Thursday, August 6, 2020

HALMASHAURI ZITUMIE ELIMU INAYOPATIKANA NANENANE KUWASAIDIA WAKULIMA VIJIJINI:NAIBU WAZIRI WAITARA


Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, Mhe. Mwita Waitara amezitaka Halmashauri zote nchini zinazoshiriki Maonesho ya Nanenane kuona namna ambayo watalaam wake watakavyoipeleka elimu waliyoipata katika maonesho hayo kwa wakulima na itakavyowasaidia wakulima, wafugaji na wavuvi hususani walioko vijijini kuleta tija katika uzalishaji.

Waiatara ameyasema hayo mara baada ya kutembelea baadhi ya mabanda ya maonesho na sehemu ya vipando vya mazao katika Viwanja vya Nyakabindi wilayani Bariadi Mkoani Simiyu ambako maonesho haya yanafanyika kitaifa mwaka 2020. 

Amesema halmashauri zinapaswa kuwatumia wataalam wa kilimo, mifugo na uvuvi kuhakikisha kuwa wanatumia elimu waliyoapata katika maonesho hayokuwafikia wakulima, wafugaji na wavuvi.

"Katika maonesho haya siku zote huwa kunakuwa na vitu vizuri tunavyoviona changamoto ipo kwenye kuyapeleka haya yaliyopo kwenye viwanja kwenda kule kwa wananchi," alisema Waitara.

Aidha, Mhe. Waitara ameupongeza mkoa wa Simiyu kwa kuwa kinara wa viwanda vidogo vidogo pamoja na viwanda vya kimkakati kikiwemo kiwanda cha chaki na kiwanda cha vifungashio wilayani Maswa. 

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Kiilimo, Mhe. Hussein Bashe amesema vijana wengi wanakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa ardhi huku akitoa rai kwa Ofisi ya Rais TAMISEMI kusisitiza Halmashauri kutenga maeneo kwa ajili ya shughuli za vijana.

 Naye Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bi. Miriam Mmbaga ameahidi kuwa mkoa huo uko tayari kutoa maeneo kwa ajili ya shughuli za vijana huku akisisitiza kuwa Simiyu itakuwa mkoa wa mfano okatika utekelezaji wa agizo hilo.

MWISHO

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, Mhe. Mwita Waitara(wa nne kulia) akizungumza na baadhi ya viongozi wakati alipokuwa akitembelea vipando vya mazao vya Halmashauri mbalimbali Agosti 04, 2020 katika maonesho ya Nanenane Kitaifa mwaka 2020 viwanja vya Nyakabindi wilayani Bariadi Simiyu. 



0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!