Thursday, August 4, 2016

SERIKALI MKOANI SIMIYU YAAMUA ASILIMIA MBILI YA USHURU WA PAMBA IJENGE MADARASA

 Na Stella Kalinga

Serikali Mkoani Simiyu imesema  asilimia mbili ya ushuru wa zao la pamba inayopatikana katika Halmashauri zote za Mkoa wa Simiyu ielekezwe katika ujenzi wa Miundombinu ya elimu ya msingi na sekondari,hususani vyumba vya madarasa.

Uamuzi huo umefikiwa kufuatia majadiliano ya pamoja kati ya Uongozi wa Mkoa na Halmashauri zote katika kikao  kilichoongozwa na Mkuu wa mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony J. Mtaka akiwa na Wakuu wa Wilaya, Wenyeviti wa Halmashauri, Wakurugenzi wa Halmashauri, Makatibu Tawala Wilaya na Wajumbe wa Kamati za Fedha za Halmashauri ili kujadili mstakabali wa ujenzi wa vyumba vya madarasa katika mkoa huo.

Mtaka amewaelekeza Wakurugezi wote wakafanye uhakiki na kuainisha takwimu sahihi  za mahitaji ya vyumba vya madarasa ili kupata uhakika wa vyumba vinavyohitajika katika mkoa mzima na kupanga mkakati wa namna vyumba hivyo vitakavyojengwa ikiwa ni pamoja na teknolojia itakayotumika katika kufyatua matofali  pamoja na gharama zake na kuwasilisha taarifa katika Ofisi yake tarehe 9 Agosti, 2016, ambapo baada ya kupata taarifa hiyo na kujiridhisha zoezi la ufyatuaji matofali kimkoa litazinduliwa rasmi Wilayani Maswa tarehe itakayopangwa na mkoa.

“ Sina uhakika sana na takwimu hizi, niwaagize tena Wakurugenzi wote mkafanye mapitio upya na uhakiki wa kina katika maeneo yenu juu ya idadi ya vyumba vya madarasa vinavyohitajika kwa Elimu ya Msingi na Sekondari. Mkae na wataalam wenu wa ujenzi mfanye tathmini ya namna mtakavyojenga kama mtatumia matofali ya kuchoma, matofali ya block au matofali yakufungamana (interlocking blocks) yanayofyatuliwa na vijana waliopewa mafunzo na Shirika la Nyumba la Taifa,ambao wako katika kila halmashauri pamoja na gharama zitakazotumika”, alisema Mtaka.

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Jumanne Sagini amewataka Wakurugenzi kufanya utaratibu wa kubadilisha matumizi ya fedha haraka  pale inapobidi kwa kufuata sheria kanuni na taratibu kufanikisha zoezi la ujenzi wa vyumba vya madarasa ili kuwatengenezea wanafunzi mazingira mazuri ya kujifunzia na kuwezesha madawati yaliyotengenezwa ambayo hayana mahali pa kuwekwa yasiharibike kwa kupigwa na jua na kunyeshewa na mvua.

Pamoja na kutenga asilimia mbili ya ushuru wa pamba, Mtaka amesema Mkoa unakusudia kufanya Harambee kubwa itakayowashirikisha viongozi na wadau wengine muhimu kutoka ndani na nje ya mkoa ambao watachangia kwa kuunga mkono jitihada za Serikali Mkoani humo, katika kuondoa tatizo la upungufu wa vyumba vya madarasa kwa Mkoa wa Simiyu.

Akichangia hoja hiyo ya harambee Mbunge wa Jimbo la Maswa Magharibi , Mhe.Mashimba Ndaki amesema, hiyo itakuwa ni fursa kwa wenyeji wa Mkoa wa Simiyu walo ndani na nje  kuchangia maendeleo ya Mkoa wao na akasisisitiza fedha zitakazokusanywa zisimamiwe vizuri na viongozi.

Katika hatua nyingine Mkuu wa Mkoa wa Simiyu amekabidhi simu tano kwa Wakuu wa Wilaya tano za Mkoa huo zilizotolewa na idara ya mahakama kwa lengo la kutekeleza mpango wa  mapambano dhidi ya rushwa na vitendo vinavyokwenda kinyume na maadili ya Utumishi wa Umma katika utoaji wa huduma za Mahakama, ambazo zitagawanywa kwa maafisa wa dawati la malalamiko kwa kila Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na akaelekeza zitumike kwa malengo yaliyokusudiwa.

Aidha, Mtaka amewataka Wakuu wa Wilaya kutenga siku maalum ya kusikiliza kero za wananchi ambayo Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi  wa Halmashauri watakaa kuwasilikiliza wananchi  na kuwapatia ufumbuzi na pale inaposhindikana masuala yao yapelekwe Ofisi ya Mkuu wa Mkoa kwa ajili ya hatua zaidi.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony J. Mtaka (katikati) akizungumza na Viongozi na Wajumbe wa Kamati za Fedha, Mipango na Uongozi kutoka Halmashauri zote,  katika kikao cha kujadili mikakati ya ujenzi wa vyumba vya madarasa mkoani humo (kushoto) Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Jumanne A. Sagini na (kulia) Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo S. Kiswaga.(Picha na Ofisi ya Mkuu wa Simiyu)
Wakuu wa Wilaya wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu (hayupo pichani) katika kikao cha kujadili mikakati ya ujenzi wa vyumba vya madarasa mkoani humo, mstari wa kwanza kutoka kushoto, Mhe. Benson Kilangi (Itilima), Joseph Chilongani (Meatu), Seif Shekalaghe, Tano Mwera (Busega) na mstari wa pili, kutoka kushoto, Mhe. Stanslaus Nyongo(Mbunge Maswa Mashariki), Mhe. Mashimba Ndaki (Mbunge Maswa Magharibi). (Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu) 
Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya Maswa, Mhe. Dila Mayeka akitoa mchango wake wa mawazo katika kikao kilichofanyika Mjini Bariadi kwa lengo la  kujadili mikakati ya ujenzi wa vyumba vya madarasa mkoani humo.(Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu)
Viongozi na baadhi Wajumbe wa Kamati za Fedha, Mipango na Uongozi wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu (hayupo pichani) katika kikao cha kujadili mikakati ya ujenzi wa vyumba vya madarasa mkoani humo,kilichofanyika Mjini Bariadi. (Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu) 
Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Jumanne A. Sagini  (kushoto) akizungumza kabla ya  kumkaribisha Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony J. Mtaka (kulia) ili azungumze na Viongozi na Wajumbe wa Kamati za Fedha, Mipango na Uongozi kutoka Halmashauri zote,  katika kikao cha kujadili mikakati ya ujenzi wa vyumba vya madarasa mkoani humo, kilichofanyika Mjini Bariadi. (Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu)









0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!