Wednesday, February 23, 2022

Mhe. Kafulila Ampongeza Diaspora wa Kike ( Dkt. Ashley Lucas) toka Simiyu, Daktari aliyeamua kuwekeza nyumbani.


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. David Kafulila ametoa pongezi hizo mara baada ya kutembelea kituo cha afya cha Barikiwa kilichopo Wilayani Maswa, kituo ambacho kimejengwa na mwanadada Mtanzania, mzaliwa wa Maswa ambaye ni Daktari.Akitoa Pongezi hizo Mhe. Kafulila amefurahishwa sana, mara baada ya kuona baadhi vijana wa kitanzania ambao ni wazalendo na wanaokumbuka kwao,kwani vijana wengi mara wapatapo fursa za kuenda nchi za nje huzamia na kutokukumbuka kabisa kirudi nyumbani.  “ Nikupongeze sana Dkt. Ashley kwa kukumbuka kurudi nyumbani na si kurudi tu bali na kuwekeza nyumbani na hasa kwa ndoto kubwa ulizonazo kuelekea Maswa”.Amesema Kafulila.
 
Akielezea Maswa ijayo Mhe. Kafulila amesema “Kipindi kifupi kijacho,Maswa, haitakuwa Maswa ya sasa, ujenzi wa reli ya SGR, utaleta fursa nyingi sana za uwekezaji, kwani majengo yanayotumika sasa kama ofisi kwa ajili ya ujenzi, baada ya ujenzi kukamilika ofisi hizo zitatumika kama chuo cha kilimo na mifugo na hivyo kuzalisha ajira na kuongeza shughuli za kiuchumi. Aidha Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Mama Samia Suluhu Hassan ina mpango wa kufungua (Logistic Hub) pamoja na dry Port/ Bandari kavu Maswa,  hivyo bila shaka unaona jinsi Maswa itakavyokuwa na shughuli nyingi na za kutosha. Hivyo wakati unaendelea na uwekezaji wako wa ujenzi wa hospitali ya Barikiwa ni vyema ukafikiria pia ujenzi wa chuo cha afya Barikiwa, kwani Mkoa wa Simiyu una changamoto kubwa sana ya ukosefu wa vyuo vya afya na utalii”. Amesema Kafulila.
 
“Kwa kawaida uwepo wa hospital huenda sambamba na uwepo wa chuo cha afya kwani hii huwezesha wanafunzi wa chuo cha afya kufanya elimu ya vitendo hapohapo hospitalini. Mfano mzuri ni hospitali ya Bugando Mwanza, Muhimbili- Dsm,Hubert Kairuki-Dsm na kadhalika hospitali zote hizo zina vyuo vya afya eneo katika eneo la hospital husika”.Amesisitiza Kafulila
 
Dkt Ashley Lucas,ni mke na mama wa watoto watatu, mzaliwa wa Maswa ambaye amepata elimu yake ya msingi katika shule ya msingi Binza,Maswa, elimu ya sekondari shule ya sekondari Mwamapalala ambapo amesoma kidato cha kwanza na baadae akaenda Kampala Uganda na kujiunga na shule ya sekondari Kampala, ambapo alipata elimu ya kidato cha pili hadi cha sita kisha chuo cha habari, Kampala (UMCAT) na baadae kupata wafadhili na kwenda nchini Marekani ambapo alikaa kwa kipindi cha miaka mitano huku akisoma na kutunukiwa digrii ya udaktari wa Kinywa na Meno ( Dental Surgery). Baada ya kumaliza masomo yake Dkt. Ashley aliamua kurejea nyumbani  Tanzania huku akiwa na lengo la kuwasaidia Watanzania wenzake na hasa wakazi wa Maswa, na hivyo kuwiwa kutumia elimu yake katika kutoa huduma za afya za kinywa na zinginezo.
 
“Hii Zahatani inaitwa Barikiwa,lakini baada ya wiki mbili hivi itapanda daraja na kuwa hospitali ya Barikiwa”. Ameeleza Dkt Ashley.
 
Zahanati hiyo ipo kwenye eneo lenye ukubwa wa hekari saba. Akielezea ndoto zake Mwana dada huyo Dkt.Ashley ameeleza kuwa “lengo langu ni  Kufanya kazi kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na taratibu za Wizara ya afya. Ninataka kujenga hospital ambayo itatoa huduma kiasi cha kwamba Wagonjwa toka Maswa au hata mkoa mzima wa Simiyu  hawatahitaji tena kwenda Bugango kwa ajili ya matibabu. Lengo langu kubwa ni kuwasaiida wakazi wa Maswa na Simiyu katika viwango vya huduma ya afya vya hali ya juu.

Vifaa tiba kwa ajilii ya wagonjwa wote hii ikiwa ni pamoja na huduma ya afya kwa mama na motto vyote vipo tayari, duka la dawa la nje, maabara,chumba cha upasuaji na chumba cha kujifungulia vyote vipo katika hatua za mwisho mwisho na hivyo vitakuwa tayari katika kipindi cha wiki mbili zijazo” Amesema Ashley.
 
Akizungumzia changamoto za mradi huu Dkt. Ashley ametaja janga la UVIKO-19, limesababisha madaktari kutoka nje ambao mara kwa mara wamekuwa wakija kujitolea kushindwa kuja, aidha alifanikiwa kupata msaada wa kontena mbili za vifaa ambalo nalo limekwama kwa sababu ya changamoto hiyo.
 
Pamoja na huduma ya kujenga majengo ambayo yatatumika kutoa huduma za kiafya, Dkt.Ashley, anatarajia kujenga nyumba za madaktari na wafanyakazi ambazo zitawezesha kukaa karibu na hospitali na hivyo kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora na salama za afya kwa masaa ishirini na nne na siku saba kwa wiki.Mwisho.








Tuesday, February 22, 2022

Serikali kukifufua Kiwanda Cha Kuchambua Pamba cha Sola Wilayani Maswa

MKUU  wa Mkoa Simiyu, David Kafulila ametaka kujua hatua zilizochukuliwa na Jeshi la Polisi dhidi ya Askari,Nuru Mtafya anaetuhumiwa kumpa ujauzito Mwanafunzi anayejulikana kwa jina la Neema Mabula wa shule ya Sekondari iliyopo wilayani Maswa mkoani humo.

Uamuzi huo umefikiwa na RC Kafulila mara baada ya mzazi wa mtoto huyo Mabula Masanja Manyanda mkazi wa kijiji cha Njiapanda kulalamika mbele ya Mkuu huyo wa Mkoa kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika jana na wananchi kutoa malalamiko yao.

Akitoa malalamiko yake amesema baada ya askari huyo ambaye alikuwa ni Askari wa Usalama Barabarani katika kituo cha polisi Malampaka kumpatia ujauzito binti yake alihamishwa na kupelekwa kituo cha polisi Maswa.

Aliendelea kueleza kuwa aliendelea kufuatia suala hilo kwa ukaribu hadi kwa Kamanda wa polisi wa mkoa wa Simiyu lakini amekuwa akipigwa danadana.

Akijibu malalamiko hayo,Rc Kafulila pamoja na kumpatia pole Mzazi huyo alimwagiza Kamanda wa Polisi mkoa wa Simiyu ACP.B.Z. Chatanda, kupata taarifa ya hatua zilizochukuliwa dhidi ya askari huyo katika kikao cha kamati ya ulinzi na usalama kitakachofanyika juma lijalo huku akisisitiza hakuna mtu aliye juu ya sheria.




" Pole sana mzazi. Naagiza RPC suala hili ulilete kwenye kikao cha Kamati ya Usalama wiki ijayo ili nijue kama kweli mmefanyia kazi kikamilifu kwani hakuna aliyejuu ya sheria haijalishi ni Polisi, Mwalimu au Hakimu na hata nikiwa mimi RC"alisema.Mwisho

Monday, February 21, 2022

Serikali Kukifufua Kiwanda Cha Kuchambua Pamba Cha Sola Wilayani Maswa

SERIKALI ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu imepanga kufufua viwanda viwili vya kuchambua pamba na kukamua mafuta ya pamba musimu huu  wa ununuzi wa zao la pamba wa mwaka 2022/2023.

Miongoni mwa viwanda vitakavyofufuliwa ni pamoja na Kiwanda cha Kuchambua Pamba cha Sola(Maarufu kwa jina la Sola Ginnery) kilichoko  mjini Maswa pamoja na kiwanda cha Lugulu  kilichoko wilaya ya Itilima.

Hayo yameelezwa na Mkuu wa mkoa wa Simiyu,David Kafulila mara baada ya kukitembelea kiwanda hicho ambacho kimeacha uzalishaji miaka mingi iliyopita kikiwa chini ya Chama cha Ushirika Cha Mkoa wa Shinyanga(SHIRECU) lakini kwa sasa kipo chini ya Chama Cha Ushirika cha  Mkoa wa Simiyu(SIMCU).

Amesema kuwa baada ya mkoa huo kufanya vizuri katika uzalishaji wa zao la pamba ndiyo maana serikali imeamua kutoa fedha kwa ajili ya kuvifufua viwanda hivyo ili shughuli za kuchakata pamba na kukamua mafuta viweze kufanya kazi mwaka huu.

Mkuu huyo wa mkoa amewataka viongozi wa SIMCU kuona umuhimu wa kutenga fedha kwa ajili ya kukarabati maghala ya kuhifadhia pamba na marobota ya pamba katika kiwanda hicho.

Awali Afisa Ushirika wa wilaya ya Maswa,Cosmas Budodi akisoma taarifa ya kiwanda hicho kwa niaba ya Uongozi wa SIMCU pamoja na kuipongeza serikali kwa hatua yake hiyo ya kukifufua kiwanda hicho hivyo wameomba pia serikali kusaidia kutatua changamoto ya deni kubwa la umeme na maji katika kiwanda hicho sambamba na kuwaondoa wananchi waliovamia eneo la kiwanda na kufanya shughuli mbalimbali za kibinadamu. Mwisho.


ITUNZENI MITARO- RC KAFULILA

MKUU wa Mkoa wa Simiyu,David Kafulila amewataka wananchi wa Mji wa Maswa mkoani humo kuitunza Mitaro ya maji ya mvua inayojengwa kwenye baadhi ya barabara za mitaa ya mji huo.

Sambamba na kuitunza amewataka kuifanyia usafi wa mara kwa mara na kutotupa takataka ndani ya mitaro hiyo ili iweze kuwasaidia kusafirisha maji ambayo awali yalikuwa wakiingia kwenye nyumba zao hasa nyakati za mvua.

Mkuu huyo wa mkoa amesema haya mara baada ya kutembelea ujenzi wa mitaro yenye urefu wa kilomita 5.5 inayojengwa kwenye mji huo chini ya Wakala wa Barabara za Vijijini na Mjini(TARURA).

Kafulila ambaye ameridhishwa na ujenzi huo unaoendelea amewataka Wakandarasi wote waliopewa kazi hiyo kukamilisha kwa wakati kama mikataba yao waliyosaini na TARURA, Simiyu kwani Serikali imetoa fedha hizo kupitia tozo za mafuta na mfuko wa barabara.

Naye Meneja wa Tarura wilaya ya Maswa,Mhandisi David Msechu amesema kuwa wanatekeleza miradi mitano ya ujenzi wa mitaro hiyo yenye thamani ya Sh 532,936,640.

Amesema mradi huo unatekelezwa  kupitia kampuni mbalimbali ambazo ni pamoja na Kampuni  ya MMETO CONSTRUCTION CO LTD ya Dar Es Salaam kwa gharama ya Sh Milioni 100,Kampuni ya FRESAM CONSTRUCTION  CO LTD ya Mwanza kwa gharama ya Sh Milionib111.2 na Kampuni ya ASSA GENERAL SUPPLIERS AND CONSTRUCTION  CO LTD ya Bunda,Mara kwa gharama ya Sh Milioni 69.

Kampuni nyingine ni MORAJ WOMEN GROUP ya Shinyanga kwa gharama ya Sh Milioni 200 na Kampuni ya WAMAMA KAZI ya Tukuyu,Mbeya kwa gharama ya Sh Milioni 52.

Mhandisi Msechu amesema katika kutekeleza mradi huo, mradi huo unakabiliwa na changamoto ya kuwepo kwa miundo mbinu ya maji iliyokatisha au kupita sambamba na barabara ambayo imesimikwa kina kifupi kukatwa na kusababisha baadhi ya wananchi kukosa huduma ya maji ila wamekuwa wakishirikiana na Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Mjini Maswa (Mauwasa)kuirejesha kwa wakati ili wananchi wapate huduma ya maji.Mwisho








Thursday, February 17, 2022

Tumieni Wakandarasi na Watoa Huduma Kutoka Simiyu- RC Kafulilla

Mhe. Kafulila ameyasema hayo hivi karibuni akiwa ameambatana na kamati ya Ulinzi na usalama ya Mkoa pamoja na mkuu wa Wilaya ya Bariadi, wakati wa ziara ya kutembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa Chuo cha VETA mkoani Simiyu. Mhe. Kafulila ametoa maelekezo hayo mara badaa ya kupokea taarifa kutoka kwa  Meneja mradi ambaye pia ni Mkuu wa chuo cha Maendeleo ya jamii Buhnamala-Bariadi, Bw.Bazil Ngoloka, kuwa matofali ya ujenzi wa mradi huo yanasambazwa na mtoa huduma kutoka Mwanza anayejulikana kama Arm Strong Company Limited.

Akizungumzia mradi huo Bw.Ngoloka ameleza, mradi wa ujenzi wa Chuo cha VETA Mkoani Simiyu ulianza tarehe 26.01.2022 kwa kazi ya awali na kazi rasmi ilianza 07/02/2022 kazi ambayo inatarajiwa kukamilika mara ifikapo 30/6/2022. Mradi huu unasimamiwa na chuo cha ufundi Arusha.

Ujenzi wa chuo cha VETA Simiyu,utagharimu kiasi cha Tsh.5,150,731,187.10,ambazo zitatumika kujenja, mabweni manne , mawili yakiwa ya kike na mawili ya kiume, majengo ya idara tisa,majengo ya utawala na huduma zinginezo 7 pamoja  na nyumba za waalimu 4. “Kwa ujumla hatua ya utekelezaji hadi sasa zimefikia hatua ya uchimbaji wa Msingi majengo kwenye kila lot na umwagaji zege kwenye baadhi ya majengo. Kiasi cha fedha zilizotumika hadi sasa  ni Tsh. 7.89 ml.’’Amesema Ngoloka.

Pamoja na mafaniko hayo Bw. Ngoloka, ametaja kukabialina na changamoto za ubovu wa barabara hasa kipindi hiki cha mvua na ongezeko la  bei za vifaa vya ujenzi kama nondo na hivyo kupelela kurudia mchakato wa manunuzi ili kupata bei halisi ya soko. 

Aidha, Mhe Kafulila aliwataka wajumbe wa kamati ya Ulinzi na usalama pamoja na mkuu wa Wilaya ya Bariadi kutoa maoni yao kuhusiana na mradi wa ujenzi huo, ambapo  Mkuu wa wilaya ya Bariadi Mhe.Lupakisyo Kapange alisisitiza umuhimu wa kutumia vijana wa Bariadi kufanya kazi za ujenzi katika mradi huo,badala ya kutumia vijana kutoka maeneo mengine na hasa mje ya mkoa wa Simiyu,labda iwe  tu kwa fani ambazo zinahitaji utaalamu maaluum,kwani mradi huo unategemewa kuongeza ajira kwa wakazi wa Baridi.

Aidha Mhe.Kapange aliahidi kutoa ushirikiano wa hali na mali  kwa Meneja wa mradi huo na kuhakikisha anapata rasilimali watu katika kamati mbalimbali za ujenzi, wanakamati ambao watatokana na uwezo wao kama ilivyoelekezwa na mkuu wa Mkoa.

Wajumbe wengine wa Kamati ya Ulinzi na Usalama walisistiza, suala la  Usalama wa Vifaa vya ujenzi katika eneo la ujenzi na mara baada ya kukamilika kwa ujenzi huo.Aidha wajumbe walikumbusha suala laupatikanaji wa Umeme ili kazi ziweze kufanyika kwa masaa 24 (usiku na Mchana) pamoja na upatikanaji wa maji safi na salama.

Ili kuhakikisha kuwa ujenzi huo unafanyika kwa viwango na kwa wakati Mkuu wa Mkoa Simiyu Mhe. David Kafulila alitoa maelekezo kwa Mamlaka ya Bonde kuja kufanya uchunguzi ili kujua maji yanapatikana wapi katika eneo husika na hatimaye Meneja mradi kuhakikisha kuwa wanachimba kisima,ambacho kitatumika wakati wa mradi wa ujenzi na baada ya mradi. Vilevile Mkuu wa Mkoa aliwaagiza TANESCO kuhakikisha kuwa kufikia ijumaa umeme uwe unapatikana katika eneo husika.

Aidha Mhe. Kafulila aliagiza kamati za ujenzi ziangaliwe upya na Mkuu wa Wilaya  pamoja na Mkurugenzi wasaidie upatikanaji wa rasilimali watu ambao watafanya kazi katika kamati mbaliambali. Mhe. Kafulila alisistiza kuwa upatikanaji wa rasilimali watu hao uwe kulingana na uwezo na si kwa majina.

Katika hatua hiyo hiyo Mhe. Kafulila alitoa maelekezo ya kuwasimamisha kazi  watoa huduma wote wanaotoka nje ya mkoa wa Simyu, labda iwe kwa maelekezo maalum au kwa watoa huduma wanatoa huduma za moja kwa moja kutoka kiwandani kama vile kiwanda cha nondo au Sementi, kwani kwa kufanya hivyo kutaokoa muda, kutapunguza gharama, kutaongeza mauzo, kupato na ajira kwa wananchi wa Simiyu.Mwisho.























 

 

 

Wednesday, February 16, 2022

WACHIMBAJI, UHAI WENU NI MUHIMU KULIKO MADINI, FUATENI TARATIBU -RC KAFULILA,

Mhe.Kafulila ameyasema hayo leo, wakati alipotembela mgodi wa EMJ, Dutwa wilayani Bariadi. Mhe kafulila amefanya ziara hiyo ili kukutana na kutatua kero za wachimbaji. Wakizungumzia kero zao, Wachimbaji hao wametaja kero hizo kuwa ni pamoja na kukatazwa kuchimba kwenye baadhi ya maeneo, uwepo wa mwekezaji mchina ambaye ameanza kujenga uzio na hivyo kuhofia uhuru wao wa kuchimba madini kwenye eneo hilo na Maduara yaliyotelekezwa kurudishwa kwa mwenye leseni, huku wao wakitafuta nguvu zaidi za kuendelea na uchimbaji.

Akijibu hoja hizo Mhe. Kafulila alimtaka Mwakilishi toka ofisi ya Madini bwana Lucas Mwakulo, kujibu kero hizo na kueleza sheria inasemaje kuhusu maduara yaliyotelekezwa. Bw.Mwaluko  alieleza kuwa ni kweli kwamba kuna eneo ambalo ofisi ya Madini imekataza uchimbaji wa madini na hiyo ni kwa sababu za kiusalama. Suala la kiusalama lipo juu ya kila kitu. Hairuhusiwi mchimbaji yeyote kuchimba katika eneo ambalo ni hatarishi.Aidha Serikali imetoa maelekezo kuwa mchimbaji anaweza kupewa kibali cha siku 30 ili apumzike na kukusanya nguvu, siku hizo zikipita shimo linarudishwa kwa mwenye leseni.

Nae katibu wa wachimbaji Bw. Ramadhani Faida, alieleza kuwa ni kweli kwamba kuna duara 5 zilizosimamishwa uchimbaji na duara hizo ni 286A, 203A,190,101B  na duara namba 237B. Akizungumzia sababu ya kufungwa mashimo hayo mkaguzi Mkuu (chief Inspector) Bw. Charles Lyaganga alizitaja sababu hizo kuwa ni Changamoto ya maji na ajali za gesi.“Sisi ndio tunatoa mapendekezo ofisi ya Madini kuwa shimo gani lifungwe baada ya ukaguzi. Tarehe 16/01/2022 tulitangaza maduara 11 kuwa hatarishi”. Amesema Lyaganga.

Mhe. Kafulila ameitaka ofisi ya madini kwa kushirikiana na Mkaguzi ,kubainisha Maduara yaliyotekelezwa kama yapo, na endapo yapo basi mabango yakawekwe kwenye maduara hayo mara moja na baada ya siku 30 yarejeshwe kwa mwenye leseni.  “Yale maeneo ambayo ni hatarishi,kimsingi kwenye hayo maeneo uchimbaji usiendelee, usimamishwe,kwani uhai wenu ni muhimu kuliko madini.Hayo maeneo msiende kama mnaenda basi muende kwa kibali cha afisa madini.Mpate  ridhaa ya afisa madini”. Ameagiza Mhe. Kafulila. 

Aidha Mhe. Kafulila ametoa ruhusa kwa wachimbaji kuendelea na uchimbaji madini kwenye maeneo yaliyo salama ili mradi wazingatie, kanuni, sheria na taratibu.  

Mkuu wa Mkoa amemwelekeza inspekta Lyaganga kufanya kazi kwa umakini na kwa ukaribu na ofisi ya madini. “Wachimbaji fuateni taratibu, sio mnaacha maduara yenu bila kufuata taratibu halafu baadae mnavizia fidia. Kwa maeneo ambayo yapo  nje ya maeneo hatarishi endeleeni na uchimbaji ”.Amesema Kafulila.

Akizungumzia suala la uwepo wa Wachina, Mhe. Kafulila alieleza kuwa uwepo wa Wachina  hao ni makubaliano kati ya mwenye leseni na  Wachina, ili waweze kufanya utafiti na kuona ni kwa jinsi gani na kwa kutumia teknologia ya juu wanaweza kupata madini zaidi, kwani wachina hao ni wazoefu na wamefanya kazi katika migodi mingine kama vile Geita.





j













Aidha ujenzi wa uzio kwenye eneo hilo ni kwa sababu za kiusalama, kama ilivyoelezwa na mwakilishi kutoka ofisi ya madini ambaye alieleza kuwa maelekezo yalishatolewa kuwa kwenye kila mgodi  ni lazima kuwe na uzio ili kuepuka uvamizi na wizi mgodini (Manyani). Mhe.Kafulila alisisitiza kuwa, pamoja na uwepo wa uzio huo wachimbaji, wataruhusiwa kuendelea na uchimbaji madini.Mwisho.

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!