Sunday, May 1, 2016

MPINA ATAKA VIONGOZI WANAOSHINDWA KUSIMAMIA USAFI WAWAJIBISHWE



Naibu Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Muungano na Mazingira, Mhe. Luhaga Mpina amewataka Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa wilaya kuwachukulia hatua viongozi wanaoshindwa kusimamia utekelezaji wa agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. John Pombe Magufuli la kufanya usafi wa Mazingira kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi.

Mhe. Mpina aliyasema hayo alipozungumza na viongozi na wananchi mara baada ya kushiriki kufanya usafi katika kituo cha Afya cha Mwandoya wilayani Meatu, zoezi ambalo lilienda sambamba na uzinduzi wa upandaji wa miti ya matunda katika mkoa wa Simiyu, ambapo Mkoa wa Simiyu umepokea jumla ya miche 18, 400 ya miembe na michungwa kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais.

Mpina alisema viongozi kuanzia ngazi ya Vijiji hadi Mkoa wanao wajibu wa kusimamia usafi wa mazingira katika maeneo yao, kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi kwa kuhakikisha wananchi wanafanya usafi kuanzia saa 12:00 hadi saa 3:00 asubuhi, ikiwa kuna wananchi watakaobainika kushindwa kutekeleza agizo hilo wachukuliwe hatua.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, Mhe. Pius Machungwa alisema viongozi wa Wilaya ya Meatu na mkoa wa Simiyu kwa ujumla wataendelea kuunga mkono juhudi za serikali katika kuhakikisha shughuli za usafi na utunzaji wa mazingira zinaendelezwa.

Wakati huo huo Mhe. Mpina amewahimiza wananchi kupanda miti yenye manufaa , hususani miti ya mbao na matunda kwa sababu itawasidia kupata fedha, chakula na malighafi kwa ajili ya viwanda mbalimbali nchini na hivyo kuinua uchumi wa mwananchi mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu , Bw. Joseph S. Nandrie alikiri mkoa kupokea jumla ya miche ya miembe na machungwa 18,400 ambayo imeshasambazwa katika Halmashauri zote sita na akaahidi kuifuatilia miti hiyo na kuhakikisha inatunzwa.

Aidha Mpina alieleza azma ya Serikali katika kuhakikisha miti inapandwa nchi nzima ili kurejesha uoto wa asili uliopotea, kuongeza uwezo wa kunyonya hewa ya ukaa ambayo imeongezeka duniani kote kutokana na mabadiliko ya tabia nchi.
“Tumeandaa Mpango wa kitaifa wa upandaji wa miti, na kwa kuanzia tumetenga shilingi bilioni 20 kwa mwaka kwa ajili ya upandaji miti nchi nzima, kwa kupanga huko tunataka kila wilaya iwe na kitalu kikubwa cha miti inayoandaliwa kwenda kwa wananchi kwa urahisi. Tunataka kufikia mwaka 2020 watu wakose mahali pa kupanda miti kwa kuwa kila mahali patakuwa na miti” alisema Mpina.

Mhe. Mpina alitoa miche hiyo 18,400 kwa Mkoa wa Simiyu ikiwa ni utekelezaji wa ahadi aliyoitoa wakati wa ziara ya Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa , aliyoifanya Mkoani Simiyu mapema mwezi Machi, 2016 na ameahidi kuongeza miche hadi kufikia 30,000. 
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Mhe. Luhaga J. Mpina akishiriki kufanya usafi pamoja viongozi na wanachi katika eneo la Kituo cha Afya cha Mwandoya, wilaya ya Meatu mkoani Simiyu Aprili 30 mwaka huu, ikiwa ni utekelezaji wa Agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, la kufanya usafi wa mazingira kila Jumamosi ya Mwisho wa mwezi. Picha Na Stella A. Kalinga

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Mhe. Luhaga J. Mpina akipanda mti wa mwembe katika kijiji cha Mwandoya wilayani Meatu, wakati wa uzinduzi wa zoezi la upandaji miti 18,400 ya michungwa na miembe iliyotolewa na Ofisi Makamu wa Rais kwa Mkoa wa Simiyu, zoezi hili lilifanyika baada ya kukamilisha usafi wa mazingira katika Kitua cha Afya cha Mwandoya, Meatu. Picha na Stella A. Kalinga


0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!