Thursday, May 5, 2016

RC SIMIYU AAGIZA KAMATI YA ULINZI NA USALAMA YA WILAYA BARIADI KUMPA TAARIFA YA MIRADI YA MAJI




Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka ameiagiza  Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Bariadi kumpelekea taarifa ya miradi ya maji inayotiliwa shaka ya kujengwa chini ya kiwango, ndani ya siku tano kuanzia tarehe 04.05.2016.

Mtaka alitoa agizo hilo jana alipokuwa akizungumza na viongozi na watendaji  katika kikao cha Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi, katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki Bariadi.

 “Siwezi kuvumilia na kuendelea kuona fedha za Serikali zinazotolewa kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji na miradi mingine kwa ajili ya maendeleo ya wananchi zinatumika vibaya au miradi ya maendeleo kutekelezwa chini ya kiwango. DC na Kamati yako ya Ulinzi na Usalama nataka uniletee taarifa ya miradi yote ya maji katika wilaya ya Bariadi inayotiliwa shaka ya kutekelezwa chini ya kiwango,Jumatatu asubuhi, ili tuchukue hatua” alisema Mtaka.

Mtaka aliwataka  viongozi na watendaji kila mmoja kutimiza wajibu wake katika kusimamia na kuhakikisha miradi yote ya Serikali inatekelezwa kwa kiwango,  kulingana na thamani ya fedha ili iweze kuleta manufaa kwa wananchi.

Aidha, Mkuu wa Mkoa alisema hatasita kumchukulia hatua mtu yeyote atakayebainika kuhusika kwa namna moja ama nyingine katika utekelezaji wa miradi hiyo chini ya kiwango hata kama ni kada wa Chama Tawala, kwa sababu amedhamiria kutekeleza ilani ya Chama cha Mapinduzi ambacho kimeaminiwa na kupewa ridhaa ya kuongoza nchi na wananchi wenyewe, ambapo aliahidi atasimamia ipasavyo ili wananchi waendelee kukiamini Chama cha Mapinduzi na Serikali yake.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony J.Mtaka (wa pili kulia) akizungumza na madiwani na watendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi (hawapo pichani) katika kikao cha Baraza la Madiwani kilichofanyika katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki Bariadi

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!