Thursday, August 11, 2016

RC SIMIYU AISHAURI SERIKALI KUFUTA MPANGO WA TASAF



Na Stella Kalinga
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka ameishauri Serikali kufuta utaratibu wa kutoa fedha kwa kaya maskini zinazotolewa kupitia Mpango wa Kunusuru kaya maskini TASAF III na badala yake uandaliwe utaratibu wa kuwawezesha wananchi kupata ruzuku ya mbegu na pembejeo nyingine za kilimo.

Mtaka ametoa ushauri huo wakati wa zoezi la uhawilishaji wa fedha katika kijiji cha Itinje wilayani Meatu, ambapo jumla ya shilingi 2,800,000 zilitolewa kwa kaya 77 zinazonufaika na mpango huo.
Mtaka amesema Serikali inatumia zaidi ya Bilioni 400 kwa ajili ya Mpango wa TASAF nchi nzima na wakati huo baadhi ya malengo ya TASAF III yameanza kutekelezwa na Serikali ikiwa ni pamoja na utoaji wa elimu bila malipo, utoaji wa huduma za afya bure kwa wazee na Mfuko wa Huduma ya Afya kwa Jamii (CHF) hivyo, malengo ya TASAF yamepungua.

“Hizi shilingi bilioni 1.7 zilizotolewa kwa mwaka mmoja kwa Meatu tu, zingetolewa kama ruzuku kwa wakulima wa pamba, mngeweza kupata mbegu bure, dawa bure mkalima pamba na mkapata fedha nyingi kuliko nikiwagawia hizi elfu thelathini, elfu hamsini na watu wengine humo katikati wanaiba hizo fedha, Nitakuwa kiongozi wa kwanza tena kijana kupendekeza huko mbele Serikali ifute mpango huu wa TASAF”, alisema Mtaka.

Mtaka amesema wananchi wanapaswa kusaidiwa  njia sahihi za kutafuta fedha kwa ajili ya kujikwamua katika umaskini ikiwa ni pamoja na kujishughulisha na kilimo, ufugaji, ujasiriamali na kupewa fedha ambazo wanufaika walio wengi  hawazitumii kwa malengo yaliyokusudiwa.

Aidha, Mtaka amesema watoto watimize wajibu wa kuwatunza wazazi wao kwa kuwa baadhi ya wanufaika wa mpango wa TASAF III ni wazee waliotelekezwa na watoto wao, hiyo wazee wawakumbushe watoto wao ili wawasaidie kuwatimizia mahitaji muhimu.
Pamoja na ushauri wake kwa Serikali Mkuu huyo wa mkoa amewataka wanufaika wa mpango huo kujiandaa  na kujipanga namna watavyojipatia mahitaji yao muhimu endapo mpango huu utasitishwa na akawataka wajikite katika ufugaji na kilimo cha Pamba na alizeti.

“Nawapa hizi pesa leo ila nawashauri kila mmoja ajipange, ikitokea TASAF inafutwa leo ajue atapataje mahitaji yake ya kila siku. Natamani muwe watu mnaopenda kupata nyavu kwa ajili ya kuvua samaki badala ya kupenda kupewa samaki, hizi pesa zitawalemaza”

Nae Mkuu wa Wilaya ya Meatu Dkt. Joseph Chilongani amesema uhalisia wa utekelezaji wa mpango huo wa kunusuru kaya maskini haujakaa vizuri kwani haoni kama unamuondolea mwananchi umaskini.

Dk Chilongani ameeleza kuwa ni vema  fedha hizo zitafutiwe utaratibu mzuri wa kuwasaidia wananchi kupitia vikundi vitakavyojishughulisha na shughuli za kuwaongezea kipato kuliko unavyotekelezwa kwa sasa.


 Mpango wa kunusuru Kaya Maskini TASAF III Wilayani Meatu unatekelezwa katika jumla ya kaya 5727 zilizoandikishwa katika vijiji 68 kati ya 106 vilivyopo wilayani humo, ambao kufikia mwezi Agosti 2016, Halmashauri ya Wilaya ya Meatu imeshapokea jumla ya shilingi 1, 793,421,272.73


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka (kulia) akimkabidhi fedha mmoja wa wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya maskini TASAF III, katika kijiji cha Itinje wilayani Meatu, wakati wa uhawilishaji wa fedha kwa wanufaika wa kijiji hicho. (Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu)
Baadhi ya wanufaika wa Mpango wa kunusuru Kaya Maskini katika kijiji cha Itinje wilayani Meatu wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka (hayupo pichani). (Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu)
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, Fabian Manoza (kushoto) akizungumza na wanufaika wa Mpango wa kunusuru Kaya Maskini katika kijiji cha Itinje wilayani Meatu (hawapo pichani) kabla ya kumkaribisha Mratibu wa TASAF Wilaya ya Meatu (hayupo pichani) kuwasilisha taarifa ya Wilaya. (Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu)
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, Pius Machungwa (wa pili kushoto), akizungumza na wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya maskini TASAF III, katika kijiji cha Itinje wilayani Meatu (hawapo pichani) kabla ya zoezi la uhawilishaji wa fedha kwa wanufaika hao  kushoto , Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka (katikati) akizungumza na wanufaika wa mpango wa kunusuru kaya maskini TASAF III, katika kijiji cha Itinje wilayani Meatu.(hawapo pichani), kabla ya zoezi la uhawilishaji wa fedha kwa wanufaika hao, kutoka kushoto Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, Fabian  Manoza, Mkuu wa Wilaya ya Meatu, Dkt. Joseph Chilongani (Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu)




0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!