Sekretarieti ya Mkoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa
Mkoani Simiyu zimekisia kutumia jumla ya shilingi 175,260,331/= kwa ajili
ya miradi ya maendeleo, mishahara na matumizi mengineyo.
Hayo yamesemwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini Machi 15, 2019 wakati akiwasilisha rasimu ya Mapendekezo ya
Mpango wa Bajeti ya mwaka 2019/2020 katika kikao maalum cha Kamati ya Ushauri
ya Mkoa(RCC) kilichofanyika Mjini Bariadi.
Amesema katika kiasi tajwa, shilingi
41,960,264,000/= zitatumika katika miradi ya maendeleo, shilingi
18,522,914,000/= kwa ajili ya matumizi mengineyo na shilingi 114,777,153,000/=
kwa ajili ya mishahara.
Aidha, Sagini amesema Mamlaka za
Serikali za Mitaa zimekadiria kukusanya jumla ya shilingi 13, 004,878,000/=
kutokana na vyanzo vyake vya ndani, ambapo kati ya hizo shilingi
4,745,216,000/= sawa na asilimia 36.5 zitatumika katika utekelezaji wa miradi
ya maendeleo na shilingi 8,259,662,000/= zitatumika kwa ajili ya
uendeshaji wa Mamlaka za Serikali za Mitaa.
Ameongeza kuwa mpango wa bajeti
umezingatia masuala muhimu kwa mkoa ambayo ni kusimamia na kudumisha
masuala ya amani na utulivu, kuimarisha utawala bora na uwajibikaji kwa
kuhakikisha uchaguzi wa Serikali za Mitaa unafanyika kwa amani na utulivu,
kujenga mazingira wezeshi kwa wawekezaji wa ndani na nje, kuimarisha
upatikanaji wa huduma bora za afya, elimu na maji hususani kwa wananchi waishio
vijijini.
Masuala mengine ni Kuzisimamia
Halmashauri ili kubuni, kuandaa maandiko na kufuatilia utekelezajiwa
miradi ya maendeleo ya kuongeza kipato cha halmashauri, kuimarisha mipango ya
matumizi bora ya ardhi,kuendeleza ujenzi wa ofisi, nyumba za viongozi na hospitali
za wilaya Itilima, Bariadi na Busega.
Pamoja na hayo mpango huu umezingatia kuimarisha
upatikanaji wa huduma za kijamii na kiuchumi, kuimarisha usimamizi wa
mapato ya ndani na kuibua vyanzo vipya, kuhuisha mipango mkakati ya mkoa na
halmashauri na kuanza kutekeleza dhana ya kuimarisha utendaji wa kuongeza tija
katika utekelezaji wa kazi na miradi ya kiuchumi.
Awali akifungua kikao cha Kamati ya
Ushauri ya Mkoa, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amemshukuru
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.John Magufuli kwa kutoa fedha
kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa na Hospitali tatu
za Wilaya mkoani hapa.
“Tunamshukuru Mhe.
Rais kwa kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya Hospitali ya Rufaa
ya Mkoa na pia tumepata shilingi bilioni
4.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali za Wilaya ya Bariadi, Busega na Itilima”
alisema Mtaka .
Katika hatua nyingine Mtaka amewapongeza Wabunge wa Mkoa huu kwa namna
wanavyoshiriki katika kuhimiza shughuli za maendeleo huku akiwataka viongozi
wote kuwaunga mkono ikiwa ni pamoja na Wakurugenzi wa Halmashauri zote mkoani
humo kujipambanua katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo itawasaidia
kuongeza kipato, huku ikiipongeza wilaya ya Maswa kwa kuanza utekelezaji wa
ujenzi wa kiwanda cha vifungashio na upanuzi wa kiwanda cha chaki miradi ambayo
itakuwa chanzo cha uhakika cha mapato kwa Halmashauri.
Wajumbe mbalimbali waliohudhuria katika
kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa waliunga mkono mapendekezo ya bajeti
ya mwaka 2019/2020 huku wakisisitiza Halmashauri kuwa na miradi ya kimkakati
ili ziweze kupata vyanzo vipya vya mapato na wananchi kujiunga na bima ya afya
ili kujihakikishia huduma za matibabu.
“Ninashauri Halmashauri ziwe na mradi ya
kimkakati itakayoziongezea mapato yao ya ndani kama ilivyofanya Maswa ambayo
inaenda kuwa na viwanda vikubwa viwili cha chaki na kiwanda cha
vifungashio, tena hasa nashauri kasi
iongezeke hapa Bariadi ambapo ndiyo sura ya Mkoa”alisema Gungu Silanga Mjumbe
wa Halmashauri kuu ya CCM Taifa,kupitia Simiyu.
“Mhe. Mkuu wa Mkoa naunga mkono suala la
kuhamasisha wananchi wetu kujiunga na Bima ya Afya tena natoa wito kwa viongozi
wenzangu tuwe mabalozi kwa wananchi wetu tuwaelimishe na kuwahamasisha kujiunga
na Bima ya Afya ili wawe na uhakika wa kupata matibabu”alisema Mwenyekiti wa
Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, Mhe. Pius Machungwa.
MWISHO
Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Bw.
Jumanne Sagini(kushoto)akiteta jambo na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony
Mtaka katika kikao maalum cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa(RCC) kilichofanyika Machi
15, 2019 Mjini Bariadi.
Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Bw.
Jumanne Sagini akiwasilisha rasimu ya
Mapendekezo ya Mpango wa Bajeti ya mwaka 2019/2020 katika kikao maalum cha
Kamati ya Ushauri ya Mkoa(RCC) kilichofanyika Machi 15, 2019 Mjini Bariadi.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony
Mtaka akifungua kikao maalum cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa(RCC) kilichofanyika Machi
15, 2019 Mjini Bariadi.
Mkuu wa Wilaya ya Maswa, Dkt. Seif
Shekalaghe akichangia jambo katika kikao maalum cha Kamati ya Ushauri ya
Mkoa(RCC) wa Simiyu kilichofanyika Machi 15, 2019 Mjini Bariadi.
Baadhi ya viongozi wa Simiyu
wakifuatilia kwa makini kikao maalum cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa(RCC)
kilichofanyika Machi 15, 2019 Mjini Bariadi.
Mkurugenzi wa Halmashari ya Mji wa
Bariadi, Bw. Melkizedeck Humbe akichangia jambo katika kikao maalum cha Kamati
ya Ushauri ya Mkoa(RCC) wa Simiyu kilichofanyika Machi 15, 2019 Mjini Bariadi.
Meneja wa Mamlaka ya Maji na Usafi wa
Mazingira Bariadi(BARUWASA) akichangia jambo katika kikao maalum cha Kamati ya
Ushauri ya Mkoa(RCC) wa Simiyu kilichofanyika Machi 15, 2019 Mjini Bariadi.
Mjumbe wa Halmashauri kuu ya CCM Taifa
kupitia Simiyu, Mhe. Gungu Silanga akichangia jambo katika kikao maalum cha
Kamati ya Ushauri ya Mkoa(RCC) wa Simiyu kilichofanyika Machi 15, 2019 Mjini
Bariadi.
Baadhi ya viongozi wa Simiyu
wakifuatilia kwa makini kikao maalum cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa(RCC)
kilichofanyika Machi 15, 2019 Mjini Bariadi.
Baadhi ya viongozi wa Simiyu
wakifuatilia kwa makini kikao maalum cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa(RCC)
kilichofanyika Machi 15, 2019 Mjini Bariadi.
0 comments:
Post a Comment