Monday, February 21, 2022

ITUNZENI MITARO- RC KAFULILA

MKUU wa Mkoa wa Simiyu,David Kafulila amewataka wananchi wa Mji wa Maswa mkoani humo kuitunza Mitaro ya maji ya mvua inayojengwa kwenye baadhi ya barabara za mitaa ya mji huo.

Sambamba na kuitunza amewataka kuifanyia usafi wa mara kwa mara na kutotupa takataka ndani ya mitaro hiyo ili iweze kuwasaidia kusafirisha maji ambayo awali yalikuwa wakiingia kwenye nyumba zao hasa nyakati za mvua.

Mkuu huyo wa mkoa amesema haya mara baada ya kutembelea ujenzi wa mitaro yenye urefu wa kilomita 5.5 inayojengwa kwenye mji huo chini ya Wakala wa Barabara za Vijijini na Mjini(TARURA).

Kafulila ambaye ameridhishwa na ujenzi huo unaoendelea amewataka Wakandarasi wote waliopewa kazi hiyo kukamilisha kwa wakati kama mikataba yao waliyosaini na TARURA, Simiyu kwani Serikali imetoa fedha hizo kupitia tozo za mafuta na mfuko wa barabara.

Naye Meneja wa Tarura wilaya ya Maswa,Mhandisi David Msechu amesema kuwa wanatekeleza miradi mitano ya ujenzi wa mitaro hiyo yenye thamani ya Sh 532,936,640.

Amesema mradi huo unatekelezwa  kupitia kampuni mbalimbali ambazo ni pamoja na Kampuni  ya MMETO CONSTRUCTION CO LTD ya Dar Es Salaam kwa gharama ya Sh Milioni 100,Kampuni ya FRESAM CONSTRUCTION  CO LTD ya Mwanza kwa gharama ya Sh Milionib111.2 na Kampuni ya ASSA GENERAL SUPPLIERS AND CONSTRUCTION  CO LTD ya Bunda,Mara kwa gharama ya Sh Milioni 69.

Kampuni nyingine ni MORAJ WOMEN GROUP ya Shinyanga kwa gharama ya Sh Milioni 200 na Kampuni ya WAMAMA KAZI ya Tukuyu,Mbeya kwa gharama ya Sh Milioni 52.

Mhandisi Msechu amesema katika kutekeleza mradi huo, mradi huo unakabiliwa na changamoto ya kuwepo kwa miundo mbinu ya maji iliyokatisha au kupita sambamba na barabara ambayo imesimikwa kina kifupi kukatwa na kusababisha baadhi ya wananchi kukosa huduma ya maji ila wamekuwa wakishirikiana na Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Mjini Maswa (Mauwasa)kuirejesha kwa wakati ili wananchi wapate huduma ya maji.Mwisho








0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!