Tuesday, April 12, 2016

ASKARI POLISI WANAOKIUKA MAADILI YA JESHI WAWAJIBISHWE




Viongozi wa jeshi la Polisi Mkoa wa Simiyu wameaswa kuwawajibisha askari polisi watakaokiuka maadili ya kazi yao ikiwemo kutoa siri za jeshi la polisi kwa wahalifu.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony John Mtaka alipozungumza na Viongozi na Askari wa Jeshi la Polisi Mkoani Simiyu jana,  katika Ukumbi wa Shule ya Sekondari Bariadi Mjini Bariadi, katika kikao cha kujitambulisha na kutoa maelekezo ya Serikali kwa Jeshi la polisi.

Mtaka amesema viongozi hao wasisite kuwawajibisha askari watakaoonekana kuvujisha siri za jeshi hilo kwa kuwa kufanya hivyo kunalifedhehesha Jeshi la Polisi.

“Hatuwezi kukukubali kudhalilisha taaluma ya jeshi la polisi, hivi askari anayetoa siri za jeshi OCD unamwangalia wa nini, hii ni fedheha. Jeshi la Polisi linaonekana la ovyo kwa sababu ya askari wachache wasiotaka kutii  na kufuata maadili; raia anashindwa kutoa taarifa katika chombo cha dola kwa sababu anaogopa chombo cha dola kitamuuza, aibu hii haivumiliki wachukulieni hatua” alisema Mtaka.

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa  amewataka viongozi wa Jeshi la Polisi kufanya kazi kwa bidii na kusimamia haki ili askari watekeleze majukumu yao  sawa sawa.

Pamoja na kuwaasa Mtaka alitoa pongezi kwa jeshi la polisi kwa kazi nzuri inayoendelea kufanyika katika maeneo tofauti ya mkoa wa Simiyu ikiwa ni pamoja na kufanikiwa kuwakamata majangili waliotungua helikopta wilayani Meatu ,kufanya oparesheni za kuteketeza mashamba ya bangi na kazi nyingine za ulinzi na usalama wa raia na mali zao.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Simiyu, ASP. Onesmo Lyanga, alisema hatasita kuwachukulia hatua viongozi  na askari wa jeshi la polisi wababaishaji, hivyo akawataka wafanye kazi zao kwa bidii.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mh. Anthony J. Mtaka (wa pili Kushoto) akizungumza na viongozi na Askari wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Simiyu (hawapo pichani) jana mjini Bariadi, kulia kwake (wa kwanza) ni Kamanda wa Polisi Mkoa. Onesmo Lyanga.




1 comment:

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!