Sunday, December 25, 2016

SERIKALI MKOANI SIMIYU YATANGAZA KILIMO CHA UMWAGILIAJI KIPAUMBELE MWAKA 2017

Na Stella Kalinga
Serikali Mkoani Simiyu imetangaza Kilimo cha Umwagiliaji kuwa kipaumbele cha mwaka 2017 hususani kilimo cha Mpunga wilayani Busega.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa huo Mhe.Anthony Mtaka katika kikao maalum kilichofanyika jana kati ya uongozi wa mkoa huo, uongozi wa wilaya ya Busega, Maafisa Watendaji wa Kata pamoja na Maafisa Ugani wa Wilaya na wa Kata.

Mtaka amesema katika kutekeleza azma ya Kilimo cha umwagiliaji kuwa kipaumbele mwaka 2017 wilayani Busega , Serikali itawahahamasisha wananchi kulima mpunga na kuhakikisha kuwa maji na miundombinu ya umwagiliaji inawafikia katika mashamba yao kwa kadri ya utaratibu utakaowekwa. 

Mtaka ameongeza kuwa kufuatia kuwepo kwa taarifa ya kutokuwa na mvua za kutosha  mwaka 2017 wananchi wamepata hofu ya mazao yao kukauka , hivyo Serikali imekusudia kuwatoa wananchi hofu hiyo kwa kuwahakikishia kuwa itawawezesha kupata maji kutoka Ziwa Victoria kwa ajili ya kumwagilia mashamba yao.

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa amesema Wilaya ya Busega ni wilaya ambayo wananchi wake wanaweza kulima kwa kipindi cha mwaka mzima kwa kuwa ina uhakika wa maji, hivyo Serikali imekusudia wananchi walime mpunga kwa misimu isiyopungua miwili kwa mwaka.

“Niko tayari kufanya ziara kila kijini hapa Busega ili nizungumze na wananchi, niwatoe hofu ya waliyo nayo juu ya mazao yao kukauka kutokana na kukosa mvua, maana Serikali itawapelekea maji” amesema Mtaka.

Pamoja na kuwahakikishia wananchi upatikanaji wa maji Serikali ya Mkoa kwa kushiriakiana na Wizara ya Kilimo,Mifugo na Uvuvi itawasaidia wananchi kupata mbegu bora ya mpunga ambayo itawawezesha kupata mavuno mengi na bora kuanzia gunia 35 hadi 40 za mpunga kwa heka moja.

Sambamba na hilo Mtaka amesema katika kutekeleza mkakati wa  Kilimo cha Umwagiliaji kama Kipaumbele; wananchi, serikali na wadau wengine wa kilimo kila mmoja atakuwa na wajibu na majukumu yake ili makakati huo utekelezwe kwa tija, ambapo amesema yapo majukumu yatakayofanywa na wananchi, mengine yatafanywa na Serikali (Halmashauri /Wizara ya Kilimo) , Viongozi na mengine yatatekelezwa na wadau.

Naye Katibu Tawala wa Mkoa huo, Ndg.Jumanne Sagini amesema Serikali ya Mkoa itaunda kikosi kazi cha Wahandisi wa Kilimo na Umwagiliaji kutoka Halmashauri zote za Mkoa huo, ambao watapaswa kuandaa mpango kazi na wajibu wa kila mdau katika utekelezaji wa mradi huo, kabla ya Januari Mosi, 2017.

Sagini amesema Wataalam hao kwa kushirikiana na watalaam wa Wilaya ya Busega watapaswa kukaa pamoja na kuandaa mpango kazi utakaobainisha mipango ya muda mrefu na ya muda mfupi, ambayo itapelekea kutekelezwa kwa mradi wa kilimo cha umwagiliaji kwa tija  na matokeo chanya kwa wananchi.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Busega Mhe. Mickness Mahela akizungumza kwa niaba ya Mwenyekiti,  amesema madiwani wote wa wilaya hiyo watatoa ushirikiano na kuhakikisha mpango huo wa kilimo cha umwagiliaji unafanikiwa kwa kiasi kikubwa na kuwasaidia wananchi.


Mkuu wa Mkoa anatarajia kuanza ziara ya siku sita wilayani Busega kuanzia Januari 03 hadi Januari 09, 2017 kwa lengo la kuzungumza na wananchi juu ya kilimo cha umwagiliaji kupitia mikutano ya hadhara, ambapo ameagiza taarifa ya mikutano hiyo zitolewe katika nyumba za ibada, kwenye mbao za matangazo za Vijiji na kata na gari la matangazo litumike ili wananchi wote wapate taarifa.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu (wa pili kushoto) akizungumza na Viongozi na Watendaji wa Halmashari ya Wilaya ya Busega (hawapo pichani) katika kikao maalum cha kujadili mkakati wa kilimo cha umwagiliaji wilayani humo, (wa tatu) Katibu Tawala Mkoa,Ndg. Jumanne Sagini.
Mkuu wa Wilaya ya Busega Mhe. Tano Mwera akizungumza na Viongozi na Watendaji wa Halmashari ya Wilaya ya Busega (hawapo pichani) katika kikao maalum cha kujadili mkakati wa kilimo cha umwagiliaji wilayani humo.
Baadhi ya Viongozi wa Mkoa wa Simiyu na Watendaji wa Wilaya ya Busega wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa, Mhe.Anthony Mtaka katika kikao maalum cha kujadili mkakati wa kilimo cha umwagiliaji wilayani Busega.

Katibu Tawala Msaidizi anayeshughulikia Huduma za Maji katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhandisi.Hatari Kapufi akichangia katika kikao maalum cha kujadili mkakati wa kilimo cha umwagiliaji wilayani Busega.

Afisa Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega akizungumza katika kikao maalum cha kujadili mkakati wa kilimo cha umwagiliaji wilayani humo kilichofanyika jana katika Ukumbi wa Silsosi.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka (wa pili kushoto)  akizungumza na Viongozi na Watendaji wa Halmashari ya Wilaya ya Busega (hawapo pichani) katika kikao maalum cha kujadili mkakati wa kilimo cha umwagiliaji wilayani humo.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!