Monday, January 9, 2017

RC SIMIYU ATOA MIEZI MITATU KWA HALMASHAURI YA BUSEGA KUJENGA MACHINJIO NYASHIMO


Na Stella Kalinga
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe.Anthony Mtaka ametoa miezi mitatu kwa Halmashauri ya Wilaya ya Busega kujenga machinjio katika Kata ya Nyashimo ambayo ni makao makuu ya wilaya hiyo.

Mtaka ameyasema hayo katika mkutano wa Hadhara uliofanyika Kijiji cha Bulima kata ya Nyashimo kwa lengo la kuhamasisha mpango wa Kilimo cha Umwagiliaji pamoja na kisikiliza kero za Wananchi na kuwapatia ufumbuzi wakati wa ziara yake wilayani humo.

Akijibu kero iliyowasilishwa na Deusdedit Mushungu mkazi wa Nyashimo ambaye alieleza kuwa wananchi wamekuwa wakitozwa ushuru wakati machinjio hayakidhi viwango, Mtaka amesema kwa kuwa Halmashauri inakusanya ushuru kutoka kwa wafanyabiashara wa nyama inapaswa kuboresha huduma ya machinjio na itakaposhindwa isiwadai wafanyabiashara hao ushuru.

“ Idara ya mifugo hakikisheni mnajenga machinjio ya Nyashimo, nawapa miezi mitatu kuanzia sasa mkishindwa nitafuta ushuru kwa wananchi kwa kuwa mtakuwa mmeshindwa kutimiza wajibu wenu kama Halmashauri” alisema Mtaka.

Afisa Mifugo wa Halmashauri ya Wilaya Busega, Ndg. Albert Francis amesema Halmashauri imetenga eneo kwa ajili ya kujenga machinjio ya kisasa katika kijiji cha Nyang’anga kwa kuwa yaliyopo kwa sasa yamejengwa karibu na makazi ya watu.

Aidha, Afisa Mifugo huyo aliongeza kuwa machinjio hayo kwa mwaka 2015/2016 yalikadiriwa kuchangia shilingi 300,000/= kwa mwezi katika mapato ya Halmashauri na  mwaka 2016/2017 yamekadiriwa kuchangia shilingi 600,000/=  mapato ambayo hayajafikia kutokana na idadi ndogo ya wachinjaji(wafanyabiashara wa nyama).

Wakati huo huo Mkuu huyo wa Mkoa akijibu ombi la wananchi wengi wa Nyashimo la kuletewa chakula cha bei nafuu ili kukabiliana na upungufu wa chakula inayotokana na baadhi ya mazao kukaua mashambani kutokana kukosa mvua za kutosha, amesema Serikali italifanyia kazi na kuona namna ya kuwasaidia.

Mtaka amesema ufumbuzi wa kudumu wa tatizo la upungufu wa chakula ni wananchi wa Wilaya ya Busega  kuhamasika na kuanza kutekeleza Mpango wa Kilimo cha umwagiliaji unaotarajiwa kuanza kutekelezwa mapema mwaka 2017 wilayani humo kama kipaumbele, kwa kuwa kuna uhakika wa maji ya Ziwa Victoria.

Mtaka amesema endapo wananchi wataonesha utayari wa kutekeleza mpango huu Serikali kwa kushirikiana na wadau wengine itafanya  utaratibu wa kuwawezesha kwenye miundombinu ya umwagiliaji na pembejeo za kilimo zikiwemo mbegu bora na mbolea kwa kadri watakavyokubaliana.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu yuko katika ziara ya siku 6 wilayani Busega ambapo anazungumza na wananchi kuelimisha na kuhamasisha kuhusu mpango wa kilimo cha umwagiliaji na kujibu kero mbalimbali za wananchi wa wilaya hiyo.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu akizungumza na wananchi wa Kata ya Nyashimo akizungumza na katika mkutano wa hadhara uliofanyika kijiji cha Bulima kwa lengo la kuhamasisha utekelezaji wa mpango wa kilimo cha umwagiliaji wilayani humo na kusikiliza na kujibu kero mbalimbali za wananchi.
Mkuu wa Wilaya ya Busega Mhe.Tano Mwera akizungumza na wananchi wa Kata ya Nyashimo aki katika mkutano wa hadhara uliofanyika kijiji cha Bulima kwa lengo la kuhamasisha utekelezaji wa mpango wa kilimo cha umwagiliaji wilayani humo na kusikiliza na kujibu kero mbalimbali za wananchi.
Diwani wa Kata ya Nyashimo, Mhe.Mickness Mahela akizungumza na wananchi wa kata hiyo katika mkutano wa hadhara uliofanyika kijiji cha Bulima kwa lengo la kuhamasisha utekelezaji wa mpango wa kilimo cha umwagiliaji wilayani humo na kusikiliza na kujibu kero mbalimbali za wananchi.
Baadhi ya viongozi na maafisa waandamizi wa wilaya ya Busega na Mkoa w Simiyu wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu,Mhe.Anthony Mtaka katika mkutano wa hadhara uliofanyika kijiji cha Bulima kata yaNyashimo wilayani Busega,  kwa lengo la kuhamasisha utekelezaji wa mpango wa kilimo cha umwagiliaji wilayani humo na kusikiliza na kujibu kero mbalimbali za wananchi.
Baadhi ya viongozi na maafisa waandamizi wa wilaya ya Busega na Mkoa w Simiyu wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu,Mhe.Anthony Mtaka katika mkutano wa hadhara uliofanyika kijiji cha Bulima kata yaNyashimo wilayani Busega,  kwa lengo la kuhamasisha utekelezaji wa mpango wa kilimo cha umwagiliaji wilayani humo na kusikiliza na kujibu kero mbalimbali za wananchi.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!