Tuesday, September 26, 2017

TCRA YATOA ELIMU KUHUSU HUDUMA YA KUHAMA MTANDAO MMOJA WA SIMU KWENDA MWINGINE BILA KUBADILI NAMBA

Mamlaka ya Mawasiliano hapa nchini (TCRA) imetoa elimu kuhusu huduma ya kuhama kutoka Mtandao mmoja wa Simu kwenda Mtandao mwingine bila kubadili Namba ya Simu(Mobile Number Portability- MNP) mkoani Simiyu.

Akizungumza na waandishi wa Habari Mjini Bariadi Mhandisi Mwandamizi wa Mawasiliano Mwesigwa Felician kutoka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania( TCRA), amesema huduma hii ni ya hiari  na inampa uhuru na kumwezesha mtumiaji wa huduma ya mawasiliano kuhamia mtandao wowote anaoutaka na kuendelea kupata mawasiliano bila kulazimika kubadili namba yake ya simu.

“Namba ya simu ya Mteja itabaki ile ile na itakuwa ni kitambulisho chake, yaani (NAMBA YAKO KITAMBULISHO CHAKO) kokote atakapohamia watu watampata, hakuna haja ya kuwataarifu marafiki,familia,  wafanyakazi wenzake au washirika wenzake katika shughuli zake kama ilivyo sasa. Tunatoa elimu hii kwenu waandishi wa habari ili na ninyi muifikishe kwa wananchi kupitia kazi zenu” amesema Mhandisi Mwesigwa.

Amesema huduma hii inamwezesha mtumiaji wa huduma za mawasiliano kuchagua mtoa huduma mwenye huduma bora zaidi(quality of service), huduma nzuri kwa wateja(customer care services), ubunifu katika kutoa huduma zake hivyo kuongeza ushindani kwenye sekta ya mawasiliano na kuchochea utoaji huduma bora na zenye gharama nafuu.

Ameongeza kuwa huduma hii inatolewa kwa wateja wa malipo ya kabla(pre paid) na malipo baada ya huduma(post paid) kupitia vituo vya mauzo au wakala anayetambuliwa mtoa huduma (Makampuni ya Mawasiliano/Simu), ambapo watumiaji wa mawasiliano watakaohitaji huduma hiyo watatembelea maeneo hayo ili kupewa utaratibu wa kuhama.

“Mtu anayetaka kuhama kutoka mtandao mmoja wa simu kwenda mwingine bila kubadiliha namba yake anapaswa kufika katika Vituo vya mauzo au wakala wa mtandao anaotaka kuhamia, kupata utaratibu na akiona ipo haja ya kuhama tena itamlazimu akae kwa mtoa huduma huyo mpya kwa muda usiopungua siku 30 kabla ya kurudi kwa yule awali au kuhamia kwa mwingine” amesisitiza Mhandisi Mwesigwa.

Kwa upande wake Naibu Mkurugenzi wa Masuala ya Watumiaji wa Bidhaa za Mawasiliano, kutoka Mamlaka ya Mamlaka ya Mawasiliano, Thadayo Ringo amesema huduma hii hapa nchini imeanza Machi Mosi mwaka huu na mpaka kufikia mwezi Juni 2017 takribani wananchi 15,000 walikuwa wameshaitumia huduma hii.

Aidha, Ringo ameongeza kuwa Tanzania ni nchi ya Tisa Barani Afrika kutoa huduma hii katika mawasiliano, ambapo amebainisha nchi nyigine zinazotoa huduma ya kuhama kutoka mtandao mmoja kwenda mwingine bila kubadili namba (MNP) kuwa ni Kenya, Rwanda, Botswana, Afrika ya Kusini, Ghana, Senegal, Namibia na Misri.


Huduma hii ya kuhama kutoka mtandao mmoja kwenda mwingine bila kubadili namba ya simu ya kiganjani, inatolewa kwa watumiaji ambao namba zao zinatumika yaani hazijafungiwa au kusimamishwa kwa muda.
Mhandisi Mwandamizi wa Mawasiliano Mwesigwa Felician kutoka TCRA akizungumza na waandishi wa habari(hawapo pichani) Mjini Bariadi mkoani Simiyu wakati wa kikao kilicholenga kutoa Elimu kuhusu huduma ya kuhama kutoka Mtandao mmoja wa Simu kwenda Mtandao mwingine bila kubadili Namba ya Simu(Mobile Number Portability- MNP).
Baadhi ya waandishi wa Habari wa Mkoa wa Simiyu wakisikiliza Mhandisi Mwandamizi wa Mawasiliano Mwesigwa Felician kutoka TCRA(hayupo pichani) wakati wa kikao cha kutoa elimu kuhusu huduma ya kuhama kutoka Mtandao mmoja wa Simu kwenda Mtandao mwingine bila kubadili Namba ya Simu(Mobile Number Portability- MNP).
Naibu Mkurugenzi wa Masuala ya Watumiaji wa Bidhaa za Mawasiliano, kutoka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania(TCRA), Thadayo Ringo akizungumza na waandishi wa habari Mjini Bariadi mkoani Simiyu wakati wa kikao kilicholenga kutoa Elimu kuhusu huduma ya kuhama kutoka Mtandao mmoja wa Simu kwenda Mtandao mwingine bila kubadili Namba ya Simu(Mobile Number Portability- MNP).
Baadhi ya waandishi wa Habari wa Mkoa wa Simiyu wakisikiliza Mhandisi Mwandamizi wa Mawasiliano Mwesigwa Felician kutoka TCRA wakati wa kikao cha kutoa elimu kuhusu huduma ya kuhama kutoka Mtandao mmoja wa Simu kwenda Mtandao mwingine bila kubadili Namba ya Simu(Mobile Number Portability- MNP).



0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!