Thursday, November 24, 2016

WANAUME WAHAMASISHWA KUFANYA TOHARA KUPUNGUZA MAAMBUKIZI YA VVU


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka(wa tatu kushoto) akizungumza na wadau wa Mapambano dhidi ya Ukimwi  katika Uzinduzi wa Mpango mkakati wa Mkoa huo uliofanyika  katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki  la Mtakatifu Yohana Mjini Bariadi.
Baadhi ya Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi na wadau wengine wa Mapambano dhidi ya Ukimwi wa Mkoa wa Simiyu wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa huo (hayupo pichani) katika Uzinduzi wa Mpango mkakati wa Mkoa huo uliofanyika  katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki  la Mtakatifu Yohana Mjini Bariadi.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Dkt. Mageda Kihulya akiwasilisha mada katika  Mkutano wa wadau wa Mapambano dhidi ya Ukimwi wa mkoa huo  uliofanyika  katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki  la Mtakatifu Yohana Mjini Bariadi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Maswa, Dkt. Fredrick Sagamiko akichangia jambo katika  Mkutano wa wadau wa Mapambano dhidi ya Ukimwi wa mkoa huo  uliofanyika  katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki  la Mtakatifu Yohana Mjini Bariadi.
Baadhi ya wadau wa Mapambano dhidi ya Ukimwi wa Mkoa wa Simiyu wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa huo (hayupo pichani) katika Uzinduzi wa Mpango mkakati wa Mkoa huo uliofanyika  katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki  la Mtakatifu Yohana Mjini Bariadi.
Mchungaji wa Kanisa la  AICT Bariadi Mjini, Amosi Ndaki(kushoto)  na Shekhe wa Mkoa wa Simiyu, Mahamoud Kalokola (kulia) wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa katika Mkutano wa wadau wa Mapambano dhidi ya Ukimwi wa mkoa huo  uliofanyika  katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki  la Mtakatifu Yohana Mjini Bariadi.
Mratibu wa Shirika lisilo la Kiserikali la AGPAHI Mkoa wa Simiyu na Shinyanga, Dkt. Gastor Njau akiwasilisha katika  Mkutano wa wadau wa Mapambano dhidi ya Ukimwi wa mkoa huo  uliofanyika  katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki  la Mtakatifu Yohana Mjini Bariadi.
Mchungaji wa Kanisa la  AICT Bariadi Mjini, Amosi Ndaki(kushoto)  akichangia jambo katika  Mkutano wa wadau wa Mapambano dhidi ya Ukimwi wa mkoa huo  uliofanyika  katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki  la Mtakatifu Yohana Mjini Bariadi
Na Stella Kalinga
Wanaume ambao bado hawajafanyiwa tohara mkoani Simiyu wamehamasishwa  kufanya hivyo ili kukabiliana na maambukizi mapya ya Virusi vya Ukimwi Mkoani humo.

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony J. Mtaka katika ufunguzi wa Mkutano wa wadau wa Mapambano dhidi ya Ukimwi na Uzinduzi wa Mpango mkakati wa Mkoa huo uliofanyika jana katika Ukumbi wa Kanisa Katoliki  la Mtakatifu Yohana Mjini Bariadi.

Mtaka amesema kwa mujibu wa tafiti  zilizofanyika nchini Afrika ya Kusini, Kenya na Uganda  imethibitishwa pasipo shaka  kuwa tohara kwa wanaume hukinga maambukizi ya Virusi vya Ukimwi kwa asilimia 60, hivyo wanaume wajitokeze waweze kupata huduma hiyo bure.

Akizungumza kwa niaba ya Mratibu wa Mapambano dhidi Ukimwi Mkoa wa Simiyu, Mratibu wa Mapambano dhidi ya Ukimwi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi, Daktari Wilfred Magulu amesema ni asilimia 32 tu ya wanaume Mkoani Simiyu ambao wamefanyiwa tohara.

Daktari Magulu amesema Serikali imeweka mkakati wa kutoa elimu kwa wananchi hususani wanaume na kuwahamasisha ili wawe na mwamko na kuona umuhimu wa kufanyiwa tohara pasipo gharama yoyote katika Hospitali zote na vituo vyote vya kutolea huduma za afya, kwa lengo la kufikia asilimia 72 ya Kitaifa.

Sambamba na hilo Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka amesema wataalam wa afya na wadau wa Ukimwi kwa ujumla wanao wajibu wa kuwaelimisha wananchi juu  ya kujikinga na maambukizi, umuhimu wa kupima VVU na kuwajengea ujasiri wa kupokea matokeo ya vipimo vyao ili wanapogundulika kuwa na maambukizi waanze matibabu mapema.

Mtaka amesema wataalam hao wanatakiwa kuliepusha Taifa katika maambukizi mapya ya VVU kwa kuwaeleza wananchi ukweli juu ya njia sahihi za kujikinga na maambukizi mapya ikiwa ni pamoja na Matumizi sahihi ya kondomu.

“Waratibu waelezeni watu umuhimu wa kujikinga na maambukizi, fanyeni utafiti kuona maduka mangapi ya vijijini yanauza kondomu mkikuta hakuna wapimeni wananchi katika hivyo vijiji muone hali ya maambukizi ikoje, Msisiishie kuyazungumza masuala haya kwenye makongamano na warsha” , alisema Mtaka.

Ameongeza kuwa Waratibu wa Mapambano dhidi ya Ukimwi katika Halmashauri zote za Mkoa huu wahakikishe baa  na nyumba zote za kulala wageni zilizopo mijini na maeneo yote yenye watu wengi zinawekewa kondomu  na elimu ya matumizi sahihi ya kondomu hizo itolewe kwa wananchi.

Wakati huo huo Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Dkt.Mageda Kihulya amesema wananchi wajijengee utaratibu wa kupima afya na wanapogundulika kuwa na maambukizi Virusi vya Ukimwi watembelee vituo vya kutolea huduma za Afya ili waanze kupewa huduma mapema.

Hali ya maambukizi ya Virusi vya Ukimwi/UKIMWI ni asilimia 3.6 kama ilivyooneshwa kwenye utafiti wa mwaka 2011-2012 ukilinganishwa na kiwango cha Kitaifa cha asilimia 5.1.


Mkutanowa wadau wa mapambano dhidi ya Ukimwi Mkoani Simiyu umewashirikisha Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri, Wenyeviti wa Halmashauri, Wabunge, Viongozi wa Madhehebu ya Dini, Waratibu wa Mapambano dhidi ya Ukimwi wa Wilaya zote na Wakuu wa Mashirika yasiyo ya Kiserikali yanayojihusisha na Mapambano dhidi ya Ukimwi mkoani humo.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!