Wednesday, May 3, 2017

NSSF YARIDHIA KUTOA BILIONI 1.5 UPANUZI KIWANDA CHA CHAKI SIMIYU

Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa NSSF imeridhia kutoa mkopo  wa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya upanuzi wa kiwanda cha chaki kilichopo wilaya ya Maswa Mkoani Simiyu.

Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Meneja wa Mipango na Uwekezaji wa NSSF  Bibi. Radhia Tambwe katika mahojiano maalum na waandishi wa Habari mara baada ya kikao cha wadau wa uwekezaji Mkoani Simiyu kilichofanyika Kata ya Lamadi wilayani Busega ambacho kimewahusisha wadau mbalimbali wa uwekezaji mkoani humo.

Bibi.Radhia amesema Bodi imefanya uamuzi huo baada ya kupitia maombi ya Halmashauri ya Wilaya ya Maswa na kuona kuwa mradi wa kiwanda cha chaki una tija kwa kuwa umewashirikisha vijana hivyo kiwanda kitakapopanuliwa kitaongeza wigo wa ajira kwa vijana, pato la wilaya na kuokoa fedha za kigeni zinazotumika kuagiza chaki nje ya nchi.

Aidha, amepongeza utekelezaji wa Kauli Mbiu ya “Wilaya Moja Bidhaa Moja” mkoani Simiyu katika Ujenzi wa Uchumi wa Viwanda ambapo amesema kupitia viwanda vitakavyoanzishwa katika kila wilaya chini ya Kauli Mbiu hii mkoa utatengeneza ajira kwa wananchi wa ndani na nje ya mkoa.
Bi. Radhia pia ametoa wito kwa wadau wengine kuunga mkono miradi ya ujenzi wa Uchumi wa Viwanda Mkoani Simiyu kwa kuwa ni miradi yenye tija kwa kuzingatia kuwa  malighafi zinazotumika zinapatikana hapa nchini na soko lake kubwa liko hapa nchini.

“Watanzania tubadilike tusikubali kila mara kugeuzwa supermarket, tuzalishe bidhaa zetu na kutumia bidhaa zetu wenyewe tujivunie tulivyonavyo ili tuweze kuendeleza nchi yetu na hatimaye Tanzania na sisi tuwe nchi yenye uchumi wa kati” alisema.

Naye  Mkurugenzi wa Benki ya Azania Ndg.Charles Jackson Itembe amesema benki hiyo iko tayari na inaunga mkono uwekezaji katika sekta ya viwanda unaofanywa na Halmashauri za Mkoa wa Simiyu chini ya Kauli mbiu ya “Wilaya Moja Bidhaa Moja” kwa kutoa uwezeshaji kifedha katika miradi iliyoaanishwa na Halmashauri husika kupitia mikopo.

Kwa upande wake Mtaalam Mbobezi wa Viwanda, Ndg. Ndaki Munyeti amesema Mkoa wa Simiyu umejipanga katika kuwashirikisha Wataalam mbalimbali katika kuchagua teknolojia itakayotumika katika viwanda vilivyopo na vitakavyoanzishwa ambayo ndiyo hatua muhimu katika ujenzi wa viwanda inayoweza kusaidia kupata bidhaa bora na kufanya viwanda vikawa endelevu.

Awali akizungumza katika ufunguzi wa kikao cha wadau wa uwekezaji wa Mkoa wa Simiyu Mkuu wa Mkoa huo, Anthony Mtaka amesema pamoja na NSSF na Benki ya Azania kukubali kuunga mkono juhudi za Ujenzi wa Uchumi wa Viwanda Mkoani Simiyu amesema Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) wameahidi kutoa fedha za upembuzi yakinifu kwa mradi utakaotekelezwa katika kila wilaya(Wilaya Moja Bidhaa Moja).

Mtaka amewataka viongozi kila mmoja awajibike ipasavyo katika eneo lake kwa kuwa wale walioteuliwa waliaminiwa na Mhe.Rais na waliochaguliwa waliaminiwa na wananchi hivyo watimize wajibu wao kuhakikisha viwanda vinasimama na kero za wananchi zinatatuliwa.

“Viongozi wenzangu wa kuteuliwa tunapaswa kuwajibika, Mhe.Rais aliacha watu wengi akatuamini akatuteua sisi, Waheshimiwa madiwani wananchi waliwaamini kuwachagua, ni lazima tuioneshe dunia kuwa inawezekana; natamani mwaka 2020 tutengeneze kura siyo mikutano ya hadhara, kila atakapo pita Mhe.Rais kuwe na kitu ambacho wananchi wanajivunia kupitia kazi zetu sisi” alisema.

Kikao cha wadau wa uwekezaji kiliwahusha wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa, Watalaam wa Sekretarieti ya Mkoa, Wakuu wa Wilaya,Wenyeviti na Makamu wenyeviti wa Halmashauri,Wakurugenzi wa Halmashauri,Wajumbe wa Kamati za Fedha za Halmashauri, Maafisa Mipango, Wachumi, Wataalam kutoka Benki ya Azania, NSSF na Watalaam wa Viwanda na Masoko.

Katika kikao hicho maandiko ya miradi ya uanzishwaji viwanda kutoka katika Halmashauri zote sita za Mkoa wa Simiyu yaliwasilishwa kwa wadau hao ambayo ni upanuzi wa kiwanda cha chaki na kiwanda cha kutengeneza vifungashio vya karatasi (Maswa), upanuzi wa Kiwanda cha Maziwa Meatu, kiwanda cha kutengeneza sabuni za maji, mche na unga Itilima, kiwanda cha kutengeneza tomato sauce na chili sauce (Busega) kiwanda cha kusaga nafaka  na kufungasha unga pamoja na unga lishe (Bariadi Mjini) na kiwanda cha kutengeneza bidhaa za Ngozi (Halmashauri ya Wilaya Bariadi) lengo likiwa ni wadau wa Taasisi za fedha na watalaam kwa pamoja kupitia maandiko hayo kujiandaa na utekelezaji.


Upanuzi wa Kiwanda cha Chaki ni agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt.John Pombe Magufuli alilolitoa kwa Uongozi wa Wilaya ya Maswa baada ya kutembelea kiwanda hicho wakati wa ziara yake mwezi Januari wilayani Maswa Mkoani Simiyu, ambapo aliagiza uongozi huo kukopa fedha kwa ajili kupanua kiwanda hicho ili kuongeza uzalishaji.
Kaimu Meneja wa Mipango na Uwekezaji wa NSSF  Bibi. Radhia Tambwe (wa pili kushoto) katika akizungumza na waandishi wa Habari mara baada ya kikao cha wadau wa uwekezaji Mkoani Simiyu kilichofanyika Kata ya Lamadi wilayani Busega.
Mkoa wa Simiyu Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka (kulia)akifungua kikao cha wadau wa Uwekezaji Mkoani humo kilchofanyika Kata ya Lamadi Wilayani Busega, (kushoto) Katibu Tawala Mkoa, Ndg Jumanne Sagini.
Viongozi na wadau mbalimbali wa uwekezaji Mkoani Simiyu wakifuatilia maandiko ya miradi ya uanzishwaji wa viwanda ikiwasilishwa katika kikao cha wadau wa uwekezaji kilichofanyika Kata ya Lamadi Wilayani Busega.
Mkurugenzi wa Benki ya Azania Ndg.Charles Jackson Itembe akizungumza na waandishi wa Habari (hawapo pichani) mara baada ya kikao cha wadau wa uwekezaji Mkoani Simiyu kilichofanyika Kata ya Lamadi wilayani Busega.
Mtaalam Mbobezi wa Viwanda, Ndg. Ndaki Munyeti akizungumza na waandishi wa Habari (hawapo pichani) mara baada ya kikao cha wadau wa uwekezaji Mkoani Simiyu kilichofanyika Kata ya Lamadi wilayani Busega.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!