Wednesday, March 7, 2018

MAAFISA MICHEZO WATAKIWA KUWASAIDIA VIJANA KUFIKIRI MICHEZO KATIKA MTAZAMO WA AJIRA NA BIASHARA


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka amewataka Maafisa Michezo na Walimu wa Michezo mkoani humo kuwasaidia Vijana wa Kitanzania kutoka kwenye nadharia ya kufikiri kuwa michezo ni afya, urafiki na  burudani tu ili waanze kufikiri michezo katika mtazamo wa biashara na ajira.

Mtaka ameyasema hayo wakati alipokuwa akifunga semina ya  kuwajengea uwezo Maafisa Michezo, Viongozi wa Vyama na Vilabu vya Michezo, makocha na walimu wa michezo shuleni, kwa lengo la  kuchochea maendeleo ya Michezo Mkoani Simiyu,  ambayo yametolewa na Dkt. Angela Daalmann  na Anja Henke ambao ni  Wataalam wa Michezo kutoka Jimbo la Hannover Nchini Ujerumani.

“Tumeleta mafunzo haya tukiamini kuwa Maafisa Michezo wote ndani ya Mkoa wa Simiyu watakuwa na msaada mkubwa kwenye kuwaandaa vijana wa Kitanzania kutoka kwenye nadharia ya kusema michezo ni afya, michezo ni upendo, michezo ni burudani ; nataka Afisa Michezo akienda kwenye implementation(utekelezaji) vijana wa mkoa wa Simiyu waanze kujenga vichwani mwao kuwa michezo ni ajira, michezo ni biashara” alisema Mtaka.

“Katika Dunia ya leo michezo ni biashara kubwa na ni ajira kubwa ya dunia ndiyo maana hapa mmefundishwa kuhusu miradi, hili suala la michezo ni burudani, michezo ni afya,  michezo ni urafiki na upendo libaki kama jambo la pili” alisisitiza

Ameongeza kuwa Maafisa Michezo pamoja na walimu wa michezo Mkoani Simiyu kupitia michezo ya UMITASHUMTA  na UMISETA wanapaswa kuwatambua watoto/vijana wenye vipaji na kuwaandaa kibiashara ili wajue kuwa vipaji vyao ni ajira zao za baadaye.

Aidha, amesema Serikali mkoani humo imedhamiria kutangaza utalii na kukuza uchumi kupitia sanaa, michezo na utamaduni na akabainisha kuwa Mkoa umeanza kutekeleza hilo kupitia  uanzishwaji wa Tamasha kubwa la michezo na utamaduni maarufu kama “Simiyu Festival” ambalo linafanyika kila mwaka na kwa mwaka 2018 litafanyika mapema mwezi Julai.

Naye Mtalaam wa Michezo kutoka Jimbo la Hannover Dkt. Angela Daalmann amesema kwamba wamehamasika kutoa mafunzo kwa maafisa, viongozi na walimu wa michezo mkoani Simiyu ikiwa ni mara ya pili sasa, kutokana na utayari wa viongozi na watalaam mkoani humo katika kuleta mapinduzi kwenye sekta ya michezo.

Afisa Michezo wa Mkoa wa Simiyu, Bw.Emmanuel Athanas amesema mafunzo hayo yataamsha ari na hamasa ya michezo kwa Maafisa Michezo na Walimu wa Michezo mkoani humo na kuwasaidia katika kuibua miradi mbalimbali itakayohusianishwa na michezo (sports projects)  sambamba na kuwatafuta wadau mbalimbali kuwezesha miradi hiyo.

Naye Afisa Michezo wilaya ya Meatu, Bw. Hassan Sengulo amesema mafunzo hayo yamewasaidia kutambua namna sahihi ya kupata fedha kwa ajili ya uendeshaji wa michezo,  hivyo watayatumia kuwaelimisha Walimu wa Michezo na Viongozi wa Vyama na Vilabu  vya Michezo namna ya kutatua changamoto ya ukosefu wa fedha za kuendeshea michezo.

Semina hii ilijumuisha jumla ya washiriki 27 kutoka Halmashauri zote sita za Mkoa wa Simiyu na baadaye ikafuatiwa na Bonanza la michezo kwa wanafunzi wa baadhi ya shule za msingi kushiriki mchezo wa riadha,  ambapo wanafunzi walipata nafasi ya kukimbia mbio za mita 100, mita 400 na mita 1500 katika Uwanja wa Shule ya Msingi Somanda Mjini Bariadi.

MWISHO
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka akizungumza katika semina ya  Maafisa Michezo, Baadhi ya walimu wa michezo na Viongozi wa Vyama vya Michezo mkoani humo  iliyofanyika Machi 06, 2018 Mjini Bariadi.
Mtalaam wa Michezo kutoka Jimbo la Hannover nchini Ujerumani  Dkt. Angela Daalmann akizungumza na  Maafisa Michezo, Viongozi wa Vyama na Vilabu vya Michezo, makocha na walimu wa michezo shuleni (hawapo pichani) mkoani Simiyu katika Semina iliyofanyika Machi 06, 2018 Mjini Bariadi.
Baadhi ya Maafisa Michezo, Viongozi wa Vyama na Vilabu vya Michezo, makocha na walimu wa michezo shuleni mkoani Simiyu wakimsikiliza Mtalaam wa Michezo kutoka Jimbo la Hannover nchini Ujerumani Dkt. Angela Daalmann katika Semina iliyofanyika Machi 06, 2018 Mjini Bariadi.
Baadhi ya Maafisa Michezo, Viongozi wa Vyama na Vilabu vya Michezo, makocha na walimu wa michezo shuleni mkoani Simiyu wakimsikiliza Mtalaam wa Michezo kutoka Jimbo la Hannover nchini Ujerumani Dkt. Angela Daalmann katika Semina iliyofanyika Machi 06, 2018 Mjini Bariadi.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka (kushoto) akiteta jambo na Mtalaam wa Michezo kutoka Jimbo la Hannover nchini Ujerumani Dkt. Angela Daalmann katika Semina ya Maafisa Michezo, Viongozi wa Vyama na Vilabu vya Michezo, makocha na walimu wa michezo shuleni mkoani Simiyu iliyofanyika Machi 06, 2018 Mjini Bariadi.
Baadhi ya Wanafunzi wa kike kutoka Shule ya Msingi Somanda A na Somanda B wakishiriki  mbio za mita 100 katika Bonanza la Michezo lililofanyika katika viwanja vya shule hiyo Machi 06, 2018 Mjini Bariadi.
Baadhi ya Wanafunzi wa kiume kutoka Shule ya Msingi Somanda A na Somanda B wakishiriki mbio za mita 400 katika Bonanza la Michezo lililofanyika katika viwanja vya shule hiyo Machi 06, 2018 Mjini Bariadi.
Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Msingi Somanda B wakitoa burudani ya ngoma ya asili ya kabila la Wasukuma katika Bonanza la Michezo lililofanyika katika viwanja vya shule hiyo Machi 06, 2018 Mjini Bariadi.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka(wa tatu kulia mbele) akiwa katika picha ya pamoja washiriki wa Semina kuwajengea uwezo Maafisa Michezo, Viongozi wa Vyama na Vilabu vya Michezo, makocha na walimu wa michezo shuleni mkoani humo pamoja na Dkt. Angela Daalmann  na Anja Henke ambao ni  Wataalam wa Michezo kutoka Jimbo la Hannover Nchini Ujerumani.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka(wa pili kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Wataalam wa Michezo kutoka Jimbo la Hannover nchini Ujerumani Dkt. Angela Daalmann(wa pili kushoto) na Anja Henke(kulia) mara baada ya kukamilika kwa semina kwa Viongozi, Maafisa na walimu wa Michezo mkoani humo (kushoto ) Mkuu wa Wilaya ya Busega, Mhe.Tano Mwera.
Afisa Michezo wa Mkoa wa Simiyu, Bw.Emmanuel  Athanas akifafanua jambo katika semina ya  kuwajengea uwezo Maafisa Michezo, Viongozi wa Vyama na Vilabu vya Michezo, makocha na walimu wa michezo mkoani humo iliyofanyika Machi 06, 2018 Mjini Bariadi.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!