Saturday, December 10, 2016

WANANCHI MKOANI SIMIYU WASHAURIWA KUZINGATIA UZAZI WA MPANGO


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka (kushoto) akikabidhi mifuko ya saruji kwa viongozi wa Kijiji cha Nyamikoma A na Kata ya  Kabita, ambapo alichangia mifuko 50 kwa shule ya msingi Fogofogo  na mifuko 50 kwa shule ya sekondari Kabita kwa ajili ya kuunga mkono ujenzi wa vyumba vya madarasa.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka  (wa pili kushoto) akizungumza na wananchi wa Kata ya Kabita Wilayani Busega (hawapo pichani) kwenye Mkutano wa Hadhara uliofanyika katika Shule ya Msingi Fogofogo, (kulia),Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega, Anderson Kabuko.
Mkuu wa wilaya ya Busega, Mhe.Tano Mwera (wa pili kushoto)akizungumza na wananchi wa Kata ya Kabita Wilayani Busega(hawapo pichani)  kwenye Mkutano wa Hadhara uliofanyika katika Shule ya Msingi Fogofogo.
Mwenyekiti wan Halmashauri ya Wilaya ya Busega, Mhe.Vumi Magoti  akizungumza na wananchi wa Kata ya Kabita Wilayani Busega(hawapo pichani)  kwenye Mkutano wa Hadhara uliofanyika katika Shule ya Msingi Fogofogo


Diwani wa Kata ya Kabita, Josiah Mgema akizungumza na wananchi wa Kata ya Kabita Wilayani Busega (hawapo pichani)  kwenye Mkutano wa Hadhara uliofanyika katika Shule ya Msingi Fogofogo, (wa pili kulia) Mkurugenzi wa Halmashauri ya Busega,Anderson Kabuko.

Baadhi ya wananchi wa Kata ya Kabita Wilayani Busega wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka  (hayupo pichani) kwenye Mkutano wa Hadhara uliofanyika katika Shule ya Msingi Fogofogo.
Na Stella Kalinga
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtaka amewashauri wananchi wa Mkoa huo kuzingatia uzazi wa mpango ili wawe na idadi ya watoto watakaoweza kuwahudumia vizuri kwa kuwapatia mahitaji yote muhimu.

Mtaka ameyasema hayo jana alipozungumza na wananchi wa Kata ya Kabita Wilayani Busega Mkoani humo kwenye  Mkutano wa hadhara uliofanyika katika Shule ya Msingi Fogofogo, kabla ya kuwakabidhi wananchi hao mifuko 100 ya saruji ikiwa ni kuwaunga mkono katika ujenzi wa vyumba vya madarasa.

Mkuu wa Mkoa ametoa kauli hiyo kufuatia taarifa ya Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Fogofogo, Nyabunyili Tolokoko kuonesha kuwa shule hiyo ina upungufu wa vyumba 21 vya madarasa kutokana na shule hiyo  kuwa na idadi ya  wanafunzi zaidi 1600.

Mtaka amesema Serikali imekuwa ikitoa elimu bila malipo kwa lengo la kuwapunguzia mzigo wananchi kwa kutoa michango isiyo ya lazima, lakini kama watakuwa na watoto wengi watakaoshindwa kuwapa huduma na mahitaji muhimu hawataona unafuu na umuhimu wa elimu bure kwa kuwa bado watakuwa na mzigo mzito.

“Ndugu zangu tuunge mkono kampeni ya Serikali ya Uzazi wa Mpango na Nyota ya Kijani, itatusaidia kupata watoto tutakaowasomesha, tutakaowalisha na  kuwahudumia vizuri. Serikali yetu inatoa elimu bure lakini fikiria mzazi kama mwakani utakuwa na watano, hata kama hutatoa ada na michango mingine utakuwa na mzigo kuwahudumia watoto hao ili kuhakikisha wanapata mahitaji yote muhimu” alisema Mtaka.

Aidha, Mtaka ametoa wito kwa  wananchi, viongozi wa dini na mashirika ya yasiyo ya kiserikali kushirikiana na Serikali katika ujenzi wa miundombinu ya shule ikiwa ni pamoja na vyumba vya madarasa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega Mhe. Vumi Magoti amewataka wananchi wa Wiaya hiyo kuchangia ujenzi wa vyumba vya madarasa kwa kadri itakavyokuwa imepangwa na Kamati za Maendeleo za Vijiji na Kata ili kukabiliana na upungufu uliopo kwa sasa.

Wakati huo huo Mkuu huyo wa Mkoa amewataka wanachi kulima mazao yanayostahilimili  ukame hususani mihogo,viazi na mtama na yale yanayokomaa kwa muda mfupi kwa kuwa hakutakuwa na mvua za kutosha, ambapo amesisitiza kila mtu ahakikishe analima ili apate chakula kwa sababu chakula cha msaada hakitakuwepo.

Sanjari na hilo amewataka wananchi  kulima pamba  na mazao ya mikunde hususani dengu , mbaazi, choroko na mbaazi   ambayo Serikali imewahakikishia wananchi soko la uhakika kutoka nchini India.
Mtaka ameongeza kuwa Viongozi wa wilaya ya Busega wahakikishe wanawasaidia na kuwasimamia wananchi katika kufanya shughuli za kilimo cha umwagiliaji na ufugajii wa samaki kwa kutumia vizmba kutokana na uwepo wa Ziwa victoria.


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu alifanya ziara wilayani Busega jana,  ambapo alizungumza na wananchi na kuchangia mifuko 100 ya saruji kwa ajili ya kuunga mkono ujenzi wa madarasa katika shule ya Msingi Fogofogo na Shule ya Sekondari Kabita zote za kata ya Kabita wilayani humo. 


0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!