Wednesday, May 31, 2017

WACHUNGAJI ,WAGANGA WA JADI WACHEZA MPIRA KULENGA KUPINGA MAUAJI YA WENYE UALBINO

Mkoa wa Simiyu umeweka historia ya Mchezo wa Mpira wa Miguu baina ya wachungaji na waganga wa jadi ikiwa ni makubaliano ya kutoa ujumbe wa kupinga mauaji ya watu wenye Ualbino na vikongwe kwa kupiga maarufuku Ramli Chonganishi ambazo zimekuwa zikichangia kwa kiasi kikubwa mauaji hayo.

Mchezo huo kati ya wachungaji na waganga wa jadi umefanyika  siku moja kabla ya kufanyika burudani kubwa ya utamaduni wa asili almaarufu Mbina ambayo hufanyika kila mwaka Mei 31,baada ya wakulima kumaliza msimu wa kilimo .

Pande zote mbili kwa  pamoja zilikubaliana  kuwa utaratibu wa kufanya vikao na michezo utakuwa endelevu na utafanyika kila mwaka kwa kuzunguka katika wilaya zote ili kuhakikisha mauji ya watu wenye ualbino na vikongwe yanakomeshwa kabisa.

 Askofu wa K.K.K.T Dayosisi ya Kusini Mashariki ya Ziwa Victoria, Dkt.Emmanuel Makala amesema Kanisa liko tayari kukemea kwa wazi mauaji ya watu wenye ualbino na linaunga mkono juhudi za Serikali za kulinda amani na kuleta maendeleo kwa wananchi.

Naye Mtemi Charles Balele Doto ambaye ni Katibu wa Umoja wa Watemi Kabila la Wasukuma amesema waganga wa jadi kazi yao ni kutoa huduma za tiba asili kwa watu na siyo kufanya ramli chonganishi zinazopelekea mauji ya watu wenye ualbino, akawataka wanaofanya hivyo waache mara moja kwa kuwa ni wababaishaji na wanadhallisha ya huduma ya tiba asili.

Akizungumza mara baada ya mchezo huo kukamilika,Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe.Anthony Mtaka amewapongeza kwa uamuzi huo ambao unatoa Taswira mpya kwa mkoa wa Simiyu  wa kuondokana na dhana iliyokuwepo ya mauaji na kuwa mkoa wa kimaendeleo na kuagiza michezo mbalimbali kufanyika kila mwezi ili kuendeleza vipaji vya mbalimbali vya wanamichezo.

Aidha, amesema Mkoa huo una agenda ya “Wilaya Moja, Bidhaa Moja, Kiwanda Kimoja ama ununue au ukodishe Simiyu, Watanzania Tupende vya kwetu”hivyo akawataka wananchi kuchangamkia fursa hizo kwa maendeleo yao na kuachana na imani potofu kuwa Viungo vya Mtu mwenye ualbino vitawapa utajiri.

“Simiyu tunajenga viwanda utajiri wako wewe usiue albino utajiri wako lima pamba uuze kwenye kiwanda cha nguo, jiandae kuwa wakala, soma vizuri uwe mfanyakazi, jiandae kuzalisha malighafi ya Viwanda vya Rais wetu Mhe.Dkt. John Pombe Magufuli”  alisema.

“Tarehe 09 Mwezi Juni tunapokea hundi ya shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa kiwanda cha chaki Maswa, Tarehe 12 Juni tunaanza upembuzi yakinifu wa viwanda vyetu viwili; upanuzi wa kiwanda cha maziwa Meatu na kiwanda cha kusindika nyanya na pilipili ili tutengeneze tomato sauce na chili sauce. Bariadi tutajenga kiwanda cha bidhaa za afya zitokanazo na pamba, Itilima tutajenga kiwanda cha kutengeneza sabuni zote hizi ni fursa” alisema

Mtaka ameongeza kuwa wazazi wote walio na watoto wenye ulemavu wa aina yoyote wasiwafiche wawatoe kwa Serikali imewatengenezea mazingira mazuri ikiwa ni pamoja na kulinda haki zao.

Wakati huo huo amewataka wananchi kuvitumia vituo vya kutolea huduma za Afya kwanza kila wanapohitaji matibabu badala ya kukimbilia kwa Waganga wa jadi hali inayopelekea wengi wao kuchelewa kupata  huduma wanapoteza maisha na kuingia katika ramli chonganishi kwa kuamini kuwa wamerogwa.

Katika Mtanange huo uliofanyika katika uwanja wa Halmashauri ya Mji Bariadi  Waganga wa kienyeji walikubali kichapo cha Magoli mawili kwa nunge(sifuri) kutoka kwa watumishi wa Mungu(Wachungaji).
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka (kulia)akimkabidhi Askofu wa K.K.K.T Dayosisi ya Kusini Mashariki ya Ziwa Victoria, Dkt.Emmanuel Makala vitabu vya Neno la Mungu vilivyotolewa na Kanisa Waadventista Wasababto (SDA) Bariadi.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka (kulia) akimkabidhi Askofu wa Kiongozi wa Waganga wa Kienyeji, Mayunga Kidoyayi vitabu vya Neno la Mungu vilivyotolewa na Kanisa Waadventista Wasababto (SDA) Bariadi.
Askofu wa K.K.K.T Dayosisi ya Kusini Mashariki ya Ziwa Victoria, Dkt.Emmanuel Makala akizungumza kabla ya kumkaribisha Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka azungumze na wananchi, wachungaji na waganga wa jadi.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka akizungumza na wananchi, wachungaji na waganga wa jadi mara baada ya mchezo wa mpira wa miguu kati ya wachungaji na waganga wa jadi kumalizika.
Baadhi ya Wachungaji wakijiandaa kuingia uwanjani kwa ajili ya mtanange dhidi ya waganga wa jadi kwa lengo la kupinga mauaji ya watu wenye ualbino, vikongwe na ramli chonganishi.
Baadhi ya wananchi wakishangilia ushindi wa kichapo cha magoli mawili cha wachungaji dhidi ya waganga wa jadi.




Waimbaji wa Kwaya ya Umoja kutoka K.K.K.T Bariadi wakiimba wimbo maalum wa kupinga mauaji ya watu wenye Ualbino kabla ya Mchezo wa mpira wa miguu kati ya wachungaji na waganga wa jadi kuanza.
Baadhi ya wananchi wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka alipozungumza na wananchi, wachungaji na waganga wa jadi mara baada ya mchezo wa mpira wa miguu kati ya wachungaji na waganga wa jadi kumalizika.
Wachezaji wa timu ya wachungaji(kulia) na waganga wa jadi (kushoto) wakiwa wamejipanga kabla ya kuanza mchezo ambao ulilenga kupinga mauaji ya watu wenye ualbino.

SIMIYU KUFANYA MAJARIBIO YA KUFUNDISHA KUPITIA MTANDAO

Mkoa wa Simiyu unatarajia kufanya majaribio ya kufundisha wanafunzi kwa kutumia mtandao kupitia programu itakayotengenezwa na watalaam wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe.Anthony Mtaka katika Maadhimisho ya Wiki ya Elimu Mkoani humo yaliyofanyika kimkoa mjini Mwanhuzi Wilayani Meatu, chini ya Kauli Mbiu “TUWEKEZE KATIKA ELIMU KWA USTAWI WA JAMII YENYE UTAALAMU WA SAYANSI NA VIWANDA KUELEKEA UCHUMI WA KATI TANZANIA”

“Tunataka tufanye majaribio,  tuanze kwa kuunganisha shule zetu za mjini wataalamu wetu wa ICT (TEHAMA) watengeneze programu,baadhi ya madarasa kama darasa la saba  tuanze kufundisha kwa kutumia mtandao” amesema.

 Wakizungumza kwa nyakati tofauti baadhi ya wanafunzi walioshiriki katika maadhimisho ya wiki ya elimu wamesema iwapo teknolojia hiyo itafanikiwa kutumika itawasaidia katika masomo yenye upungufu wa walimu hususani wa sayansi, ambapo wameiomba Serikali kuendelea kutatua changamoto ya upungufu wa vyumba vya madarasa na vifaa vya maabara ili kuwawezesha kujifunza vema masomo hayo kwa nadharia na vitendo.

Kwa upande wake Afisa Elimu wa Mkoa wa Simiyu, Julius Nestory amesema maadhimisho ya wiki ya Elimu yaliyoanza Mei 24 ni moja ya tathmini ya malengo yaliyowekwa Mei 2016 na miongoni mwa mafanikio ya malengo hayo ni ujenzi wa vyumba vya madarasa zaidi ya 180 chakula cha mchana kutolewa katika shule za kutwa lililotekelewa kwa asilimia 43.

Katika hatua nyingine Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe Anthony Mtaka amesema Serikali imepanga kupitia Watalaam hao wa TEHAMA pia kwa kutumia teknolojia nyepesi, itengenezwe programu itakayosaidia kutoa taarifa za uwepo wa watumishi mahala pa kazi.

Aidha ameongeza kuwa katika kipindi hiki ambacho Serikali Mkoani Simiyu imejipanga kufanya mapinduzi ya Viwanda, imedhamiria kuwatumia Watalaam wa TEHAMA kutengeneza mfumo wa taarifa na takwimu sahihi za kila sekta zikiwemo za kilimo, mifugo, elimu ili mtu akitaka taarifa yoyote ya Simiyu azipate kwa urahisi (awe nazo mkononi).

“Miaka minne ijayo hatutakuwa na Simiyu mnayoiona leo, kama kuna mtu anafikiri ni maneno atupe muda; tunataka tuwapunguzie Watanzania kufanya rejea nchi nyingine waje kwenye mkoa wetu. Tarehe 09/05/2017 Maswa wanapokea hundi ya shilingi Bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa kiwanda cha chaki Maswa, Meatu upembuzi yakinifu unaanza tarehe 12/06/2017 ujenzi wa kiwanda cha maziwa” amesema.

Wakati huo huo Mkuu huyo wa Mkoa amesema Serikali inalitafutia ufumbuzi wa kudumu suala la bei ya pamba ambalo limekuwa likiwakatisha tamaa wakulima kwa kuwa wafanyabiashara wananunua pamba kwa bei ya chini kwa kigezo cha kuwa bei katika soko la dunia iko chini.

Mtaka amesema Simiyu inaoongoza kwa kulima pamba lakini Halmashauri na wananchi hawanufaiki kwa kiwango kinacholingana na uzalishaji uliopo, hivyo watatafutwa watalaam ambao watachunguza bei ya pamba katika soko la dunia na akasisitiza kuwa mfanyabiashara yeyote atakayeona pamba haina faida kwake aache katika Msimu wa mwaka 2018 Halmashauri zitanunua.


Wiki ya Elimu huadhimishwa kila mwaka mwezi Mei ikiwa na lengo la kuwakutanisha wadau wa elimu, kuona shughuli mbalimali za elimu, kufanya tathmini ya mipango ya elimu ya mwaka uliopita na kuweka mipango ya mwaka mwingine.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka akimsikiliza Beatus John mwanafunzi wa darasa la saba katika Shule ya Msingi Mwanhuzi katika maonesho ya elimu yaliyoandaliwa wakati wa maadhimisho ya wiki ya elimu kimkoa wilayani Meatu.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka(wa nne kushoto) na viongozi mbalimbali wa mkoa na wilaya ya Meatu wakipokea maandamano ya wanafunzi wa shule za msingi na sekondari  za wilayani Meatu wakati wa maadhimisho ya wiki ya elimu kimkoa.
Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Kimali wilayani Meatu wakiwa bango lao wakati maandamano katika maadhimisho ya wiki ya elimu kimkoa iliyofanyika wilayani humo.
Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Msingi Mwanhuzi wilayani Meatu wakiwa katika maandamano na mabango yenye jumbe mbalimbali  wakati  wa maadhimisho ya wiki ya elimu kimkoa iliyofanyika wilayani humo.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka akizungumza na wadau wa elimu mkoani humo wakati maadhimisho ya wiki ya elimu kimkoa iliyofanyika Wilayani Meatu.

Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Jumanne Sagini akizungumza na wadau wa elimu mkoani humo wakati maadhimisho ya wiki ya elimu kimkoa iliyofanyika Wilayani Meatu.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka akimsikiliza Alex Silas mwanafunzi wa darasa la saba katika Shule ya Msingi Mshikamano katika maonesho ya elimu yaliyoandaliwa wakati wa maadhimisho ya wiki ya elimu kimkoa wilayani Meatu
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka na Katibu Tawala Mkoa Jumanne Sagini(kulia) na Mkuu wa Wilaya ya Bariadi na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Meatu Juma Mwibuli (kushoto) wakiteta jambo wakati wa maadhimisho ya wiki ya elimu kimkoa wilayani Meatu.

Katibu Tawala Mkoa Simiyu Jumanne Sagini akizungumza na wanafunzi wa shule ya Sekondari Meatu waliokuwa wakionesha kwa vitendo matumizi ya vifaa vya maabara, wakati wa maadhimisho ya wiki ya elimu kimkoa wilayani Meatu.

Monday, May 29, 2017

RAS SAGINI AWATAKA WAKURUGENZI KUANDAA MIPANGO MIKAKATI YA HALMASHAURI

Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg.Jumanne Sagini amewataka Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri Mkoani Humo kuandaa mipango mikakati katika Halmashauri zao.

Sagini ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo ya siku tatu ya uandaaji wa Mipango mikakati ya Mamlaka za Serikali za Mitaa Mkoani humo yanayofanyika Lamadi wilayani Busega, chini ya Mpango wa Maboresho ya Usimamizi wa Fedha za Umma katika Mamlaka za Serikali za Mitaa(PFMRP).

Amesema wakurugenzi wote wahakikishe wanatumia rasilimali zilizopo katika maeneo yao kuhakikisha kuwa wanakamilisha uandaaji wa mipango mikakati hiyo.

“ Niwaombe Wakurugenzi Watendaji kuepuka visingizio vya kutokuwa na fedha kutekeleza jambo hili na badala yake mjipange kwa kutumia rasilimali tulizonazo” amesema.
Aidha, amesema Mpango Mkakati ni muhimu kwa kila Halmashari kwa kuwa unasaidia Halmashauri kufikia malengo ya kuanzishwa kwake na kuboresha utoaji huduma za kiuchumi na kijamii kwa wananchi.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi, Ndg.Abdallah Malela  amesema mafunzo hayo yatawasaidia wao kama viongozi na watendaji wengine katika Halmashauri zao kutekeleza shughuli mbalimbali za maendeleo zikiwemo za uanzishwaji  na uendeshaji wa viwanda kimkakati.

Wakati huo huo pia Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri kuendelea kutenga maeneo ili kuwezesha utekelezaji wa Sera ya Ujenzi wa Uchumi wa Viwanda Mkoani humo.

Mafunzo ya uandaaji wa Mipango mikakati ya Mamlaka za Serikali za Mitaa (Halmashauri) Mkoani yamewahusisha Wakurugenzi, Wataalam wa Idara ya Kilimo, Fedha, Mipango na Maendeleo ya Jamii kutoka Halmashauri zote sita (06) za mkoa huo (Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi, Busega, Itilima, Maswa, Meatu na Halmashauri ya Mji Bariadi).

 
Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg.Jumanne Sagini (wa pili kulia) akizungumza na washiriki wa mafunzo ya uandaaji wa mipango mikakati ya Halmashauri mkoani humo yaliyofanyika Lamadi wilayani Busega
Washiriki wa mafunzo ya uandaaji wa mipango mikakati ya Halmashauri mkoani Simiyu wakimsikiliza Katibu Tawala Mkoa huo, Ndg.Jumanne Sagini katika ufunguzi wa mafunzo hayo wilayani Busega
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi, Ndg.Abdallah Malela akichangia jambo wakati wa mafunzo ya uandaaji wa mipango mikakati ya Halmashauri mkoani Simiyu yaliyofanyika Lamadi wilayani Busega
Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Mipango na Uratibu kutoka Sekretarieti ya Mkoa wa Simiyu, Ndg.Donatus Weginah (kushoto)akizungumza na washiriki wa mafunzo ya uandaaji wa mipango mikakati ya Halmashauri mkoani humo yaliyofanyika Lamadi wilayani Busega

Washiriki wa mafunzo ya uandaaji wa mipango mikakati ya Halmashauri mkoani Simiyu wakimsikiliza Katibu Tawala Mkoa huo, Ndg.Jumanne Sagini katika ufunguzi wa mafunzo hayo wilayani Busega

Friday, May 26, 2017

RC MTAKA : HUDUMA YA AFYA NGAZI YA JAMII ITUMIWE VIZURI KUOKOA MAISHA YA WANANCHI

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amesema iwapo Mpango wa Huduma ya Afya ngazi ya Jamii utatumika vizuri utasaidia kuokoa Afya na maisha ya wananchi wengi Mkoani humo.

Mtaka ameyasema hayo katika kikao kilicho wahusisha Viongozi ngazi ya Mkoa,Wilaya, watendaji wa Kata, Mitaa na Vijiji wa Halmashauri ya Wilaya Bariadi, Itilima na Mji wa Bariadi, ambacho kililenga kutoa elimu kuhusu utekelezaji wa mpango wa huduma ya Afya ngazi ya Jamii  mkoani humo.

Mtaka amesema mwamko wa kupata huduma za afya katika vituo vya kutolea huduma za afya kwa wananchi katika maeneo mengi mkoani humo  uko chini, hivyo mpango huu wa kutoa huduma ngazi ya kaya utasaidia kuhamasisha wananchi kutafuta huduma za afya katika vituo hivyo badala ya kutegemea tiba za kienyeji.

“Tukitumia huduma hii ya Afya Majumbani vizuri itasaidia sana, tukifika mahali ambapo jamii yetu itapata mwamko wa kupata matibabu katika vituo stahiki vya afya tutakua tumeokoa jamii yetu,  kwa sababu bado wapo wanaoamini kupata matibabu katika tiba za kienyeji; tungehitaji wananchi wetu huduma ya kwanza kwenye afya iwe vituo vyetu kutolea huduma za afya na siyo tiba mbadala” amesema Mtaka.

“........kwa sisi ambao tunatengeneza Mkoa wetu katika Uchumi, Uchumi ni Afya wananchi hawawezi kufanya kazi wakajenga uchumi kama hawatakuwa na afya njema” alisisitiza.

Aidha, Mtaka amewataka Watendaji wa Kata, Mitaa na Vijiji kufanya utambulisho wa kutosha wa wahudumu wa afya ya Msingi ngazi ya jamii watakaokuwa wakitoa huduma kwa wananchi katika maeneo yao ili wataalam hao wasije wakapata madhara yoyote wakati wakitekeleza majukumu yao.

Mkuu huyo wa Mkoa pia amewataka wananchi kuachana na taratibu za kimila zinazoathiri utendaji wa watumishi wa Umma ikiwemo kutumia mahakama za kimila (dagashida) na akawataka viongozi hao kuwasaidia wananchi kubadilika ili wahudumu wa afya ngazi ya Jamii watakaopelekwa katika maeneo yote ya mkoa huo watekeleze majukumu yao bila vikwazo vyovyote.

Wakati huo huo Mtaka ameomba Shirika lisilo la Kiserikali la AMREF lisaidie katika kuajiri wahudumu wa afya ngazi ya jamii walipewa mafunzo, ili wasaidie kutoa huduma na kupunguza changamoto ya upungufu wa watoa huduma wakati Serikali ikiendelea kushughulikia suala hilo.

Vile vile ametoa wito kwa wadau mbalimbali wa afya ikiwemo Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kushughulikia suala la upatikanaji wa vifaa ili watoa huduma ngazi ya jamii watakapowafikia wananchi waweze kutoa huduma stahiki kwa wakati.

 Kwa upande wake Afisa wa Mpango wa Huduma ya Afya ngazi ya Jamii kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt.Ama Kasangala amesema Wizara imetengeneza miongozo ya kuwafundisha wahudumu hao wanapokuwa kazini ili waimarike na kutoa huduma nzuri.

Naye Kaimu Mratibu wa Mpango wa Huduma ya Afya Ngazi ya Jamii, Dkt. Bahame Ntelemko amesema mpango umelenga kuwatumia wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii kusaidia kuboresha huduma za afya hususani katika huduma za mama wajawazito na uzazi kwa ujumla.

Dkt. Ntelemko amesema kwa mwaka 2016 wanawake takribani 45 walipoteza maisha kutokana na masuala ya uzazi ambapo vifo vingi vinatokana na ukosefu wa elimu ikiwemo kutojua umuhimu wa kuwahi katika vituo vya kutolea huduma, ambapo amesema uwepo wa huduma katika kaya utasaidia kupunguza idadi ya vifo hivyo.


Mafunzo yanayofanywa na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto  kwa kushirikiana na Shirika lisilo la Kiserikali la AMREF, kuhusu utekelezaji wa Mpango wa Huduma za Afya ya Jamii ngazi ya Jamii Mkoa wa Simiyu, yameshawafikia Watendaji wa Kata, Mitaa na Vijiji zaidi ya 350. 
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe.Anthony Mtaka akizungumza na Watendaji wa Kata, Mitaa na Vijiji katika kikao cha kutoa elimu kwa viongozi hao kilichofanyika Mjini Bariadi kuhusu utekelezaji Mpango wa Huduma za Afya ya Jamii ngazi ya Jamii Mkoani humo.
Dkt.Ama Kasangala kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, akizungumza na Watendaji wa Kata, Mitaa na Vijiji katika kikao cha kutoa elimu kwa viongozi hao kilichofanyika Mjini Bariadi kuhusu  utekelezaji Mpango wa Huduma za Afya ya Jamii ngazi ya Jamii Mkoani Simiyu.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe.Anthony  Mtaka(kushoto) na Dkt.Ama Kasangala kutoka Wizara ya Afya wakiteta jambo katika kikao cha kutoa elimu kwa viongozi hao kilichofanyika Mjini Bariadi kuhusu utekelezaji Mpango wa Huduma za Afya ya Jamii ngazi ya Jamii Mkoani humo.
Baadhi ya Watendaji Kata, Mitaa na Vijiji kutoka kwa Halmashauri ya Wilaya ya Itilima wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu,Mhe.Anthony Mtaka katika kikao cha kutoa elimu kwa viongozi hao kilichofanyika Mjini Bariadi kuhusu utekelezaji Mpango wa Huduma za Afya ya Jamii ngazi ya Jamii Mkoani humo.
Baadhi ya Watendaji Kata, Mitaa na Vijiji kutoka kwa Halmashauri ya Mji Bariadi wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu,Mhe.Anthony Mtaka katika kikao cha kutoa elimu kwa viongozi hao kilichofanyika Mjini Bariadi kuhusu utekelezaji Mpango wa Huduma za Afya ya Jamii ngazi ya Jamii Mkoani humo.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe.Anthony Mtaka(wa tano kulia) akiwa katika picha ya pamoja na  Baadhi ya Watendaji Kata, Mitaa na Vijiji kutoka kwa Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe.Anthony Mtaka(wa tano kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Baadhi ya Viongozi wa Mkoa, Wizara ya Afya  na  Watendaji Kata, Mitaa na Vijiji kutoka kwa Halmashauri ya Wilaya ya Itilima
Baadhi ya Watendaji Kata, Mitaa na Vijiji kutoka kwa Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu,Mhe.Anthony Mtaka katika kikao cha kutoa elimu kwa viongozi hao kilichofanyika Mjini Bariadi kuhusu utekelezaji Mpango wa Huduma za Afya ya Jamii ngazi ya Jamii Mkoani humo

Wednesday, May 24, 2017

WANUFAIKA TASAF WAHIMIZWA KUWAPELEKA WATOTO SHULE, KLINIKI

Wanufaika wa Mradi wa Mpango wa Kunusuru kaya maskini TASAF III hususani wanaopewa ruzuku ya utimizaji wa masharti ya elimu na afya wamehimizwa kuwapeleka watoto kliniki na kuhakikisha watoto wao wanahudhuria shuleni.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Ndani kutoka TASAF Makao Makuu, Ndg. Christopher Sanga katika kijiji cha Migato wilayani Itilima wakati wa ziara ya tathmini ya utekelezaji mradi wa TASAF wilayani humo.

Sanga amesema Serikali ina mpango mzuri kwa wananchi wa kuhakikisha watoto wote wenye umri wa kwenda shule wanapelekwa shule na pia watoto wote wenye umri chini ya miaka mitano wanapelekwa kiliniki na kupata  huduma za afya zinazotakiwa, hivyo akawaasa kutorudisha nyuma juhudi za Serikali.

Aidha, amesema lengo kuu la Serikali ni kuhakikisha nguvu kazi inajengwa kwa kutoa elimu na kuangalia afya za watoto wakiwa bado wadogo ili watakapobainika kuwa na matatizo ya kiafya wapatiwe matibabu mapema kwa lengo la kuimarisha afya na  kutoathiri ukuaji wao.

Ameongeza kuwa utafiti uliofanyika kuhusu utekelezaji wa awamu zilizotangulia za Mpango wa TASAF ulionesha kuwa, kumekuwa na miundombinu mingi ya elimu na afya lakini kaya maskini zimekuwa hazipeleki watoto katika huduma hizo, hivyo Serikali ikatoa ruzuku ya elimu na afya na kuwawekea masharti wazazi ili kuhakikisha wanawapeleka watoto katika huduma hizo.

Amesisitiza kuwa Mpango wa TASAF unafuatilia mahudhurio ya watoto wanaopata ruzuku ya utimizaji wa masharti ya elimu na ili ruzuku hiyo iendelee kutolewa kwa wanafunzi hao ni lazima mahudhurio yao yasiwe chini ya asilimia 80 kwa muhula, wasipohudhuria kuna adhabu inayotolewa ikiwa ni pamoja na kupunguzwa kwa ruzuku hiyo.

“ Miongoni mwa madhara ya watoto kutohudhuria masomo katika muhula husika kwa kaya zinazonufaika na TASAF kwa kupata ruzuku ya elimu ambayo inasaidia kaya hizo, ni kupungua kwa ruzuku na inapopungua uwezo wa kaya katika kujikimu na kufanya mabadiliko ya kiuchumi  unaathirika” amesema Sanga.

Kwa upande wake Bibi. Ngolo Buzenganwa mkazi wa kijiji cha Migato ambaye ni mnufaika wa Mpango wa TASAF III amewataka wazazi wenzake kufuatilia maendeleo ya watoto wao na kukagua daftari zao mara kwa mara ili ruzuku inayotolewa isipunguzwe na iwasaidie kuwawezesha kupata mahitaji muhimu ya shule kwa ajili ya watoto wao.

Katika hatua nyingine wanufaika wa Mpango wa TASAF III wameshukuru mpango huo kwa kutatua changamoto ya upungufu wa maji kwa kuwachimbia visima vya maji kupitia programu ya kazi za ajira za muda na kuomba kuongezewa idadi ya visima hivyo katika awamu nyingine ya utekelezaji wa mradi.

“Tunaishukuru sana TASAF kutuletea maji kwa visima hivi, tulikuwa tunatembea muda mrefu sana zaidi ya saa moja kufuata maji, lakini sasa hivi maji yapo karibu tena ni maji safi na salama” amesema Maila Limbu mkazi  wa Migato.

Naye Mhandisi wa Maji wa Halmashauri ya Wilaya ya Itilima,Goodluck Masige amesema Serikali Wilayani humo imeweka mpango wa kuviwekea pampu visima vyote 194 vilivyochimbwa kupitia mradi wa TASAF ili kuwarahisishia wananchi kupata maji kwa urahisi zaidi kuliko teknojia inayotuika sasa ya kuvuta kwa kamba.


Wilaya Itilima ni moja ya Wilaya tano zinazofanyiwa tathmini ya utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru kaya Maskini (TASAF III) katika awamu hii, tathmini inayofanywa na wataalam kutoka TASAF Makao Makuu, Benki ya Dunia na wadau wengine wa maendeleo (wadau washiriki wa mradi) ambao ni UNDP, UNFPA, ILO pamoja na Umoja wa Nchi za Ulaya(EU).
Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Ndani kutoka TASAF Makao Makuu, Ndg. Christopher Sanga(wa pili kulia) akizungumza na wanufaika wa TASAF III katika kijiji cha Migato wilaya ya Itilima.
Ndg. Wolter Soer (wa pili kushoto) kutoka Benki ya Dunia akizungumza na baadhi ya wanufaika wa TASAF III katika kijiji cha Migato wilaya ya Itilima katika majadiliano yaliyofanywa katika vikundi kupata maoni ya tathmini ya utekelezaji wa mpango huo.
Mnufaika wa TASAF III kutoka kijiji cha Migato wilaya ya Itilima akichota maji katika moja ya visima vilivyochimbwa na TASAF kupitia programu ya kazi za ajira za muda katika kijiji hicho.
Ndg. Wolter Soer kutoka Benki ya Dunia(wa kwanza kushoto) na Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Ndani kutoka TASAF Makao Makuu, Ndg. Christopher Sanga(mwenye miwani) wakimsikiliza mmoja wa wanufaika wa TASAF III katika Kijiji cha Migato akiwaeleza juu faida anazopata kupitia fedha anazopokea kupitia mpango huo.
Mmoja wa wanufaika wa TASAF III katika Kijiji cha Migato akipokea fedha katika zoezi la uhawilishaji lililofanyika kijijini hapo
Baadhi ya wanufaika wa TASAF III wa Kijiji cha Migato wakiimba wimbo maalum wa kuwakaribisha wataalam kutoka TASAF Makao Makuu, Benki ya Dunia na wadau wengine wa maendeleo (wadau washiriki wa mradi) ambao ni UNDP, UNFPA, ILO na Umoja wa Nchi za Ulaya(EU) waliofika kufanya tathmini ya utekelezaji wa mradi wa TASAF III Wilayani Itilima.
Mnufaika wa TASAF III kutoka kijiji cha Migato wilaya ya Itilima akichota maji katika moja ya visima vilivyochimbwa na TASAF kupitia programu ya kazi za ajira za muda katika kijiji hicho.

Monday, May 15, 2017

DED MEATU: MBEGU BORA, KILIMO CHA MKATABA MKOMBOZI KWA WAKULIMA WA PAMBA

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, Fabian Manoza amesema Matumizi ya Mbegu bora na Kilimo cha Mkataba ni suluhu ya wakulima wa pamba inayoweza kuwasaidia kuongeza uzalishaji.
Manoza ameyasema hayo wakati akitoa taarifa ya Wilaya ya Meatu kuhusu kilimo cha Pamba kwa Wakuu wa Mikoa nane ya Kanda ya Magharibi inayolima pamba waliotembelea eneo hilo kutoka Simiyu, Shinyanga, Geita, Mwanza, Kagera, Kigoma, Singida na Tabora katika ziara yao kuona mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora ya pamba(UKM08) katika kata ya Mwabusalu wilayani Meatu.
Amesema kupitia kilimo cha mkataba wananchi watakuwa na uhakika wa kupata pembejeo bora za kilimo zikiwemo mbegu bora, mbolea na viuadudu kutoka kwa watu au makampuni yatakayoweka mikataba nao.
“Tunatarajia kuongeza uzalishaji ili kupata kata nyingi zaidi, tumewasisitiza wananchi kuwa kilimo hiki cha mbegu bora lazima kiendane na kilimo cha mikataba, wale wanaohitaji kununua pamba lazima waingie mikataba na wakulima ili wapate faida walizokuwa hawazipati; baadhi yao wamekuwa wakihangaika hawana uwezo wa kununua mbegu, viuadudu na kuhudumia mashamba, lakini wakiingia mikataba hao watakaonunua pamba watatoa huduma zote hizo kwa wakulima” alisema.
Ameongeza kuwa pamoja na kilimo cha mkataba na matumizi ya mbegu bora ili kuboresha uzalishaji wa pamba Wataalam wa Kilimo wanapaswa kuwapa wakulima huduma zote muhimu za ugani ili wazingatie taratibu zote za kuandaa mashamba, upandaji na utunzaji wa pamba.
Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Meja Jenerali Ezekiel Kyunga ameitaka Bodi ya Pamba nchini kuboresha utaratibu wa kilimo cha mkataba ili kiweze kuwanufaisha wakulima badala ya kuwakatisha tamaa.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mhe.Aggrey Mwanri amesema ni vema Bodi ya Pamba ikaweka  utaratibu utakaowawezesha wakulima kupata mbolea na zana bora za kilimo kwa mkopo ambao watarejesha baada ya mavuno.
Mkurugenzi wa Bodi ya Pamba, Marco Mtunga amesema wakulima wa pamba kwa miaka ya nyuma wamekuwa wanakumbana na changamoto mbalimbali ikiwemo  ukosefu wa mbegu bora na kutopanda kwa kuzingatia mistari, hivyo katika msimu wa mwaka 2017 jumla ya tani 8000 za mbegu bora zitazalishwa kwa ajili ya kusambaza kwa wakulima na jitihada zinaendelea kufanywa kupitia kilimo cha mkataba kuhamasisisha wakulima kulima kwa kuzingatia ushauri wa wataalamu.
Aidha, Mtunga amesema ili kuongeza uzalishaji wa pamba wakulima wahamasishwe kulima kilimo cha mkataba na ili kilimo cha mkataba kiwe na tija kwao Bodi hiyo inaendelea kutimiza wajibu wake kusimamia masharti yaliyowekwa katika utekelezaji wa mikataba hiyo kati ya wachambuzi  na wakulima wa pamba.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe.Dkt.Rehema Nchimbi amesisitiza kuwepo kwa mikakati ya kilimo cha umwagiliaji katika zao la pamba ikiwepo uchimbaji wa mabwawa makubwa yatakayowasaidia wakulima wakati wote badala ya kutegemea mvua tu.
Naye  Bw.Charles Thobias Mkulima wa kata ya Mwabusalu ambaye ametumia mbegu bora ya pamba ya (UKM08) amesema mbegu hiyo imekuwa mkombozi kwa wakulima kwa kuwa kulingana na mazao yalivyo sasa shambani, mavuno yataongezeka kwa kiasi kikubwa ikilinganishwa na msimu uliopita.

Utekelezaji wa Mpango wa uzalishaji wa Mbegu bora katika kata ya Mwabusalu Wilaya ya Meatu Mkoani Simiyu umehusisha jumla ya wakulima 1,709 katika vijiji vinne ambao kwa pamoja wameweza kulima jumla ya ekari 6,506 na unafadhiliwa na Programu ya Kuendeleza Kilimo cha Pamba chini ya usimamizi wa Bodi ya Pamba.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, Fabian Manoza(Mwenye kofia ya njano0 akitoa maelezo kwa Wakuu wa Mikoa ya Kanda ya Magharibi inayolima pamba ya Simiyu, Shinyanga, Geita, Mwanza, Kagera, Kigoma, Singida na Tabora walipotembelea mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora ya pamba(UKM08) katika kata ya Mwabusalu wilayani humo

Mkuu wa Wilaya ya Bariadi,Mhe.Festo Kiswaga (wa tatu kushoto) akiwakaribisha wakuu wa mikoa ya Kanda ya Magharibi inayolima pamba  walipotembelea mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora ya pamba(UKM08) katika kata ya Mwabusalu wilayani Meatu

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe.Dkt.Rehema Nchimbi (wa pili kushoto) akichangia jambo wakati wa ziara ya wakuu wa mikoa ya Kanda ya Magharibi inayolima pamba  walipotembelea mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora ya pamba(UKM08) katika kata ya Mwabusalu wilayani Meatu(kulia) Mkuu wa Wilaya ya Bariadi,Mhe.Festo Kiswaga ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Simiyu,Mhe.Anthony Mtaka.

Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mhe.Aggrey Mwanri (wa pili kushoto) akichangia jambo wakati wa ziara ya wakuu wa mikoa ya Kanda ya Magharibi inayolima pamba  walipotembelea mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora ya pamba(UKM08) katika kata ya Mwabusalu wilayani Meatu.
Mkurugenzi wa Bodi ya Pamba, Marco Mtunga akitoa ufafanuzi wa hoja mbalimbali kwa wakuu wa mikoa ya Kanda ya Magharibi inayolima pamba  walipotembelea mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora ya pamba(UKM08) katika kata ya Mwabusalu wilayani Meatu
Mkuu wa Mkoa wa Geita,  Meja Jenerali Ezekiel Kyunga akiwasalimia wananchi wa Kata ya Mwabusalu wakati wa ziara ya Wakuu wa Mikoa ya Kanda ya Magharibi inayolima pamba  walipotembelea mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora ya pamba(UKM08) ya katika kata hiyo wilayani Meatu.
Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Meja Jenerali Salum Kijuu akisalimiana na baadhi ya viongozi wa Wilaya ya Meatu  wakati wa ziara ya Wakuu wa Mikoa ya Kanda ya Magharibi inayolima pamba  walipotembelea mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora ya pamba(UKM08) ya katika kata hiyo wilayani Meatu.
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga akiwasalimia wananchi wa Kata ya Mwabusalu wakati wa ziara ya Wakuu wa Mikoa ya Kanda ya Magharibi inayolima pamba  walipotembelea mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora ya pamba(UKM08) ya katika kata hiyo wilayani Meatu.
Baadhi ya Wakuu wa mkoa ya Kanda ya Magharibi inayolima pamba  wakati wa ziara yao walipotembelea mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora ya pamba(UKM08) ya katika kata ya Mwabusalu wilayani Meatu.

Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Brigedia Jenerali Emmanuel Maganga akisalimiana na baadhi ya viongozi wa Wilaya ya Meatu  wakati wa ziara ya Wakuu wa Mikoa ya Kanda ya Magharibi inayolima pamba  walipotembelea mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora ya pamba(UKM08) ya katika kata hiyo wilayani Meatu

Bw.Charles Thobias Mkulima kutoka kata ya Mwabusalu ambaye ametumia mbegu bora ya pamba ya (UKM08) akitoa maelezo kwa Wakuu wa Mikoa ya Kanda ya Magharibi inayolima pamba ambayo ni  Simiyu, Shinyanga, Geita, Mwanza, Kagera, Kigoma, Singida na Tabora walipotembelea mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora ya pamba(UKM08) katika kata hiyo wilayani Meatu.

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!