Wednesday, March 3, 2021

KILO 145,000 ZA CHOROKO ZAUZWA MNADA WA KWANZA SIMIYU

 Takribani kilo 145,000 za zao la choroko mkoani Simiyu zimeuzwa kupitia mnada uliofanyika kwa mara ya kwanza katika ghala lililopo kiwanda cha zamani cha kuchambua pamba cha Sola wilayani Maswa, ambapo kilo moja ya choroko imeuzwa kwa shilingi 1578 kwa kilo( kwa bei ya mnada) na mkulima kulipwa shilingi 1610 kwa kilo baada ya kupunguzwa kwa baadhi ya tozo.

 

Akizungumzia mnada huo Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bi. Miriam Mmbaga amesema bei hiyo ya choroko kwa njia ya mnada inamkomboa mkulima na itamsaidia kuona faida na tija zaidi ya kilimo ikilinganishwa na bei ya awali ambayo mkulima alikuwa akilipwa shilingi 800 mpaka shilingi 1200 kwa kilo.

 

“Bei ya leo ya mnada ilikuwa shilingi 1578 kwa kilo ambayo kwa maoni ya wakulima ina faida, lakini Halmashauri kwa kushirikiana na ushirika wameongeza shilingi 32 kwa kilo ili kumsaidia mkulima kufanya maandalizi ya msimu unaofuata wa mazao mengine na shughuli nyingine, kwa hiyo leo mkulima amepata shilingi 1610 kwa kilo,” alisema Mmbaga.

 

Aidha, Mmbaga amewahakikishia wakulima usalama wa mazao yao yatakapopokelewa katika maghala makuu kwa kuwa watunza maghala wamekata bima zote ikiwepo bima ya moto na wizi kwa ajili ya kubeba dhamana ikiwa kutatokea majanga au wizi.

 

Wakati huo huo Mmbaga ametoa wito kwa wakulima kulima kilimo biashara ili waweze kupata faida na kuona tija katika kilimo chao huku akiwasisitiza kutumia fedha zao vizuri kwa kuwekeza kwenye shughuli za maendeleo ili waweze kutatua mahitaji mbalimbali ya kijamii.

 

Katika hatua nyingine Mmbaga ametoa wito kwa Wafanyabiashara kutoka mikoa yote nchini kushiriki katika minada ya ununuzi wa choroko katika maghala yaliyopo mkoani hapa na kuwahakikishia ushirikiano wakati wowote watakapohitajika.

 

Bw. Daniel Mipawa ambaye ni mkulima kutoka Chama cha ushirika cha Msingi cha Nhaya amesema uuzaji wa choroko kupitia mnada ameupokea vizuri kwa kuwa umekuwa msaada kwenye suala la bei maana wakulima wamekuwa wakiwauzia choroko baadhi ya wafanyabiashara shilingi 800 mpaka shilingi 1200.

 

Naye mfanyabiashara Ibrahim Musa akizungumzia hali ya mnada na bei ya choroko amesema “Bei ya mnada wa leo wa choroko ya shilingi 1578 kwa kilo ilikuwa haitulipi lakini tumekaa na viongozi wa serikali wameamua kutupunguzia baadhi ya tozo, kwa kuwa wametupunguzia baadhi ya tozo na kuturudishia gharama za usafiri sasa hivi tutaenda vizuri.”

 

Kwa upande wake Msimamizi wa ghala kuu Maswa, Bw. Abdallah Ngozi amesema mnada wa choroko umeenda vizuri na kushauri wakulima pamoj na kuwa na nafasi ya kuamua kuuza au kutokuuza kulingana na bei ya mnada wa siku husika wawe makini kwa kuwa wanaweza kukataa kuuza na bei ikashuka zaidi ya ile ya awali

MWISHO

Baadhi ya vijana wakishusha choroko zilizokusanywa kutoka kwa wakulima kupitia Vyama vya Ushirika vya Msingi (AMCOS) na kuzipeleka ghala kuu ili zihifadhiwe kwa ajili ya kuuzwa kupitia mnada katika mfumo wa stakabadhi ghalani


Namna mnada wa choroko unavyoonesha na kuendeshwa kupitia mtandao

Baadhi ya Vijana wakipakia choroko katika mifuko maalum yenye nembo ya alama ya Chama Kikuu cha Ushirika cha Mkoa wa Simiyu (SIMCU) tayari kwa ajili ya kuzihifadhi kwa ajili ya kusubiri mnada.

Baadhi ya vijana wakishusha choroko zilizokusanywa kutoka kwa wakulima kupitia Vyama vya Ushirika vya Msingi (AMCOS) na kuzipeleka ghala kuu ili zihifadhiwe kwa ajili ya kuuzwa kupitia mnada katika mfumo wa stakabadhi ghalani.


Mkuu wa Wilaya ya Maswa, Mhe. Aswege Kaminyoge(kulia) akiteta jambo na Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bi. Miriam Mmbaga mara baada ya mara baada ya muda wa choroko za Simiyu kumalizika Machi 02, 2021.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bi. Miriam Mmbaga akiangalia namna mnada wa choroko unavyofanyika kupitia mtandao kwa kutumia kompyuta iliyokuwa mbele yake (haipo pichani) katika eneo la Sola Wilayani Maswa Machi 02, 2021 wengine ni wafanyabiashara wa choroko wakifuatilia mnada huo pia.

Afisa Kilimo wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Iman Matimbwa (kulia) akimuonesha jambo Mkuu wa Wilaya ya Maswa, Mhe. Aswege Kaminyoge (kushoto) kuhusu mnada wa choroko kupitia mtandao, mara baada ya muda wa choroko za Simiyu kumalizika Machi 02, 2021.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bi. Miriam Mmbaga akiangalia namna mnada wa choroko unavyofanyika kupitia mtandao kwa kutumia kompyuta iliyokuwa mbele yake (haipo pichani) katika eneo la Sola Wilayani Maswa Machi 02, 2021.



0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!