Wednesday, March 1, 2017

WANANCHI WAOMBWA KUTOA USHIRIKIANO KWA WATAFITI VIASHIRIA NA MATOKEO YA UKIMWI

Na Stella Kalinga
Serikali Mkoani Simiyu  imetoa wito kwa wananchi na wadau mbalimbali Mkoani humo kutoa ushirikiano kwa  wataalam wa Utafiti wa Viashiria na Matokeo ya Ukimwi(Tanzania HIV Impact Survey-THIS)  ili takwimu zitakazopatikana  ziendane na hali halisi ya mkoa.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Bariadi Mhe.Festo Kiswaga  wakati  akisoma hotuba kwa Niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe.Anthony Mtaka  leo mjini Bariadi , katika mkutano wa wadau wa Utafiti huo unaotarajiwa kufanyika mwezi Machi mwaka huu Mkoani humo.

Amesema kwa kuwa utafiti huo unafanyika katika ngazi ya kaya kwa kuzingatia sampuli iliyopendekezwa na Wataalam   ambapo  amesisitiza elimu itolewe kwa familia zitakazochaguliwa kupimwa ili ziwe tayari kupima na kupokea majibu.

“Mtakubaliana nami kwamba sera na mipango bora hutegemea upatikanaji wa takwimu sahihi na bora , hivyo nitoe wito kwa wadau wote wa mkoa wetu kutoa ushirikiano wa karibu kwa watafiti ili kufanikisha zoezi hili muhimu kwa Taifa letu” alisema.

Akitoa ufafanuzi wa Utafiti wa Viashiria na Matokeo ya Ukimwi Mkoani Simiyu, Bibi.Mihayo Bupamba  kutoka Shirika lisilo la Kiserikali la ICAP amesema utafiti utafanyika katika ngazi ya kaya kupitia sampuli (baadhi ya kaya) zilizochaguliwa kwenye maeneo tisa (09) kutoka wilaya zote mkoani humo, ambapo amesisitiza kuwa utafiti huo utahusisha upimaji wa hiari wa Virusi vya Ukimwi, Homa ya Ini na Kaswende baada ya watafiti kuzungumza na walengwa.

Bupamba amesema  utafiti huu unalenga kukusanya taarifa za maambukizi mapya ya VVU, kiwango cha VVU mwilini kwa wanaoishi na VVU, wastani wa maambukizi ya VVU kwa watu wa rika zote,wingi wa chembechembe za kinga mwilini (CD4 T-cell count), viashiria vya usugu wa dawa,na kiwango cha maambukizi ya kaswende na homa ya ini kwa watu wenye umri wa miaka 15 na zaidi.

Ameongeza kuwa utafiti huo pia unatarajia kukusanya taarifa za upatikanaji na utumiaji wa huduma zitolewazo katika kudhibiti maambukizi ya VVU na UKIMWI na viashiria vya tabia hatarishi zinazochangia maambukizi ya VVU ambayo kwa mujibu wa tafiti zilizopita inaonekana kupungua kutoka asilimia 7 mwaka 2013 mpaka asilimia 5.1 mwaka 2011.

“ Utafiti wa awamu hii ni wa tofauti na tafizi zilizofanyika miaka ya nyuma, unahusisha watu wa rika zote katika kaya zilizochaguliwa... na wote wataopima watapewa matokeo yao papo hapo”alisema

Bupamba amesema kupitia utafiti huo kaya/ familia zitatambua hali zao kiafya na wale watakaokutwa na maambukizi wataanzishiwa huduma za matibabu,kusisitiza kuwa pia Serikali itapata takwimu zitakazotumika kupanga sera na mipango mbalimbali kwa manufaa ya wananchi na Taifa kwa ujumla.

Wakizungumza katika mkutano huo Wawakilishi wa Madhehebu ya Dini Sheikh wa Mkoa wa Simiyu, Mahamoud Kalokola na Mchungaji wa Kanisa la AICT, Josephati Magori wamesema viongozi wa dini watatoa ushirikiano kwa watafiti katika kuwahamasiha wananchi na wakawataka  watafiti hao kuwashirikisha viongozi wa dini hususani katika ngazi ya Kata na Vijiji au Mitaa kila watakapofanya utafiti.

Naye  Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg.Jumanne Sagini amewahakikishia wataalam na watafiti wote kuwa Serikali na Watendaji mkoani humo itatoa ushirikiano wa dhati kila watakapohitajika.
Utafiti wa Viashiria na Matokeo ya Ukimwi ambao umeshaanza kutekelezwa kwa baadhi ya mikoa utatekelezwa  nchi nzima katika maeneo 525 utazifikia  kaya 16,000 wananchi 42, 000 ambapo kati ya hao watoto ni 8,000.

Mkutano wa wadau wa utafiti huo umewahusisha viongozi wa Serikali ngazi ya mkoa na Wilaya, watendaji wakiwepo waratibu wa ukimwi Mkoa na Wilaya, watakwimu, maafisa maendeleo  ya jamii, viongozi wa madhehebu ya dini wadau wengine kutoka mashirika yasiyo ya Kiserikali.

Mkuu wa Wilaya ya Bariadi Mhe.Festo Kiswaga(wa pili kulia)  akizungumza na wadau wa Utafiti wa Viashiria na Matokeo ya Ukimwi mjini Bariadi leo, kwa Niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu utafiti unatarajiwa kuanza mwezi huu.
Baadhi ya Viongozi na Watendaji wa Serikali,viongozi wa Dini na wadau wengine wa Utafiti wa Viashiria na Matokeo ya Ukimwi, wakimsikiliza Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe.Festo Kiswaga katika mkutano uliofanyika leo mjini Bariadi.
Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg.Jumanne Sagini akizungumza na wadau wa Utafiti wa Viashiria na Matokeo ya Ukimwi katika Mkutano uliofanyika leo mjini Bariadi , utafiti ambao unatarajiwa kuanza kufanyika Mkoani Humo mwezi huu.
Mdau wa Utafiti wa Viashiria na Matokeo ya Ukimwi  Bibi.Mihayo Bupamba  kutoka Shirika lisilo la Kiserikali la ICAP akiwasilisha mada kwa wadau wa utafiti huo mkoani Simiyu katika mkutano uliofanyika Mjini Bariadi.

Sheikh wa Mkoa wa Simiyu,Mahamoud Kalokola akichangia mada katika mkutano wa wadau w Utafiti wa Viashiria na Matokeo ya Ukimwi mkoani humo katika mkutano uliofanyika Mjini Bariadi.






0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!