Saturday, July 16, 2016

WAZIRI TIZEBA:WANUNUZI WA PAMBA WATAKAOCHEZEA MIZANI WAKAMATWE


Serikali imesema itawachukulia hatua kali Wafanyabiashara wa pamba watakaochezea mizani kwa lengo la kuwaibia wananchi pale wanaponunua pamba.

 Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mhe. Charles Tizeba wakati wa ziara yake ya siku moja Mkoani Simiyu ,alipotembelea kituo cha kununulia pamba cha N.G.S ,katika kijiji cha Luguru wilayani Itilima.

Waziri Tizeba alisema Serikali haitavumilia vitendo vya unyonyaji dhidi ya mkulima kwa kuwa inafanya kila jitihada   kuwasaidia wakulima wa pamba ili waone umuhimu wa zao hilo na kuhakikisha wanazalisha pamba bora.

Aidha, Waziri Tizeba ameitaka Bodi ya Pamba kuwachukulia wakulima wote watakaobainika kuuza pamba iliyochafuliwa kwa kuwekwa maji, mchanga na mafuta kwa kuwa wanaharibu ubora wa pamba na hivyo kuchangia kushusha thamani ya pamba ya Tanzania katika soko la dunia.

“Sheria ni msumeno unakata kote, Serikali itawachukulia hatua wafanyabiashara wa pamba wanaochezea mizani na ninyi wananchi mnaoweka maji,mafuta na mchanga kwenye pamba muache, mkiendelea mtachukuliwa hatua kwa sababu mnasababisha pamba yetu inashuka thamani katika soko la Dunia”, alisema Tizeba

Kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Simyu, Anthony J. Mtaka amesema Serikali imekusudia kutatua kero za wakulima wa pamba  na kuwakikishia mazingira mazuri ya uzalishaji ikiwa ni pamoja na wakulima kupata mbegu bora, dawa na kuhakikisha wanauza pamba kwa bei nzuri.

“Kwa muda mrefu mmekuwa mkilima pamba na kupata mavuno yasiyoridhisha mpaka mkakata tamaa na kuanza kulima mazao mengine, tunataka pamba kama zao kuu la biashara mkoani Simiyu lizalishwe kwa wingi na katika ubora”, alisema Mtaka wakati alipozungumza na wananchi wa Luguru.

Sanjari na hilo Waziri, Tizeba ametoa wito wa wakulima kuwatumia Maafisa ugani waliopo katika maeneo yao ili wapate ushauri wa kitaalam juu ya kanuni bora za kilimo katika zao la pamba na mazao mengine wanayolima.

Akiwasilisha taarifa ya Mkoa kwa Waziri wa Kilimo,Mifugo na Uvuvi, Katibu Tawala Mkoa, Bw. Jumanne A. Sagini alisema Mkoa wa Simiyu una jumla ya Maafisa Ugani 261 waliopangwa kwenye kata na vijiji na wasimamiwa kikamilifu katika kutimiza majukumu yao ikiwa ni pamoja na kutoa ushauri  wa kitaalam kwa wakulima.

 Waziri Tizeba pia aliwahamasisha wananchi wa Mkoa wa Simiyu kulima kwa wingi dengu, choroko na mbaazi kwa sababu Serikali ya India kupitia kwa Waziri Mkuu wake imesema inahitaji kati ya tani milioni sita hadi nane za choroko, dengu na mbaazi.

Mkoa wa Simiyu unategemea Kilimo kwa asilimia kubwa ambapo sekta ya kilimo inachangia takribani asilimia 75 ya pato la Mkoa na zao kuu la biashara  ni pamba.

Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mhe. Charles Tizeba (kulia) akikagua mzani wa kupimia pamba katika kituo cha kununulia pamba cha N.G.S kilichopo Luguru, wilayani Itilima wakati wa ziara yake Mkoani Simiyu. (Picha Stella A. Kalinga)

Baadhi ya viongozi na wadau wa pamba wa Mkoa wa Simiyu wakimsikiliza Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mhe Charles Tizeba (hayupo pichani) wakati akizungumza na wakazi wa Luguru, wilayani Itilima, (wa kwanza kulia) Katibu Tawala Mkoa, Bw.Jumanne A. Sagini (wa pili) Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony J. Mtaka. (Picha Stella A. Kalinga)

Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Mhe. Charles Tizeba (kulia) akizungumza na wakazi wa Luguru Wilayani Itilima mara baada ya kukagua mzani wa kupimia pamba katika kituo cha kununulia pamba cha N.G.S kilichopo Luguru, wilayani Itilima wakati wa ziara yake ya siku moja Mkoani Simiyu. (Picha Stella A. Kalinga)


0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!