Tuesday, August 14, 2018

MWENGE WA UHURU KUPITIA MIRADI 36 SIMIYU YENYE THAMANI YA ZAIDI YA SHILINGI BILIONI NANE

Jumla ya miradi 36 yenye thamani ya shilingi  bilioni 8.4  iliyopo katika Halmashauri sita za Mkoa wa Simiyu itapitiwa na Mwenge wa Uhuru ambao umeanza rasmi mbio zake mkoani humo, Agosti 15, 2018.
Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka wakati akisoma salamu za mkoa wakati wa mapokezi ya Mwenge wa Uhuru katika Kijiji cha bukundi wilayani Meatu ukitokea wilaya ya Mkalama Mkoani Singida Agosti 14, 2018.

Mtaka amesema kuwa miradi hiyo inayotarajiwa kupitiwa  na Mwenge wa Uhuru ni kutoka katika Idara  ya Elimu, Afya, Maji, Viwanda, Kilimo, Maliasili, Barabara,Utawala, Sekta binafsi na Vijana na Wanawake.

Akizungumzia Ujumbe wa Mwenge wa Uhuru mwaka 2018 ambao umejikita zaidi katika Elimu kwa kauli Mbiu “ELIMU NI UFUNGUO WA MAISHA; WEKEZA SASA KWA MAENDELEO YA TAIFA LETU” amesema, Elimu ni kipaumbele cha kwanza kwa mkoa huo, ambapo wameweka mikakati mbalimbali ya kuinua elimu na ujenzi wa miundombinu ya elimu.

“ Simiyu ni mkoa pekee ambao wanafunzi wa madarasa ya mitihani wanakaa katika kambi za kitaaluma, pia ufaulu wa wanafunzi wetu umeongezeka mfano, mwaka 2017 mkoa wa Simiyu ulikuwa wa 26 Kitaifa kati ya mikoa 31 lakini mwaka 2018 mkoa umeshika nafasi ya 10 katika matokeo ya kidato cha Sita” alisema.

Aidha, Mtaka amesema Simiyu inaendelea kuboresha miundombinu ya elimu kwa kushirikisha jamii na wadau mbalimbali ikiwa na mkakati wa kujenga shule tatu ambazo ni Shule ya Sekondari ya Ufundi Simiyu, Shule ya Sekondari ya Wasichana na Shule ya Sekondari ya Wavulana.

Hata hivyo Mwenge wa Uhuru ukiwa wilayani Meatu umepita katika miradi mbalimbali ikiwa ni pamoja na mradi wa vyumba vya madarasa katika shule shikizi ya Mwanyahina, Mradi wenye majengo manne katika Hospitali ya Wilaya; (jengo la wodi ya wazazi, jengo la upasuaji, maabara na nyumba ya mtumishi), mradi wa ujenzi wa mahakama ya mwanzo Itinje na mradi wa ushonaji wa wanawake wa Kijiji cha Mwamishali.

Akizungumza kwa nyakati tofauti katika miradi iliyopitiwa na Mwenge wa Uhuru, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2018, Ndg. Charles Francis Kabeho amewataka viongozi na watendaji kusimamia miradi ya maendeleo kwa weledi na kuhakikisha inatekelezwa kwa wakati kwa  viwango vinavyohitajika na kuzingatia thamani ya fedha(value for maoney) ili wananchi wapate huduma
.
“Utawala wa Awamu ya tano unataka watu wafanye kazi na kuwajibika kweli,tunaposema HAPA KAZI TU Mhe. Rais anamaanisha, tukisimamia miradi kwa ulegelege hatutaweza kufika, inawezekana hata kuchelewa kwa miradi ni kwa sababu watu wanataka maslahi yao na kusababisha huduma za kijamii zinakwama ili wao wanufaike, watendaji wa aina hiyo awamu ya tano hatuwahitaji” alisema Kabeho

Kwa upande wake mkuu wa Wilaya ya Meatu, Dkt. Joseph Chilongani akizungumza mara baada ya Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa kuweka jiwe la msingi mradi wa madarasa ya shule shikizi ya Mwanyahina amesema Viongozi wa wilaya watasimamia ujenzi wa mradi huo na kuhakikisha unajengwa  kwa viwango na kwa wakati ili shule hiyo iwanufaishe wananchi wa vijiji jirani vinavyoizunguka.

Mwenge wa Uhuru umeanza mbio zake mkoani Simiyu katika Wilaya ya Meatu Agosti 14, 2018, Agosti 15 utakuwa halmashauri ya Wilaya ya Itilima, Agosti 16 Halmashauri ya mji wa Bariadi, Agosti 17 Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi, Agosti 18 Halmashauri ya Wilaya ya Busega, Agosti 19 Halmashauri ya Wilaya ya Maswa na tarehe Agosti 20, utakabidhiwa mkoani Shinyanga.

MWISHO


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka(kulia) akipokea Mwenge wa Uhuru kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Dkt. Rehema Nchimbi katika Kijiji cha Bukundi wilayani Meatu, Agosti 14, 2018.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka(kushoto) akimkabidhi Mwenge wa Uhuru Mkuu wa Wilaya ya Meatu, Mhe. Dkt. Joseph Chilongani mara baada ya Mapokezi ya Mwenge wa Uhuru katika Kijiji cha Bukundi ukitokea Wilayani Mkalama, mkoani Singida, Agosti 14, 2018.
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2018, Ndg. Charles Francis Kabeho akiondoka mara baada ya kuweka jiwe la msingi ujenzi wa Vyumba vya madarasa katika Shule shikizi ya Mwanyahina wilayani Meatu, Agosti 14, 2018.
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2018, Ndg. Charles Francis Kabeho akikata utepe kuashiria ufunguzi wa Klabu ya Wapinga Rushwa katika Shule ya Sekondari ya Bukundi,wilayani Meatu, Agosti 14, 2018.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2018, Ndg. Charles Francis Kabeho akisalimiana na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka mara baada ya makabidhiano ya Mwenge wa Uhuru kati ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu na Mkuu wa Mkoa wa Singida, katika Kijiji ca Bukundi, wilayani Meatu, Agosti 14, 2018.
Wananchi wa Wilaya ya Meatu   jamii ya Wataturu wakitoa burudani kwa wananchi wa Bukundi kabla ya makabidhiano ya Mwenge wa Uhuru, kati ya Mkoa wa Simiyu na Mkoa wa Singida katika Kijiji cha Bukundi wilayani humo, Agosti 14, 2018.

Mkimbiza Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2018, Ndg. Issa Abass Mohamed kutoka Kusini Pemba akisalimiana na Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini mara baada ya kukabidhi rasmi kwa viongozi wa Mkoa wa Simiyu kutoka Singida katika Kijiji cha Bukundi wilayani Meatu Agosti 14, 2018.
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2018, Ndg. Charles Francis Kabeho(wa pili kulia) akishangilia pamoja na wakina mama wa kikundi cha ushonaji Mwanyahina wilayani MEATU baada ya kuwafungulia mradi wao, Agosti 14, 2018.


0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!