Thursday, June 8, 2017

LIFE MINISTRY YATOA MSAADA WA VIFAA TIBA HOSPITALI TEULE YA MKOA SIMIYU

Shirika la Kidini la Madhebu ya Kikristo la Life Ministry limetoa vifaa tiba vyenye thamani ya zaidi ya shilingi Milioni 40 kwa Hospitali Teule ya Mkoa wa Simiyu, Mjini Bariadi.

Akipokea vifaa tiba  hivyo Mkuu wa Mkoa huo, Mhe.  Anthony  Mtaka ameishukuru Life Ministry kwa msaada huo na kuwahakikishia kuwa vifaa hivyo vitasaidia kuboresha utoaji wa huduma za afya kwa wananchi katika hospitali hiyo.

Aidha, amesema Serikali iko tayari kushirikiana na madhehebu ya dini katika  kuhakikisha kuwa afya za wananchi zinakuwa salama, hivyo akawahakikishia kuwa  milango iko wazi kwa taasisi nyingine za dini zinazotaka kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuboresha huduma za afya.

Mtaka ameongeza kuwa ili Madaktari na wauguzi waweze kutekeleza majukumu yao vizuri ni lazima wawezeshwe vifaa, hivyo msaada huo utawatia moyo na kuongeza ari ya kufanya kazi.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Life Ministry hapa nchini, Dismas Shekalaghe amesema vifaa hivyo vimetolewa kama sehemu ya kuisaidia jamii ambavyo vitawawezesha madaktari na wauguzi kuwahudumia wananchi.

Shekalaghe ameongeza kuwa wao wanaamini kuwa ili mtu aweze kumtumikia Mungu  ni lazima awe na afya njema, hivyo kupitia msaada huo wa vifaa wagonjwa watahudumiwa na kurudi katika hali zao kawaida na kuendelea kumtumikia Mungu na kufanya shughuli za maendeleo.

Naye Mganga Mfawidhi wa Hospitali Teule ya Mkoa wa Simiyu, Dkt.Fredrick Mlekwa akitoa shukrani kwa Life Ministry amesema, msaada huo umefika katika wakati muafaka ambapo amesisitiza kuwa uongozi wa Hospitali umefarijika kupata vifaa hivyo ambavyo vitawasaidia kutoa huduma bora kwa wananchi.

“Tumefarijika sana kupata msaada huu na walengwa ambao ni wananchi watapata huduma bora  kupitia vifaa hivi, naomba nitoe wito kwa Mashirika mengine  ya madhehebu ya dini  kuendelea kutusaidia kwa kuwa Hospitali hii inawahudumia watu wenye mahitaji mbalimbali” alisema Dkt.Mlekwa.

Baadhi ya Vifaa vilivyotolewa na Life Minisry ni pamoja na viti vya kubebea wagonjwa(wheel chairs), vifaa vya viungo bandia, vifaa vya huduma za meno, vifaa vya vinavyotumika katika upasuaji, bandeji na mabomba ya sindano.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.  Anthony  Mtaka(katikati), Mganga Mfawidhi wa Hospitali Teule ya Mkoa, Dkt. Fredrick Mlekwa(kushoto) wakipokea baadhi ya vifaa vilivyotolewa  Life Ministry kutoka kwa Mkurugenzi wa Shirika hilo la dini, Bw. Dismas Shekalaghe(Kulia)

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.  Anthony  Mtaka(katikati), Mganga Mfawidhi wa Hospitali Teule ya Mkoa, Dkt. Fredrick Mlekwa(kushoto) wakikabidhiwa viti vya kubebea wagonjwa na Mkurugenzi wa Life Ministry Bw. Dismas Shekalaghe (kulia).  ambavyo ni miongoni mwa vifaa vilivyotolewa  Shirika hilo la Kikristo kwa Hospitali Teule  ya Mkoa wa Simiyu.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.  Anthony  Mtaka akizungumza na wachungaji wa madhehebu ya Kikristo wakati wa makabidhiano ya vifaa tiba vilivyotolewa na Shirika la Kikristo la Life Ministry kwa Hospitali Teule ya Mkoa wa Simiyu, mjini Bariadi

Mganga Mfawidhi wa Hospitali Teule  ya  Mkoa wa Simiyu, Dkt.Fredrick Mlekwa akizungumza wakati wa makabidhiano ya vifaa tiba vilivyotolewa na Shirika la Kikristo la Life Ministry kwa Hospitali Teule ya Mkoa wa Simiyu, mjini Bariadi.
Mkurugenzi wa Life Ministry hapa nchini, Dismas Shekalaghe(wa pili kulia) wakati wa makabidhiano ya vifaa tiba vilivyotolewa na Shirika hilo la Kikristo kwa Hospitali Teule ya Mkoa wa Simiyu, mjini Bariadi.
Baadhi ya Viti vya kubebea wagonjwa(wheel chairs) vilivyotolewa na Shirika la Madhehebu ya Kikristo la Life Ministry kwa Hospitali Teule ya Mkoa wa Simiyu, mjini Bariadi.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!