Monday, July 11, 2016

WAKULIMA WA PAMBA WAASWA KUTOWEKA MAJI, MCHANGA, MAFUTA KULINDA UBORA WA PAMBA



Wakulima wa pamba mkoani Simiyu wameaswa kuacha tabia ya kuweka maji ,mchanga, na mafuta katika pamba kwa kisingizio cha kuongeza uzito na wale watakaokaidi watachukuliwa hatua kali 

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony J. Mtaka wakati alipozungumza na Wafanyabiashara wa Pamba pamoja na Wenyeviti  na Wakurugenzi wa Halmashauri zote za Mkoa wa Simiyu wakati wa mjadala wa suala la ununuzi wa pamba katika msimu wa mwaka 2016.

Mtaka amesema wakulima wanaoweka maji , mchanga na mafuta katika pamba wanachangia katika kushusha thamani  pamba ya Tanzania na hivyo kufanya  thamani yake kuwa chini katika soko la dunia.
“Mkoa wa Simiyu unazalisha zaidi ya asilimia 60 ya pamba ya Tanzania kwa hiyo kama pamba hii ikiharibiwa ni wazi kwamba ni pamba ya Tanzania inaharibiwa,mwaka jana tumeuza zaidi ya kilo milioni 70; kama mkoa unaozalisha pamba kwa wingi   tumejipanga kurejesha heshima ya zao la pamba” alisema Mtaka.

Aidha, Mtaka amekemea tabia ya wafanyabiashara kuwaibia wakulima kwa kuchezea mizani na akaagiza atakayebainika achukuliwe hatua kali.

“Hatutavumlia kuona wafanyabiashara wanaowaibia wakulima kwa kufanya ujanja ujanja katika mizani tukiwabaini tutawachukulia hatua kali, na hili limeshaanza kufanyiwa kazi, katika wilaya ya Meatu baadhi ya wafanyabiashara wameshtakiwa , naupongeza sana uongozi wa wilaya ya Meatu” , alisema Mtaka.

Kwa upande wao Wakurugenzi na Wenyeviti wa Halmashauri wameahidi kutoa ushirikiano kwa wanunuzi na kuwaomba watoe malipo ya awali (advanced payment) ili kupunguza madeni yasiyoya lazima na kuzifanya Halmashauri kuendesha baadhi ya shughuli muhimu kupitia ushuru wa pamba.

 Wakati huo huo Mtaka amewataka mawakala wa makampuni yanayojihusisha na ununuzi wa pamba kuwa waaminifu kwa kuacha tabia ya kukimbia na fedha wanazopewa kwa ajili ya kununua pamba na kuwadanganya wakulima kwa kuchezea mizani (kuchakachua) pale wanapopima pamba.

“ Mawakala wa makampuni wafanye kazi yao kwa uaminifu kwa kuwa hiyo ni sehemu ya ajiria kwao, wasilazimishe wafanyabiashara kwenda kutafuta mawakala Kenya, Uganda au nchi nyingine kwa sababu ya kukosa sifa ya uaminifu.Wawe waaminifu kwa fedha wanazopewa na kupima kwa mizani ambazo hazijachakachuliwa” alisema Mtaka. 

Msimu wa ununuzi wa pamba mkoani Simiyu umeanza na Serikali imeagiza wafanyabiashara  kununua kilo moja kwa shilingi 1000 na kuendelea.














0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!