Monday, June 14, 2021

KATIBU TAWALA MKOA WA SIMIYU BI. PRISCA KAYOMBO AFUNGUA MICHEZO YA UMISSETA MKOA


Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu Bi. Prisca Kayombo, tarehe 11/06/2021 alifungua rasmi,michezo ya UMISSETA Mkoa, michezo ambayo ilikuwa ikifanyika katika shule ya Sekondari ya Wasichana Maswa.

Akizungumza Kaimu Afisa Elimu Mkoa Bwn.Charles Maganga alisema mashindano ngazi ya Mkoa yameanza leo 11/6/21 na yatakamilika 13/6/21 kwa kuunda timu ya Mkoa. Kauli mbiu ya Mashindano haya ya mwaka 2021 ni : “Michezo,Sanaa na  Taaluma Kwa Maendeleo ya Uchumi wa Viwanda”.

Mashindano haya yana jumla ya washiriki 679, kati yao wanafunzi 600,waalimu 61, madaktari 2 na viongozi 16.Washiriki hawa ni kutoka Halmashauri zote za Mkoa.Idadi ya Michezo inayoshindaniwa ni saba na michezo 4 kati ya hiyo inahusisha wavulana na wasichana.
Michezo hiyo ni pamoja na Riadha, Mpira wa Miguu, Mpira wa Wavu, Mpira wa Mikono,Mpira wa kikapu, Mpira wa Netiboli na fani za ngoma na kwaya.

Ili kuendesha mashindano kwa ufanisi tumeunda kamati ya ndhamu, afya, usafi na mazingira. Pia tumeunda kamati za michezo.Kamati hizi zina jukumu la kusimamia uendeshaji wa michezo kwa kuzingatia sheria na kanuni za michezo husika.Na wajumbe wa kamati hizi ni waalimu wa michezo husika.Hali ya kambi ni nzuri, hatujakumbanana changamoto
yeyote, wanamichezo wana ari kubwa ya kishindana katika hali ya utulivu, upendo

Aidha Mkurugenzi wa Halmashauri ya Maswa Dkt. Fredrick Sagamiko, alimkaribisha Mgeni rasmi Bi. Kayombo na kumhakikishia kuwa hali ya Maswa ni shwari hivyo wanamichezo wasiwe na wasiwasi kabisa.

Katibu Tawala, Bi. Kayombo  ambaye  alikuwa mgeni rasmi alikuwa na haya ya kusema;
napenda kuwashukuru  Wazazi/ walezi kwa kuwaruhusu wanafunzi kushiriki michezo.Pia niwashukuru wadau mbalimbali kwa kuwezesha maandalizi mazuri.Niwapongeze wanamichezo  wote kwa kuunda timu za halmashauri, ni matumaini yangu kuwa vipaji mlivyo vionyesha vitaendelea kuonekana katika mashindano haya yatakayofanyika katika ngazi ya Taifa, Mkoani Mtwara kuanzia 20/6/2021 - 03/7/2021.

Kama ilivyo  kauli mbiu ya mwaka. huu Michezo na Sanaa ni sehemu ya Taaluma na maendeleo ya Elimu. Michezo ni muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu na imekuwa chimbuko kubwa la kuzalisha na kukuza wanamichezo mbalimbali  wanaounda timu za Taifa. Lengo la michezo hii ni kujenga na kuimarisha umoja, udugu, upendo, mshikamano, hali ya kujiamini, kukuza taaluma na utimamu wa akili kwa wanafunzi.

Tafiti mbalimbali  zimebainisha kuwa michezo huchangia katika kuimarisha ushiriki wa wanafunzi kitaaluma kwa kupunguza utoro na kuimarisha afya za wanafunzi.Michezo imesaidia kujenga mshikamano kimkoa kwa kuwaleta pamoja wadau wa elimu na michezo.

Nitoe  wito kwa wanafunzi wote watakaochaguliwa kuunda timu ya Mkoa, mzingatie kanuni za michezo,  tumieni vipaji vyenu kuhakikisha kuwa  tunapata ushindi. Tumieni fursa hiyo kuutangaza mkoa wa simiyu.Waalimu  chagueni wanafunzi na sio mamluki kwani itakuwa aibu kwa mkoa.Ikiwa mtawela Mamluki.

Changamoto ya viwanja vya michezo, natoa maelekezo maafisa michezo, kuendelea  kupima viwanja vyote vinavyohitajika kwenye maeneo ya shule ili wakuu wa shule waweze kusimamia utengenezaji  wa viwanda hivyo kwa kushirikiana na wanafunzi na vitumike  wakati wote,tusisubiri tu kipindi cha michezo hii ya UMISSETA.

 Ili kufanya vizuri zaidi katika Sekta ya Michezo na Elimu kwa ujumla ni vyema tukazingatia yafuatayo: imarisheni nidhamu yenu katika nyanja zote,nidhamu na maadili ya waalimu na wanafunzi viendelee kudumishwa,Wanafunzi/ wanamichezo sikilizeni na kuzingatia maelekezo, mbinu na mikakati mbalimbali mtakayopewa na waalimu wenu.Watoto waende salama na kurudi salama, nidhamu na maadili vidumishwe, mahusiano kati ya waalimu na watoto, yawe ya mzazi na mtoto.Nami nawatuma mkaniletee ushindi.

Michezo sio uadui hivyo watakaoteuliwa na wasioteuliwa wasilete uadui. Maendeleo yetu hutokana na kuweka  bidii katika michezo.

Akitoa neno la shukrani Bi.Line Chanafi, alisema mgeni rasmi kwa niaba ya wenzangu nikuahidi ushirikiano. Sisi tupo vizuri na tumeanza  vizuri na hatuna mamluki, tuna wanafunzi/ wanamichezo halali, tutafanya yote uliyotuagiza na hasa nidhamu.

MWISHO























0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!