Tuesday, September 20, 2016

RC AWATAKA WATENDAJI WA HALMASHAURI NA MADIWANI KUTOINGIZA MASLAHI BINAFSI KATIKA MIRADI YA BARABARA

Na Stella Kalinga
Madiwani na watendaji wa Halmashauri wameaswa kuacha kuingiza maslahi binafsi katika ujenzi wa miradi ya barabara ili kufanya miradi kusimamiwa na kujengwa katika kiwango kinachostahili.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony John Mtaka katika kikao cha Bodi ya Barabara kilichofanyika katika Ukumbi wa kanisa Katoliki Mjini, Bariadi.

Mtaka amesema ili miradi ya ujenzi wa barabara isimamiwe vizuri na iweze kujengwa kwa viwango vinavyotakiwa madiwani na watendaji wasiwe sehemu ya wazabuni au wakandarasi wa miradi hiyo, ili waweze kuwasimamia wakandarasi wa miradi hiyo na kuwachukulia hatua pale wanapotekeleza miradi chini ya kiwango.

Aidha, Mtaka amewataka Wenyeviti wa Halmashauri kusimamia kwa umakini vikao vya mabaraza ya madiwani vya kuamua matengenezo ya barabara ili kipaumbele cha kwanza kiwe ni kwa barabara ambazo zimeharibika sana.

“Wenyeviti wa Halmashauri waongozeni madiwani kuepuka ubinafsi katika miradi ya barabara ambapo kila Diwani anataka apewe fedha kidogo kidogo ya kujenga au kukarabati hata kama fedha hiyo ni kidogo sana. Kipaumbele cha kwanza kiwe ni barabara ambazo zimeharibika sana au hazipitiki kabisa katika Halmashauri” alisema Mtaka.

Sanjali na hilo Mkuu huyo wa Mkoa amewataka viongozi wa ngazi zote kutoa elimu kwa wananchi juu ya utunzaji wa alama za barabarani zinazowekwa na Wakandarasi na Wakala wa Barabara(TANROADS) pamoja na kuacha kupitisha mifugo barabarani ambayo inasababisha mmomonyoko wa udongo ili barabara zidumu.

Naye Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Jumanne Sagini amesisitiza Wahandisi wa Halmashauri kuhakikisha wanaweka alama katika mipaka ya hifadhi ya barabara ili iwe rahisi kutambua na kuepuka maeneo hayo kuvamiwa na kutumiwa tofauti na yalivyokusudiwa. 
  
Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Maswa Mashariki, Mhe. Satanslaus Nyongo amesema Wakala wa Barabara(TANROADS) kwa kushirikiana na Wabunge wa Mkoa wa Simiyu, wafanye jitihada za kuzungumza na Waziri mwenye dhamana na ujenzi wa Barabara ili kipande cha barabara cha Maswa hadi Bariadi chenye kilomita 50 kitengewe fedha za ujenzi kwa kiwango cha lami; kwa kuwa barabara ya Mwigumbi-Maswa-Bariadi –Lamadi itakapokamilika itaweza kuunganisha Mkoa wa Simiyu na mikoa mingine hivyo kuufungua kiuchumi.

Akizungumzia barabara hiyo Meneja wa Mkoa wa Wakala wa Barabara(TANROADS) Mhandisi Albert Kent amesema kipande cha Lamadi-Bariadi kimekamilika, mkandarasi anaendelea na ujenzi wa kipande cha Mwigumbi-Maswa na kipande cha Maswa hadi Maswa kitajengwa kulingana na kadri kaitakavyotengewe fedha katika bajeti, kwa kuwa utekelezaji wa mradi huo unategemea upatikanaji wa fedha.

Mkoa wa Simiyu una mtandao wa barabara zenye jumla ya kilomita 4,730.95 ambazo zimegawanyika katika makundi yafuatayo:-Barabara kuu kilometa 334.72, barabara za Mkoa kilometa532.30, barabara za wilaya kilometa 2420.5 na barabara za vijijini 1451.53; kati ya hizi kilomita 141.76 zina kiwango cha lami, kilomita 2453.59 kiwango cha chanagarawe na kilometa 2134.7 za kiwango cha udongo. 


Kutoka kushoto, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Simiyu, Dkt. Titus Kamani, Mkuu wa mkoa wa Simiyu, Mhe. Antony Mtaka, Katibu Tawala Mkoa, Jumanne Sagini na Mbunge wa Jimbo la Meatu Mhe. Luhaga Mpina wafuatilia mjadala katika kikao cha Bodi ya Barabara ya Mkoa, kilichofanyika Mjini Bariadi kwa lengo la kupanga na kujadili maendeleo ya Barabara katika Mkoa


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony John Mtaka (kulia) akizungumza na wajumbe wa Bodi ya Barabara ya Mkoa huo (hawapo pichani) katika kikao cha Bodi hiyo kilichofanyika Mjini Bariadi kwa lengo la kupanga na kujadili maendeleo ya barabara katika mkoa (kushoto) ni Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Simiyu, Dkt. Titus Kamani.

Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kisesa, Mhe. Luhaga Mpina (kulia) akichangia jambo katika Kikao cha Bodi ya Barabara ya Mkoa, kilichofanyika Mjini Bariadi Mkoni Simiyu kwa lengo la kupanga na kujadili maendeleo ya Barabara katika Mkoa , (kushoto) Katibu Tawala wa Mkoa huo, Jumanne Sagini.
Mbunge wa Jimbo la Maswa Mashariki, Mhe. Stanslaus Nyongo (kushoto) akichangia jambo katika Kikao cha Bodi ya Barabara ya Mkoa, kilichofanyika Mjini Bariadi Mkoni Simiyu kwa lengo la kupanga na kujadili maendeleo ya Barabara katika Mkoa
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Simiyu, Dkt. Titus Kamani akizungumza na Wajumbe wa Bodi ya Barabara kilichofanyika Mjini Bariadi kwa lengo la kupanga na kujadili maendeleo ya Barabara katika Mkoa huo. 
Baadhi ya Wajumbe wa Bodi ya Barabara ya Mkoa wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony J. Mtaka ktika kikao cha Bodi ya Barabara kilichofanyika Mjini Bariadi kwa lengo la kupanga na kujadili maendeleo ya Barabara katika Mkoa.
Mkuu wa Wilaya ya Maswa, Mhe. Dkt Seif Shekalaghe (wa pili kushoto, mstari wa pili) akichangia jambo katika Kikao Cha Bodi ya Barabara kilichofanyika Mjini Bariadi kwa lengo la kupanga na kujadili maendeleo ya Barabara katika Mkoa
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony John Mtaka (kushoto) akizungumza na wajumbe wa kikao cha Bodi ya Barabara ya Mkoa(hawapo pichani) katika kikao cha Bodi ya hiyo kilichofanyika Mjini Bariadi kwa lengo la kupanga na kujadili maendeleo ya barabara katika mkoa, (kulia) Katibu Tawala Mkoa Simiyu, Jumanne Sagini.
Meneja wa Mkoa wa Wakala wa Barabara(TANROADS), Mhandisi Albert Kent akiwasilisha taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa Barabara kwa wajumbe wa kikao cha Bodi ya Barabara ya Mkoa kilichofanyika Mjini Bariadi,  kwa lengo la kupanga na kujadili maendeleo ya Barabara katika Mkoa.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, Mhe. Pius Machungwa akichangia jambo katika Kikao Cha Bodi ya Barabara kilichofanyika Mjini Bariadi kwa lengo la kupanga na kujadili maendeleo ya Barabara katika Mkoa.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!