Tuesday, July 19, 2016

RC SIMIYU: VIONGOZI WA DINI WAHUBIRINI WATU WAACHANE NA USHIRIKINA



Viongozi wa dini wametakiwa kuwahubiria waumini  wao kuachana na imani za kishirikina ikiwa ni pamoja na kuamini katika ramli chonganishi.

Wito huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony J. Mtaka wakati alipozungumza na washirika wa Kanisa la Waadventista Wasabato na wakazi wa Bariadi, wakati wa ufunguzi wa  mahubiri yaliyoandaliwa na Kanisa La Wadventista Wasabato Mtaa wa Ntuzu ambayo yameanza rasmi mapema wiki hii katika viwanja vya mpira  wa mikono, karibu na Kanisa la Waadventista Wasabato Mjini Bariadi.

Mtaka  amesema baadhi ya wananchi wamekuwa wanaamini katika ramli chonganishi hali inayosababisha baadhi yao kupoteza maisha kwa sababu ya kukosa tiba sahihi kutokana na wao kuamini katika masuala ya uganga hata kama magonjwa wanayoumwa yanatibika katika vituo vya kutolea huduma za Afya.

“Nawaomba muwahubirie sana watu wa Bariadi, kuna watu hapa akiumwa malaria anaamini  mpaka akachanjwe chale  kwa mganga ndiyo atapona, naamin viongozi wote hapa mtaona ni jinsi gani hawa watu wanahitaji kusaidiwa”, alisema Mtaka.

Kwa upande wake Mjumbe wa Kamati ya Maandalizi ya Mahubiri hayo Mchungaji Peter Bahini alisema Mahubiri hayo yamelenga kuwatoa watu katika vitendo vya uhalifu  na vile vinavyoendana na imani za kishirikina ikiwa ni pamoja na ukataji wa mapanga hasa kwa vikongwe na mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi (Albino).

Mchungaji Bahini alisema mahubiri hayo yamesaidia zaidi ya watu 200 kubadili tabia zao kwa kuacha maovu  ambao wamekukubali kubatizwa.

Wakati huo huo Mkuu wa Mkoa wa Simiyu amewataka waimbaji wa kwaya ya Kanisa la Waadventista Wasabato-Kurasini, kuweka malengo ya kuwa na studio ya kurekodi nyimbo ili warekodi nyimbo zao katika studio yao wenyewe, ambapo aliahidi kuchangia na kuwashirikisha wadau wengine na wapenzi wa kwaya hiyo kuchangia.

“Ndugu zangu kwaya ya SDA Kurasani ni kwaya Kongwe mno, mna zaidi ya miaka thelathini, sasa hivi mlipaswa kuwa na studio yenu wenyewe, hampaswi kuwa miongoni mwa watu wanaoibiwa kazi zao”, alisema Mtaka.

Aidha, Mtaka alishauri Uongozi wa Kwaya SDA Kurasini kuanzisha vitu viwili kwanza,  ikiwa ni tovuti itakayotumika kutangaza kazi mbalimbali za kwaya na kufungua akaunti ya benki ambayo itatumika na mashabiki hao kuichangia michango mbalimbali kwa ajili ya kuiwezesha kwaya katika masuala mbalimbali.
    
Sanjari na hilo Mkuu wa Mkoa alisema amesikitika kuona  baadhi ya shule za madhehebu ya dini zimefanya vibaya katika matokeo ya Mtihani wa Kidato cha Sita kwa mwaka  2016, ambapo aliwataka Viongozi wa Madhehebu ya dini kuliangalia kwa upya suala hilo, kulifanyia kazi na kuweka mikakati ya kufanya vizuri katika mitihani ya kitaifa ijayo.

Mahubiri yaliyoandaliwa na Kanisa La Wadventista Wasabato Mtaa wa Ntuzu yaliyofunguliwa na Mhe. Mkuu wa Mkoa yanatarajiwa kufungwa rasmi Julai 30, 2016.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony J. Mtaka akivalishwa skafu na vijana wa Pathfinder wa  kanisa la Waadventista (Wasabato),ikiwa ni maandalizi ya  kufungua mahubiri yaliyoandaliwa na kanisa hilo mjini Bariadi mapema wiki hii.(Picha na Stella A. Kalinga)
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony J. Mtaka (mwenye skafu ya njano kulia) akiimba pamoja na Waimbaji wa Kwaya ya kanisa la Waadventista (Wasabato) ya Kurasini Dar es Salaam, mara baada ya kufungua mahubiri yaliyoandaliwa na kanisa hilo mjini Bariadi, mapema wiki hii.(Picha na StellaA. Kalinga)
Mkuu wa Mkoa Mhe. Anthony J. Mtaka (mwenye skafu ya njano kulia) akiimba pamoja na Waimbaji wa Kwaya ya kanisa la Waadventista (Wasabato) ya Kurasini Dar es Salaam mara baada ya kufungua mahubiri yaliyoandaliwa na kanisa hilo mjini Bariadi, mapema wiki hii, (wa pili kulia) Afisa Upelelezi wa Mkoa, Jonathani Shana. (Picha na Stella A. Kalinga)

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!