Wednesday, July 20, 2016

WAKUU WA WILAYA, WAKURUGENZI WAAGIZWA KUHAKIKI WANAFUNZI HEWA



Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony J. Mtaka amewataka Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri zote kutambua idadi kamili ya wanafunzi katika maeneo yao, ili fedha zinazoletwa na Serikali kwa ajili ya elimu bila malipo zifanye kazi iliyokusudiwa.

Mhe. Mtaka amelitoa agizo hilo katika kikao cha kazi kilichokusudia kutoa tathmini ya elimu na kutoa dira ya usimamizi na uendeshaji wa elimu katika mkoa, ambacho kiliwahusisha wadau mbalimbali wa elimu wa Mkoa wa Simiyu kilichofanyika mjini Bariadi, katika ukumbi wa Shule ya Sekondari Bariadi.

Mhe. Mtaka alisema baadhi ya walimu wakuu na wakuu wa shule wamekuwa wakitoa takwimu zisizo sahihi pale zinapohitajika ili waweze kuletewa fedha nyingi  za elimu bila malipo kuliko idadi halisi ya wanafunzi waliopo shuleni.

“Nawaagiza Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wote kila mmoja katika eneo lake ahakikishe anatambua idadi kamili ya wanafunzi kwa kila shule ili kubaini wanafunzi hewa, Wakurugenzi muwasilishe taarifa hizo katika Kamati za Ulinzi na Usalama za wilaya; katika taarifa muoneshe hatua mlizochukua dhidi ya wakuu wa shule na walimu wakuu waliodanganya takwimu za wanafunzi”, alisema Mtaka. 

Mtaka alisema kumekuwa na tatizo la utoro na mdondoko kwa shule za msingi na sekondari katika Mkoa wa Simiyu ambapo wanafunzi wanaachishwa shule kwa sababu mbalimbali zikiwemo za kuchunga  mifungo na kuozwa kwa wanafunzi wa kike.

Kufuatia kuwepo kwa tatizo la utoro Mkuu wa Mkoa aliwataka Wakurugenzi kuwataka walimu wakuu na wakuu wa shule kutoa maelezo ya kina juu ya matumizi ya fedha za elimu ya bila malipo kwa wanafunzi watoro.

Aidha, Afisa Elimu Mkoa, Mwl. Julius Nestory amewaomba Wenyeviti wa Halmashauri na Wabunge wasaidie katika kusimamia sheria zilizoandaliwa kwa ajili ya kudhibiti suala la utoro,  ikiwa ni namna mojawapo ya kukabiliana na ujinga kwa jamii ya watu wa Simiyu.

Wakati huo huo Mbunge wa Maswa Mashariki, Mhe. Stanslaus Nyongo amesema katika harakati za kusaidia kuondoa ujinga Mkoani Simiyu, amewaomba wafanyabiashara wa Mkoa wa Simiyu kuwekeza katika elimu ikiwa ni pamoja na kujenga shule na vyuo kwa kuwa sekta binafsi ina mchango mkubwa katika maendeleo ya elimu nchini.

Katika mikakati ya kuongeza kiwango cha ufaulu, Mhe. Mkuu wa Mkoa aliagiza madarasa ya mitihani kwa shule za msingi na sekondari yalelewe na viongozi na yatafutiwe utaratibu wa kuwa na kambi za kitaaluma kama ilivyo kwa upande wa michezo, ambapo wanafunzi kutoka maeneo tofauti watakutanishwa na kushindanishwa ili kuwajengea uwezo na kuwaandaa kwa ajili ya mitihani ya kitaifa.

Kiwango cha ufaulu kwa mwaka 2015 katika Mkoa wa Simiyu kimepanda ikilinganishwa na mwaka 2014 ambapo kwa upande wa darasa la saba ufaulu umepanda kufikia asilimia 61 mwaka 2015 kutoka asilimia 44 mwaka 2014, kidato cha nne asilimia 72.5 kutoka 70 mwaka 2014 na kidato cha sita 2015 ufaulu ulipanda mpaka asilimia 98.2. 

Mkuu wa Mkoa Mhe. Anthony J. Mtaka (katikati) akizungumza na wadau wa elimu katika kikao cha tathmini ya elimu na dira ya usimamizi na uendeshaji wa elimu mkoani Simiyu,(kushoto) Katibu Tawala Mkoa Simiyu, Bw.Jumanne A. Sagini na (kulia) Afisa Elimu Mkoa , Mwl. Julius K. Nestory.(Picha na Stella A. Kalinga)
 
Kutoka kulia, Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga, anayefuata, Mkuu wa Wilaya ya Itilima Mhe.Benson Kilangi, Mkuu wa Wilaya ya Meatu Mhe. Joseph Chilongani na Mkuu wa Wilaya ya Busega Mhe.Tano Mwera wakipiga makofi kuashiria pongezi wakati Mkuu wa Mkoa wa Simiu alipokuwa akizungumza na Wadau wa elimu Mjini Bariadi.
Mkuu wa Mkoa wa Simiy, Mhe. Anthony J. Mtaka akipewa maelezo juu ya jaribio la namna ya kutambua kemikali  na Christina Francis, mwanafunzi wa darasa la saba katika Shule ya Msingi Somanda A, kabla ya kufungua  kikao cha tathmini ya elimu na dira ya usimamizi na uendeshaji wa elimu mkoani Simiyu, kilichofanyika jana Mjini Bariadi. (Picha na Stella A. Kalinga)
Mkuu wa Mkoa wa Simiy, Mhe. Anthony J. Mtaka akivalishwa skafu na Vijana wa Skauti katika Shule ya Sekondari Bariadi, kabla ya kufungua  kikao cha tathmini ya elimu na dira ya usimamizi na uendeshaji wa elimu mkoani Simiyu, kilichofanyika jana Mjini Bariadi. (Picha na Stella A. Kalinga)

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!