Thursday, March 8, 2018

WANAWAKE WATAKIWA KUWALINDA WATOTO WA KIKE DHIDI YA MIMBA ZA UTOTONI


Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe.Festo Kiswaga ametoa wito kwa wanawake  wote Mkoani Simiyu kuwa mstari wa mbele katika kuwalinda watoto wa kike na kuhakikisha hawakatishwi masomo kwa sababu ya kupewa mimba wakiwa (katika umri mdogo) shuleni na badala yake wamalize masomo ili watimize ndoto zao.

Kiswaga ameyasema hayo leo wakati alipokuwa akizungumza na wanawake wa Mkoa wa Simiyu kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa huo, Mhe.Anthony Mtaka,  katika Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, yaliyofanyika Kimkoa katika Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi Mjini hapo.

Amesema Serikali ya awamu ya tano imetoa fursa kwa watoto wote kupata elimu bila malipo hivyo wazazi hususani wanawake (wakinamama) wanapaswa kutimiza wajibu wao katika kuhakikisha wanawasaidia watoto wao ikiwa ni pamoja na kufuatilia mienendo yao na kuwaonya wanapoenda kinyume  ili waweze kutimiza ndoto zao.

“Endapo mama kwenye familia atatimiza wajibu wake wa kumwangalia na kumwonya mtoto wa kike kuachana na vitendo vitakavyopelekea kupata mimba,  huyo mtoto atakuwa salama; kwa hiyo wakinamama timizeni wajibu wenu wa kuhakikisha mnawalinda watoto wa kike kama walivyofanya wazazi wetu zamani ili waweze kumaliza shule salama” alisema Kiswaga.

Ameongeza kuwa  wazazi wanapaswa kutoa ushirikiano kwa Serikali katika kuwafichua wanaume wote waliowapa mimba wanafunzi wa kike na kuhakikisha wanafikishwa katika vyombo vya dola ili waweze kuchukuliwa hatua badala ya kuwa upande wa wahalifu hao na kuwatetea.

Katika hatua nyingine Kiswaga ameziagiza Halmashauri zote mkoani Simiyu kuhakikisha kwamba zinatekeleza maagizo ya Serikali katika kutenga asilimia 10 kwa ajili ya wanawake na vijana na kuzitoa kama ilivyokusudiwa ili kuyasaidia makundi hayo kupata mitaji kwa ajili ya kuendeshea shughuli mbalimbali  za kuwaingizia kipato.

Aidha, ametoa wito kwa wanawake wa Mkoa wa Simiyu kuunga mkono juhudi za Serikali Mkoani humo katika uanzishwaji wa viwanda vidogo ili kutekeleza kwa vitendo Mkakati wa  Mkoa wa “Wilaya Moja Bidhaa Moja”, kwa lengo la kuwezesha kujitegemea kiuchumi na kuondokana na utegemezi kwa wanaume.

Awali akimkaribisha mgeni rasmi Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake (UWT) Mkoa wa Simiyu Mariam Manyangu amewataka wanawake wa Mkoa huo kufanya kazi kwa bidii na  kujiamini katika majukumu yao ya kila siku.

Akizungumza kwa niaba ya wanawake wa Mkoa wa Simiyu, Mwenyekiti wa Maandalizi ya Siku ya Wanawake mkoani SIMIYU, Mwl. Rachel Ernest amesema Wanawake Mkoani humo wanalaani vitendo vya baadhi ya watu katika jamii kuendelea kumtumia mtoto wa kike kama kitega uchumi kwa tamaa ya kupata  ng’ombe, hivyo kumkatisha masomo ili aolewe na kushindwa kutimiza  ndoto za maisha yake .

Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani kwa mwaka 2018 yameadhimishwa chini ya Kauli Mbiu isemayo “Kuelekea Uchumi wa Viwanda, Tuelimishe Usawa wa kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake Vijijini”,   ambapo wanawake mkoani Simiyu walianza maadhimisho hayo kwa kwenda kuwaona wagonjwa(wanawake na watoto) katika Hospitali Teule ya Mkoa wa Simiyu na kutoa misaada mbalimbali ikiwemo sabuni na vinywaji.

Baadhi ya wanawake wa Mkoa wa Simiyu wakiwa katika maandamano kuelekea Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi katika Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika Kimkoa Mjini Bariadi.

Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe.Festo Kiswaga akizungumza na wanawake wa Mkoa wa Simiyu (Akimwakilisha Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Anthony Mtaka) katika Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, yaliyofanyika Kimkoa Mjini Bariadi katika Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi.

Kaimu Mkurugenzi wa Mji wa Bariadi, Bi. Suzana Sabuni akizungumza na wanawake wa Mkoa wa Simiyu, katika Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, yaliyofanyika Kimkoa Mjini Bariadi katika Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi.

Baadhi ya wanawake wa Mkoa wa Simiyu wakiwa katika maandamano kuelekea Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi katika Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika Kimkoa Mjini Bariadi.
Bi. Ruth Seni Mjasiriamali kutoka MCSEKA Group Company Mjini Bariadi,  wanaojishughulisha na utengenezaji wa sabuni aina zote akitoa maelezo juu ya bidhaa hizo kwa Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga(hayupo pichani)  alipotembelea banda lao maonesho wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika Kimkoa Mjini Bariadi.
Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga (katikati) akizungumza na wajasiriamali wa Kikundi cha CHIKOMO cha Mjini Bariadi Mkoani Simiyu mara baada ya kutembelea banda lao la maonesho wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika Kimkoa Mjini hapo.


Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga (kushoto) akimsikiliza Mjasiriamali Bi. Wilielimina Edward mara baada ya kuona bidhaa alizozitengeneza  baada ya kutembelea banda lake la maonesho wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Mkoani Simiyu yaliyofanyika Kimkoa Mjini Bariadi.
Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Simiyu Mhe. Mariam Manyangu akizungumza na wanawake wa Mkoa wa Simiyu, katika Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, yaliyofanyika Kimkoa Mjini Bariadi katika Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi.
Msanii Elizabeth Maliganya akitoa burudani pamoja na wasanii wengine kutoka Simiyu Band wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Mkoani Simiyu yaliyofanyika Kimkoa Mjini Bariadi.
Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambayo Mkoani Simiyu yameadhmisha katika Halmashauri ya Mji wa Bariadi, Bibi. Rachel Ernest akisoma risala kwa niaba ya wanawake wa Mkoa wa Simiyu wakati wa Maadhimisho hayo .

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!