Monday, August 22, 2016

RAIS SHIRIKISHO LA RIADHA ATOA WITO KWA WATANZANIA KUMPOKEA ALPHONCE SIMBU


Na Stella Kalinga

Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT) ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka ametoa wito kwa Watanzania kujitokeza katika kumpokea Mwanariadha, Alphonce Simbu ambaye ameshika nafasi ya tano katika mashindano ya Olimpiki ya Marathoni yaliyofanyika Jijini  Rio de Janeiro nchini Brazili.

Mtaka amesema hayo wakati wa mahojiano maalum na Waandishi wa Habari Ofisini kwake juu ya namna Shirikisho hilo lilivyopokea nafasi ya Mwanariadha huyo katika mashindano ya Olimpiki ya Marathoni mwaka 2016.

Mtaka amesema Mwanariadha huyo na wenzake wanatarajiwa kurejea nchini siku ya Alhamisi mchana tarehe 25 Agosti,2016 katika Uwanja wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere Dar es Salaam, ambapo taratibu za mapokezi zinaendelea kufanywa na Kamati Tendaji ya Shirikisho na akawaomba viongozi katika wizara yenye dhamana na michezo kuona namna ya kushiriki katika mapokezi ya mwanariadha huyo.  

“Hatujapata medali lakini nafurahi kuona mapokeo ya watu kuona kiu ya kuwa tunafanya vizuri , nafikiri mapokeo hayo yaendelee. Kitendo cha Alphonce Simbu kuwa miongoni mwa wanariadha bora watano si jambo dogo, tangu mwaka 1964 Tanzania hatujawahi kupata ushindi katika riadha, Nawaomba Watanzania tumuunge mkono Alphonce Simbu kwa kuwa ameliletea heshima Taifa”alisema Mtaka.

Mtaka amesema ushindi wa Alphonce umetoa mwanga kuwa endapo Serikali itawekeza katika riadha Watanzania wataweza kufanya vizuri katika mashindano ya Jumuiya ya Madola na  Mashindano mengine ya Kimataifa katika siku zijazo, kwa kuwa kabla ya mashindano ya Olimpiki Shirikisho la riadha liliwekeza kwa wanariadha ambapo walikaa kambini kwa takribani miezi nane na shirikisho lilikuwa likiwalipa shilingi 600,000/=  kwa kila mmoja.

Aidha, Mtaka ameshukuru baadhi ya Mashirika ambayo yamejitoa kumsaidia Mwanariadha huyo pamoja na maendeleo ya Riadha na Shirikisho la Riadha kwa ujumla, yakiwemo TTCL, DSTV na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania(TCRA) na akasema Viongozi wa Shirikisho la riadha wamedhamiria kuhakikisha Riadha inailetea heshima Taifa na inawatoa Watanzania Kimasomaso katika medani ya michezo.

“Mwanariadha huyu ameitangaza nchi, Olimpiki ina watazamaji wengi duniani ambao jana wametazama yale mashindano, yule mtangazaji alipomtaja Alphonce Sumbi kuwa namba tano, alisema anatoka katika nchi ambayo Rais wake Kauli mbiu yake ni HAPA KAZI TU. Ni maneno ya Kiswahili lakini yametangazwa na Mtangazaji kutoka katika Shirika la Utangazaji la Kimataifa, ni faraja kubwa hii ni brand kwa nchi; Alphonce ameibrand nchi na Kauli mbiu ya Mhe. Rais”, alisema Mtaka.

Kwa upande wake Katibu wa Chama cha Riadha Mkoa wa Simiyu na Katibu wa Vyama vya Riadha Kanda ya Ziwa, Yohana Msese amempongeza Mwanariadha Alphonce na kuiomba Serikali kutilia mkazo suala la michezo mashuleni ili kuweza kuwatambua watoto wenye vipaji katika michezo mbalimbali na kuwawezesha katika kuviendeleza vipaji hivyo ili kuwajengea mazingira mazuri ya kuwa wachezaji wazuri kwa siku za usoni.

Alphonce Felix Simbu ameshika nafasi ya tano katika mashindano ya Olimpiki ya Mbio za Marathoni za Kilomita 42

Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akizungumza na Waandishi wa Habari Ofisini kwake (hawapo pichani) katika mahojiano maalum juu ya nafasi ya Mwanariadha Mtanzania, Alphonce Sembu aliyeshika nafasi ya tano katika mbio za kilomita 42 kwenye Mashindano ya Olimpiki ya Marathoni yaliyofanyika Jijini  Rio de Janeiro nchini Brazili.(Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu)
Mwanariadha Mtanzania, Alphonce Sembu aliyeshika nafasi ya tano katika mbio za kilomita 42, kwenye Mashindano ya Olimpiki ya Marathoni yaliyofanyika Jijini  Rio de Janeiro nchini Brazili.

Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka (kushoto) akizungumza na Waandishi wa Habari Ofisini kwake (hawapo pihani), katika mahojiano maalum juu ya nafasi ya Mwanariadha Mtanzania, Alphonce Sembu aliyeshika nafasi ya tano katika mbio za kilomita 42, kwenye Mashindano ya Olimpiki ya Marathoni yaliyofanyika Jijini  Rio de Janeiro nchini Brazili , (kulia)  Katibu wa Vyama vya Riadha Kanda ya Ziwa, Yohana Msese.(Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa)

Mwalimu Mbezi Ally, Katibu wa Chama cha Riadha Wilaya ya Bariadi, akizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo pichani) katika mahojiano maalum juu ya nafasi ya Mwanariadha Mtanzania Alphonce Sembu aliyeshika nafasi ya tano katika  Mashindano ya Olimpiki ya Marathoni yaliyofanyika Jijini  Rio de Janeiro nchini Brazili.(Picha na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu)

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!