Friday, March 24, 2017

RAS Sagini: Viongozi, Watumishi Shirikianeni na Wadau Kuboresha Huduma Za Afya

Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg. Jumanne Sagini  ametoa wito  kwa viongozi na watumishi mkoani humo kushirikiana na wadau mbalimbali wenye nia njema ya kuunga mkono juhudi za Serikali katika uboreshaji wa huduma za afya kwa wananchi.

Sagini ameyasema hayo leo katika ufunguzi wa kikao cha kuutambulisha Mradi wa USAID Boresha Afya, kilichofanyika katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki Mjini Bariadi.

Amesema Simiyu ni miongoni mwa mikoa saba ambayo Mradi wa USAID Boresha Afya utatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano (2017-2022), hivyo akawataka viongozi na wataalam kushirikiana na wadau hao kuhakikisha mradi huu unasaidia kubadilisha mfumo wa utoaji huduma za afya katika maeneo yaliyobainishwa.  

Aidha, ameongeza kuwa ujio wa Mradi huu katika Halmashauri zote za Mkoa wa Simiyu uwe ni chachu ya kuhakikisha huduma za Afya zinapatikana kirahisi kwa wananchi wa Mkoa huo.

“Ndugu washiriki nichukue nafasi hii kushukuru mashirika na wadau mbalimbali wanaounga mkono juhudi za Serikali, natoa wito kwa Idara ya Afya Mkoa na wilaya kutoa ushirikiano wa karibu kuhakikisha mradi huu unafanikiwa na unatoa matunda tarajiwa”

Sagini amesema Serikali inafanya juhudi za kukabiliana na viashiria visivyoridhisha katika utoaji huduma za afya ikiwemo kupunguza vifo vya akina mama vitokanavyo na uzazi ambavyo vinafikia 556 kwa kila vizazi hai 100,000 kwa sasa.

“Vifo hivi vinachangiwa na mambo mengi, ikiwemo mahudhurio hafifu ya wajawazito kliniki katika theluthi ya kwanza ya mimba kwa asilimia 24 na wajawazito wanaohudhuria kliniki kwa mahudhurio manne au zaidi kwa asilimia 51” amesema Sagini.

Sagini amesisitiza kuwa mafanikio katika suala la kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi halitatatuliwa na sekta ya Afya pekee bali kwa ushirikiano wa sekta zote za maendeleo.

Kwa upande wake Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa wa Simiyu, Dkt.Fredrick Mlekwa amesema Mradi huu umekuja katika wakati muafaka ambao mkoa unafanya jitihada mbalimbali za kukabiliana na vifo vya akina mama vitokanavyo na uzazi na vifo vya watoto wadogo chini ya miaka mitano.

Naye Dkt.Joseph Masenga kutoka USAID Boresha Afya amesema mradi huo katika mkoa wa Simiyu utajikita kuunga mkono juhudi za Serikali katika huduma za uzazi wa mpango, Malaria, Huduma za Afya ya Mtoto, huduma za Uzazi, Lishe na maeneo mengine mtambuka ikiwemo jinsia, heshima na ushirikishwaji wa jamii katika huduma za Afya (ngazi ya jamii).

Kwa upande wake Mratibu wa Mradi wa USAID Boresha Afya wa Mkoa wa Simiyu , Dkt. Charles Suka amesema utambulisho wa mradi huo umefanyika kwa viongozi na watendaji wa mkoa huo ili wawe na uelewa wa pamoja ili waweze kutoa mchango katika utengenezaji wa mpango mkakati wa kupunguza vifo vya mama na mtoto na kuweka mpango wa utekelzaji wa  wa mradi kwa miaka mitano.


Mradi wa USAID Boresha Afya Mkoani Simiyu, unatekelezwa kwa ubia wa mashirika ya Jhpiego, Engenderhealth katika mikoa ya Kanda ya Ziwa na Magharibi ambayo ni Simiyu, Mara,Kagera, Kigoma, Shinyanga, Geita na Mwanza katika kipindi cha miaka mitano(2017-2022).
Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg. Jumanne Sagini  akizungumza na Viongozi na Wataalam wa Afya mkoani humo (hawapo pichani) katika ufunguzi wa kikao cha kuutambulisha Mradi wa USAID Boresha Afya, kilichofanyika leo  katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki Mjini Bariadi
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Dkt.Mageda Kihulya akizungumza na Viongozi na Wataalam wa Afya mkoani humo (hawapo pichani) katika ufunguzi wa kikao cha kuutambulisha Mradi wa USAID Boresha Afya, kilichofanyika leo  katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki Mjini Bariadi
Viongozi na Wataalam wa Afya mkoani Simiyu wakimsikiliza Katibu Tawala Mkoa wa Mkoa huo, Ndg. Jumanne Sagini (hayupo pichani)  katika ufunguzi wa kikao cha kuutambulisha Mradi wa USAID Boresha Afya, kilichofanyika leo katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki Mjini Bariadi
Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg. Jumanne Sagini (wa nne kushoto)  akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi na Wataalam wa Afya mkoani humo baada ya ufunguzi wa kikao cha kuutambulisha Mradi wa USAID Boresha Afya, kilichofanyika leo katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki Mjini Bariadi

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!