Saturday, July 14, 2018

WIZARA YA MADINI YAKABIDHI ENEO LA UJENZI WA KITUO CHA UMAHIRI SIMIYU


Wizara ya Madini kupitia Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini (SMMRP) imekabidhi eneo la ujenzi wa Kituo cha Umahiri Bariadi Mkoani Simiyu kwa Mkandarasi wa ujenzi huo SUMA JKT ambao unaotarajiwa kuanza mwezi huu wa Julai 2018.

Makabidhiano hayo yamefanyika jana Mjini Bariadi Mkoani Simiyu na kushuhudiwa na Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Anthony Mtaka, mara baada ya timu ya wataalam wa Wizara ya Madini na SUMA JKT kutembelea eneo la ujenzi lililopo Nyaumata Mjini Bariadi.

Akizungumzia kituo hicho Afisa Madini Mkoa wa Simiyu, Bw. Fabian Mshai amesema  “Kituo hiki ni Jengo la Ofisi ambalo litakuwa na kumbi  za kutolea mafunzo mbalimbali yahusianayo na uchimbaji wa madini unaozingatia kanuni za afya, usalama, uchambuzi wa madini na uhifadhi wa mazingira kwa wachimbaji wadogo ili uchimbaji uwe wenye tija”

Mshai ameongeza Kituo hiki cha Umahiri Bariadi kitajengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 1.3 na Kampuni ya Ujenzi ya SUMA JKT  na kusimamiwa na Kampuni ya Sky Actate Consultants.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Madini kwa kuamua kujenga Kituo hicho kwa kuwa mkoa huo ni mpya na unahitaji majengo mengi, hivyo amaesema ujenzi huo utajibu mahitaji ya mkoa katika kuwasaidia wachimbaji wadogo kuondokana na uchimbaji wa kienyeji na kwenda kwenye uchimbaji wa kisasa

"Wachimbaji wetu wadogo wamekuwa wakifanya shughuli zao kienyeji lakini uwepo wa kituo hiki utajibu mahitaji yao kwa sababu kitakuwa ni sehemu sahihi ya wao kupata elimu juu ya uchimbaji bora, wataalam wa madini watakuwa karibu kwa kuwa ukamilishaji wa kituo hiki utaenda sambamba na uwepo wa rasilimaliwatu" alisema Mtaka.

“ Sisi kama mkoa tuna faida ya uwepo wa rasilimali madini tuna nikeli, shaba, dhahabu, cobalt, tuna chumvi katika wilaya ya Meatu lakini pia tuna madini ya ujenzi kama kokoto, mchanga na mengine, hivyo uwepo wa kituo cha umahiri kutasaidia wachimbaji kufanya kazi zao katika utaalam ili uchimbaji ufanyike kwa ufanisi na uwe na tija” alisema.

Ameongeza kuwa uwepo wa kituo hicho pia utachangia kuboresha mazingira ya utendaji kazi ndani ya mkoa tofauti na ilivyo sasa, ambapo watumishi hao wanatumia majengo ya kukodi ambayo wakati mwingine hayakidhi mahitaji yao.

Amesema kuwepo kwa kituo hicho pia kutasaidia kufikia lengo la Serikali la kuhakikisha Sekta ya Madini inakuwa moja ya vyanzo vikubwa vya mapato kwa kuwekeza utaalam wa rasilimali watu, majengo, upimaji na utaalam mbalimbali wa kusaidia wachimbaji wadogo; hivyo akasisitiza SUMA JKT kukamilisha ujenzi wa kituo hicho kwa wakati.

Naye Luteni Kanali Petro Ngata Meneja wa SUMA JKT Kanda ya Ziwa amemhakikishia Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka kuwa kazi ya ujenzi wa Kituo cha Umahiri Bariadi itafanyika kwa wakati.



Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtaka (katikati) akishuhudia makabidhiano ya nyaraka za Ujenzi wa Kituo Mahiri cha Mkoa wa Simiyu kati ya Meneja wa SUMA JKT Kanda ya Ziwa Luteni Kanali Petro Ngata na Meneja na Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini (SMMRP), Bw. Andrew Erio  kutoka Wizara ya Madini, yaliyofanyika jana katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, mara baada ya makabidhiano ya eneo la ujenzi wa kituo hicho Mjini Bariadi.
Baadhi ya Viongozi wa SUMA JKT na Wizara ya Madini wakikagua eneo la Ujenzi wa Kituo Mahiri Bariadi Mkoani Simiyu, kabla ya kufanya makabidhiano ya eneo hilo jana Mjini Bariadi.

Baadhi ya Viongozi wa SUMA JKT na Wizara ya Madini wakiangalia mchoro wa Jengo la Kituo cha Umahiri Bariadi Simiyu, katika  eneo la Ujenzi wa Kituo hicho kabla ya kufanya  makabidhiano ya eneo hilo jana Mjini Bariadi, kwa ajili ya kuanza taratibu za ujenzi.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka(wa sita kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa SUMA JKT baada ya kushuhudia makabidhiano ya nyaraka  za ujenzi wa Kituo cha Umahiri Bariadi kati ya Mkandarasi ambaye ni SUMA JKT na Wizara ya Madini yaliyofanyika jana katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu mara baada ya makabidhiano ya eneo la ujenzi wa kituo hicho Mjini Bariadi.



Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa SUMA JKT baada ya kushuhudia makabidhiano ya nyaraka  za ujenzi wa Kituo cha Umahiri Bariadi kati ya Mkandarasi ambaye ni SUMA JKT na Wizara ya Madini yaliyofanyika jana katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu mara baada ya makabidhiano ya eneo la ujenzi wa kituo hicho Mjini Bariadi.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!