Sunday, May 15, 2016

RC SIMIYU AMPA SIKU TANO MTAALAM MSHAURI MRADI WA BARABARA BARIADI MJINI KUWASILISHA MAPITIO YA GHARAMA ZA MRADI(BOQ)



Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtaka,  ametoa siku tano kwa Mtaalam Mshauri wa Mradi wa Ujenzi wa Barabara za Halmashauri ya Mji wa Bariadi (NOR PLAN) kuwasilisha mapitio ya Mchanganuo wa Gharama (BOQ) ya Ujenzi wa barabara hizo katika Ofisi yake.

Mtaka alitoa agizo hilo jana wakati wa ziara yake ya ukaguzi wa miradi ya ujenzi wa barabara aliyoifanya katika Halmashauri ya Mji Bariadi, akiambatana na Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Bariadi.

 Mtaka alisema ipo haja kwa Uongozi wa Mkoa kuona mapitio hayo ili Ofisi ya Mkoa na watendaji wengine wayapitie na kuona kama kuna vitu ambavyo si vya msingi au vyenye gharama kubwa wamshauri Mtaalam mshauri na Mkandarasi kuviondoa ili kupunguza gharama ya mradi huo uliopangwa kutekelezwa kwa shilingi bilioni 9.1 kwa kilomita 6.

“Katibu Mkuu TAMISEMI alipokuja alikuagiza ufanye review ya BOQ na akataka uanishe kiasi gani cha fedha kitaokolewa . Nakala hiyo tunapaswa tuipate sisi kama viongozi wa mkoa, naagiza uilete hiyo review Ijumaa saa 4:00 asubuhi, halafu  Katibu Tawala Mkoa atakaa na Wataalam wa Sekretarieti  na wadau wengine ambao kwa pamoja watashauri nini kifanyike”alisema Mtaka.

Aidha, baada ya Mhandisi wa Mkandari wa Mradi, Jassie And Company Ltd (JASCO), Ndg. Daniel Nila kueleza kuwa gharama za ujenzi wa barabara hizo zilipangwa kuwa shilingi bilioni 1.3 kwa kilomita moja,  kutokana na barabara hiyo kupangwa kujengwa kwa hadhi ya barabara ya uwanja wa ndege; Mkuu wa mkoa aliwashauri kuangalia mazingira ya Mji wa Bariadi na kujenga barabara inayoendana na mazingira ili kupunguza gharama zisizo za lazima.

Sanjari na hilo Mkuu wa mkoa alitoa wito kwa Wakandarasi wazawa wanaopewa dhamana ya kutekeleza miradi ya Serikali, kuweka uzalendo mbele na kutekeleza miradi kwa kiwango.

Kwa upande wake Mhandisi Victor Malya kutoka Kampuni ya NOR PLAN (Mtaalam Mshauri wa Mradi), alisema tangu Mradi wa ujenzi wa barabara za Mji Bariadi uanze kutekelezwa mwezi Agosti, 2015 hadi sasa umetekelezwa kwa asilimia 50, ulitarajiwa kukamilishwa mwezi Agosti 2016  lakini kutokana na sababu mbalimbali ikiwepo mvua kubwa iliyonyesha mwezi Novemba na Desemba mradi huo hautaweza kukamilika ndani ya muda uliopangwa katika mkataba.

Pamoja na maelezo hayo kutoka kwa Mhandisi Malya, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu alimtaka Mkandarasi wa mradi huo  (JASCO) kuongeza kasi ya utekelezaji  kufikia mwezi Oktoba mradi uwe umetekelezwa kwa asilimia kubwa ili barabara hizo zikatumiwe na viongozi na wananchi wakati wa maadhimisho ya Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2016, kwa sababu kama zitakuwa  zimefungwa kama ilivyo sasa  zitasababisha usumbufu.
Mkuu wa mkoa wa Simiyu Mhe. Anhony J. Mtaka (wa kwanza kulia) akimsikiliza Mhandisi wa Ujenzi wa Sekretarieti ya Mkoa, Deusdedit Mshuga akitoa maelezo na kuonesha mapungufu aliyoyaona katika barabara ya Muungano-Malambo iliyojengwa na Mkandarasi Mzawa GAT Engineering, wakati wa ziara yake ya kukagua miradi ya Barabara mjini Bariadi.




0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!