Sunday, March 27, 2016

RC SIMIYU AAGIZA MENEJA MAMLAKA YA MAJI ACHUNGUZWE

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony J. Mtaka ameviagiza Vyombo vya Ulinzi na Usalama, kumkamata na kumchunguza Meneja wa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Wilayani Maswa (MAUWASA) Mhandisi. Lema Jeremia.
Mtaka ametoa agizo hilo kufuatia taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Wilaya ya Maswa Mhe. Rosemary Kirigini kuwa Meneja huyo anatuhumiwa kushindwa kusimamia Mamlaka hiyo na kutoa taarifa za uongo kuhusu mwenendo mzima wa utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa chujio la maji, katika Bwawa la New Sola lililopo katika Kijiji cha Zanzui kwa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya.
Aidha, Bi.Rosemary Kirigini amesema Meneja huyo anapaswa kuchukuliwa hatua kwa kuwa  utekelezaji wa mradi huo ulikuwa ukifanyika bila uwepo wa Bodi ya Mamlaka ya Maji. “Mhe. Mkuu wa Mkoa kwa maneno ya Mwenyekiti wa Bodi, anasema bodi hii imeanza kazi hivi karibuni kwa maana hiyo haikuwepo, mimi nasema  akamatwe na afikishwe mahakamani” alisema Kirigini.
Mtaka amesema pamoja na mradi wa ujenzi wa chujio, Mamlaka hiyo imekuwa ikisambaza maji kwa wananchi bila kuweka dawa, hali ambayo inaweza kusababisha magonjwa ya mlipuko kama kuhara na kipindupindu.
“Unakusanya fedha kutoka kwa wananchi kila mwezi, lakini unawapatia maji yasiyo na dawa  na unaona hilo ni jambo la kawaida tu. Unakusanya shilingi milioni 20 kwa mwezi kutokana na kuwauzia maji wananchi ambao ni wateja wa mamlaka yako , lakini unashindwa kutoa shilingi milioni 1.7  kununua dawa kwa ajili ya kutibu maji, kwa nini usishukuliwe hatua?”, alihoji Mtaka.
Wakati huo huo Mhe. Mtaka amefuta maadhimisho ya kilele cha wiki ya maji kilichopangwa kufanyika  kimkoa wilayani Meatu na ameelekeza fedha zilizokuwa zimepangwa kufanikisha maadhimisho hayo zitumike kununua madawati.
“Nimefuta maadhimisho ya kilele cha wiki ya maji kwa sababu hatuwezi tukawa tunafanya sherehe  kuadhimisha wiki ya maji wakati watu wanakunywa maji ya tope” alisema Mtaka.


0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!