaidi ya masaa matatu. Tulikuwa tunaamka usiku kwenda kufuata maji  na wakati mwingine tukichelewa kurudi tunapigwa na waume zetu” alisema Bibi Monica.

Akitoa shukrani kwa niaba ya Serikali, Mkuu wa mkoa wa Simiyu amesema Serikali inatambua na kuthamini mchango wa mashirika ya dini katika maendeleo ya nchi ya Tanzania na watu wake na akaahidi kuulinda mradi huo na miradi mingine ya Life Ministry inayotekelezwa katika mkoa wa Simiyu.

Aidha, Mtaka alisema wafadhili kama hao wamekuwa wadau wakubwa wa maendeleo tangu uhuru hivyo  aliwahakikishia kuwa watapata ushirikiano wa kotosha kutoka kwa Viongozi wa Serikali ngazi ya kijiji hadi Mkoa pale watakapohitaji  kutekeleza miradi mingine ya maendeleo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Life Ministry Tanzania Bw.Dismas Shekalaghe aliwataka wakazi wa Ikindilo kukilinda na kukitunza kisima hicho na miundombinu yake ili kiwanufaishe kwa kuwapa huduma  ya maji safi iliyo endelevu, ambapo walaihidi kukifanyia ukarabati kila baada ya mwaka mmoja.
Shirika la Life Ministry linafanya kazi katika nchi zaidi ya 198 duniani, Pamoja na kuchimba visima vitatu katika mkoa wa Simiyu wanatarajia  kuwasaidia wananchi  katika maeneo mengine,  hususani kilimo cha mboga mboga ili kuwakwamua katika umasikini.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka  (katikati) akikata utepe wakati wa uzinduzi wa kisima kilichochimbwa na shirika la dini la Life Ministry kwa ajili ya wakazi wa Ikindilo wilayani Itilima, kushoto kwake ni Mkurugenzi wa Shirika la Life Ministry Bw. Dismas Shekalaghe na kulia kwake ni Diwani wa kata ya Ikindilo, Mhe.Joseph Kulwa. Picha na Stella Kalinga


 Mkurugenzi wa Shirika la Life Ministry Bw. Dismas Shekalaghe (kulia) akizungumza na wananchi wa Ikindilo (hawapo pichani) kabla ya uzinduzi wa kisima cha maji, wa pili kulia Mkuu wa mkoa wa Simiyu akifatiwa na Mkuu waWilaya ya Itilima Mhe. Georgiina Bundala.



Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!