Wednesday, February 26, 2020

KIWANDA CHA VIFAA TIBA SIMIYU KUIPUNGUZIA MSD UAGIZAJI WA VIFAA TIBA NJE YA NCHI


Kukamilika kwa kiwanda cha vifaa tiba vitokanavyo na zao la pamba kinachotarajiwa kujengwa Bariadi mkoani Simiyu kutaipunguzia Bohari ya dawa (MSD) uagizaji wa bidhaa hizo toka nje ya nchi kwa asilimia 38.3.

Hayo yamebainishwa na Waziri wa Nchi ofisi ya Waziri Mkuu, Uwekezaji, Mhe. Angella Kairuki kwenye mkutano wa mashauriano kati ya Serikali, Wawekezaji na Wafanyabiashara mkoani Simiyu uliofanyika Februari 25, 2020 Mjini Bariadi, kwa lengo la kujadili changamoto mbalimbali za biashara na uwekezaji na ufumbuzi wake.

“MSD imekuwa ikitumia zaidi ya shilingi bilioni 147 kununua dawa na vifaa tiba zaidi ya 19 kutoka nje ya nchi, tunaamini kwa kuanzisha kiwanda cha vifaa tiba vitokanavyo na pamba  na bidhaa zingine 19 zikiwemo nguo za madaktari na wauguzi tunaamini tutaiondolea MSD uagizaji wa bidha hizo kwa asilimia 38.3,”alisema Mhe. Kairuki.

Amesema kiwanda hicho kitasaidia kufikia azma ya Serikali ya kuongezea thamani zao la pamba badala ya kuisafirisha, ambapo kwa sasa zaidi ya asilimia 70 ya pamba inasafirishwa nje ya nchi.

Aidha, Mhe Kairuki ametoa wito kwa wawekezaji na Wafanyabiashara mkoani Simiyu kutumia fursa za uwekezaji zilizopo katika viwanda vya ngozi, nyama,vyakula vya mifugo, viwanda vya mafuta ya kula; huku akiwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kujenga mazingira wezeshi kwa biashara na uwekezaji, kupunguza kero ya utitiri wa kodi na tozo mbalimbali, kupunguza mamlaka za udhibiti wa kibiashara na kuondoa muingiliano wa mamlaka hizo.

Katika hatua nyingine Mhe. Kairuki ameupongeza uongozi wa mkoa wa Simiyu kwa Simiyu kuwa mkoa wa kwanza kuzindua mwongozo wa uwekezaji nchini mwaka 2017 pamoja na kutekeleza mkakati wa Wilaya Moja Bidhaa Moja(One District One Product -ODOP).

Kwa upande wa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji amesema  zabuni ya kiwanda cha vifaa tiba vitokanavyo na pamba  kinachotarajiwa kujengwa Mkoani Simiyu imeshatangazwa na jiwe la msingi linatarajiwa kuwekwa mwezi Mei, 2020.

Naye mkuu wa mkoa huo, Mhe. Anthony Mtaka amesema ni vema Bodi ya Pamba itoe viuadudu kwa wakulima wa pamba kwa wakati ili kudhibiti madhara yanayoweza kusababishwa na magonjwa huku akisisitiza bei ya pamba kupangwa mapema kabla ya msimu.

Aidha, Mtaka ameomba Waziri anayeshughulikia Uwekezaji kuona namna ya kuwasaidia wafanyabiashara na wawekezaji katika changamoto ya kufungiwa biashara zao, ambapo baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakifungiwa biashara na viongozi au watendaji kutoka katika Taasisi au Ofisi mbalimbali za Serikali.

Naye Katibu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara mkoa wa Simiyu, Bw. Zebedayo King ameomba mabaraza ya biashara yafanyike  kwa wakati  ili wafanyabiashara waendelee kupata fursa ya kukutana na viongozi wa Serikali na Taasisi za Fedha na kujadili namna ya kutatua changamoto mbalimbali katika biashara na uwekezaji ikiwemo masuala ya kodi, kulipwa madeni yao kwa wakati pamoja na mazingira ya uwekezaji na biashara kwa ujumla.

Awali akiwasilisha changamoto zinazowakabili wakulima wa pamba Mwenyekiti wa chama cha Ushirika Mkoa wa Simiyu(SIMCU) Charles Madata amesema baadhi ya wakulima hawajalipwa fedha zao na dawa hazitolewi kwa wakati, hivyo akaomba wakulima wasaidiwe kutatua changamoto hizo ili waone faida ya kilimo cha zao hilo.

Mkutano wa mashauriano kati ya Serikali, Wawekezaji na Wafanyabiashara mkoani Simiyu uliwahusisha viongozi wa Serikali wakiongozwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu uwekezaji, Mhe. Angella Kairuki, Manaibu Waziri kutoka Wizara ya Fedha na Mipango, Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Ardhi na Makazi, Wizara ya Maliasili na Utalii, Ofisi ya Rais Muungano na Mazingira, Wizara ya Madini, Wizara ya ujenzi, Viongozi wa Mkoa, Viongozi wa Jumuiya za Wafanyabiashara, wakulima na Wajasiriamali
MWISHO.

 Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Uwekezaji, Mhe. Angella Kairuki akiteta jambo na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka katika Mkutano wa mashauriano kati ya Serikali, Wawekezaji na Wafanyabiashara mkoani Simiyu uliofanyika Februari 25, 2020 Mjini Bariadi.


 Baadhi ya Wafanyabiashara wa Mkoa wa Simiyu wakifuatilia hoja na maelezo kutoka kwa Viongozi wa Serikali wakati wa Mkutano wa mashauriano kati ya Serikali, Wawekezaji na Wafanyabiashara mkoani Simiyu uliofanyika Februari 25, 2020 Mjini Bariadi.


 Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyabiashara mkoa wa Simiyu, Bw. John Sabo akichangia hoja katika Mkutano wa mashauriano kati ya Serikali, Wawekezaji na Wafanyabiashara mkoani Simiyu uliofanyika Februari 25, 2020 Mjini Bariadi.


 Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akizungumza katika Mkutano wa mashauriano kati ya Serikali, Wawekezaji na Wafanyabiashara mkoani Simiyu uliofanyika Februari 25, 2020 Mjini Bariadi.


 Meneja Masoko wa Busega Mazao Company Ltd, Bw. Innocent Mafuru akichangia hoja katika Mkutano wa mashauriano kati ya Serikali, Wawekezaji na Wafanyabiashara mkoani Simiyu uliofanyika Februari 25, 2020 Mjini Bariadi.


 NaibuWaziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji akitoa ufafanuzi wa changamoto mbalimbali zilizowasilishwa na wawekezaji na wafanyabiashara wa Mkoa wa Simiyu, katika Mkutano wa mashauriano kati ya Serikali, Wawekezaji na Wafanyabiashara mkoani Simiyu uliofanyika Februari 25, 2020 Mjini Bariadi.


 NaibuWaziri wa Viwanda na biashara, Eng. Stella Manyanya  akitoa ufafanuzi wa changamoto mbalimbali zilizowasilishwa na wawekezaji na wafanyabiashara wa Mkoa wa Simiyu, katika Mkutano wa mashauriano kati ya Serikali, Wawekezaji na Wafanyabiashara mkoani Simiyu uliofanyika Februari 25, 2020 Mjini Bariadi.


Mwenyekiti wa Chama cha Ushirika Mkoa wa Simiyu, Bw. Charles Madata akiwasilisha changamoto za wakulima wa pamba katika Mkutano wa mashauriano kati ya Serikali, Wawekezaji na Wafanyabiashara mkoani Simiyu uliofanyika Februari 25, 2020 Mjini Bariadi.


0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!