Thursday, October 22, 2020

KIDATO CHA NNE SIMIYU KUANZA KAMBI ZA KITAALUMA OKTOBA 30

 Wanafunzi wa Kidato cha nne mkoani Simiyu wanatarajia kuanza kambi za kitaaluma tarehe 30 Oktoba 2020, kwa ajili ya kujiandaa na mtihani wa Taifa unaotarajiwa kufanyika kuanzia tarehe 23 Novemba 2020 hadi tarehe  11 Desemba, 2020. 

Taarifa hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka wakati akizungumza na Maafisa Elimu, wakuu wa shule na baadhi ya wanafunzi wa kidato cha nne baada ya kufunga kikao maalum cha kutangaza na kutathmini  matokeo ya Mtihani wa Utimilifu (Mock)  kilichofanyika jana Mjini Bariadi. 

Mtaka amesema wanafunzi wote wa kidato cha nne waliopata daraja la I (division one) daraja la IV (division four), daraja la sifuri (division zero) katika Mtihani wa Mock mwaka 2020 na wale wanaotoka katika shule zenye watahiniwa  pungufu ya 30 Serikali imeandaa utaratibu kwa ajili yao, hivyo tarehe 30 Oktoba wanapaswa kufika katika vituo vilivyoandaliwa ambavyo ni Shule ya Sekondari Simiyu na Shule ya Msingi Ndekeja. 

“Mwaka huu kumekuwa na majanga  mengi ya moto, majanga ya moto dawa yake si kufunga kambi za shule na ndiyo maana shule za bweni hazijafungwa, tumekuwa na utaratibu wa kambi za kitaaluma kwa watoto wote wa kidato cha nne wa Mkoa wa Simiyu wa shule za Serikali; maelekezo yangu, kambi za kitaaluma kwenye maandalizi ya kidato cha nne zianze na ziendelee mpaka tutakapoanza mtihani wa Taifa,” alisema Mtaka. 

Mtaka amezitaka Kamati za Ulinzi na Usalama za wilaya zote mkoani Simiyu kuendelea kuchukua tahadhari na kinga zote za majanga ya moto, huku akibainisha kuwa elimu ya tahadhari ya majanga ya moto imeshatolewa katika shule zote na vifaa vya kuzimia moto vimefungwa  katika baadhi ya shule ikiwemo shule ya Sekondari Simiyu ambacho ni kituo cha kambi hizo.

 

Akizungumzia suala la motisha kwa walimu na wanafunzi watakaofanya vizuri katika mtihani wa Taifa wa Kidato cha nne amesema mwalimu atapewa shilingi 30,000/= kwa kila alama A itakayopatikana kwenye somo lake na shilingi 10,000/= kwa alama B.

Ameongeza kuwa mwanafunzi atakayepata daraja la kwanza pointi saba atapewa shilingi 1,000,000/= na ikiwa atakuwa miongoni mwa wanafunzi kumi bora Kitaifa ataongezewa shilingi 1,000,000/=na kumfanya apate shilingi 2,000,000/=, ambapo amesisitiza kuwa mwanafunzi wa kike atakayefanya vizuri kuliko wenzake wote atapewa shilingi 500,000/= na ikitokea msichana aliyeongoza amepata daraja la kwanza pointi saba atapewa shilingi 1,500,000/=

Shule ya Serikali ya Sekondari ya Mkoa wa Simiyu itakayoingia katika shule 10 bora Kitaifa itapewa zawadi ya shilingi 5,000,000/= huku akiahidi kuwapeleka walimu wote ambao Halmashauri yao itafanya vizuri na kuingia katika nafasi kumi bora Kitaifa kwenda kufanya utalii wa ndani katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.

Kwa upande wake Afisa Elimu wa Mkoa wa Simiyu Mw. Ernest Hinju amesema katika matokeo ya mtihani wa Taifa wa kidato cha nne mwaka 2019 Simiyu ilishika nafasi ya tano Kitaifa na matarajio ya mwaka huu ni kushika nafasi ya kwanza Kitaifa, huku akibainisha kuwa maandalizi yanaendelea vizuri na wazazi wamehamasika kuwachangia wanafunzi chakula.

Kwa upande wao walimu na wanafunzi wameshukuru Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka kuruhusu kambi za kitaaluma kwa kuwa kambi hizo zimekuwa msaada sana kwa wanafunzi hususani wale ambao wanatoka katika mazingira magumu ambayo hawawezi kujisomea kwa uhuru.

“Awali tuliposikia kambi zimeahirishwa tulisononeka sana maana kambi zimekuwa msaada hasa kwa watoto wanaotoka katika mazingira magumu, hata walimu tunabadilishana utaalamu na mbinu za ufundishaji; tunamshukuru Mhe.RC kuruhusu kambi maana miaka ya nyuma Simiyu ilikuwa nyuma sana kwa ufaulu; lakini sasa hivi tumetoka huko tumepanda mfano matokeo ya kidato cha sita mwaka huu tumeshika nafasi ya tatu na kidato cha nne mwaka 2019 tulishika nafasi ya tano Kitaifa,” Mwl. Khamis Lubugwa.

“Kambi za kitaaluma zimekuwa na msaada sana hususani kwa watoto wa kike, tunapokuwa kambi tunapata muda mwingi wa kujisomea kuliko tunapokuwa nyumbani lakini vile vile tunapokuwa kambi inatusaidia kuepukana na vishawishi mbalimbali maana miongoni mwetu wako wanaotoka mbali, tumejisikia vizuri kufunguliwa kwa kambi na tunatarajia kufanya vizuri sana,” Nshoma Joseph mwanafunzi wa kidato cha nne shule ya sekondari Bariadi.

MWISHO

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akizungumza na baadhi ya Maafisa Elimu, wakuu wa shule na na baadhi ya wanafunzi wa kidato cha nne katika shule ya sekondari Bariadi baada ya kufunga kikao cha kutangaza na kutathmini  matokeo ya Mtihani wa Utimilifu (Mock)  kilichofanyika jana Mjini Bariadi.
Baadhi ya wanafunzi wa kidato cha nne katika Shule ya Sekondari Bariadi wakishangilia mara baada  ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akitangaza kuanza kwa kambi za kitaaluma kwa wanafunzi hao Oktoba 30, 2020 baada ya kufunga kikao cha kutangaza na kutathmini  matokeo ya Mtihani wa Utimilifu (Mock)  kilichofanyika jana Mjini Bariadi.

Baadhi ya wanafunzi, walimu, Maafisa Elimu, wakuu wa shule wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka (hayupo pichani)  baada ya kufunga kikao cha kutangaza na kutathmini  matokeo ya Mtihani wa Utimilifu (Mock)  kilichofanyika jana Mjini Bariadi.
Baadhi ya wanafunzi wa kidato cha nne katika Shule ya Sekondari Bariadi wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akitangaza kufunguliwa kwa kambi za kitaaluma kwa wanafunzi hao Oktoba 30, 2020 baada ya kufunga kikao cha kutangaza na kutathmini  matokeo ya Mtihani wa Utimilifu (Mock)  kilichofanyika jana Mjini Bariadi.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akizungumza na wanafunzi na walimu na Maafisa Elimu, wakuu wa shule na baadhi ya wanafunzi wa kidato cha nne baada ya kufunga kikao cha kutangaza na kutathmini  matokeo ya Mtihani wa Utimilifu (Mock)  kilichofanyika jana Mjini Bariadi.
Baadhi ya Makamu Wakurugenzi, Maafisa Elimu, wakuu wa shule wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka (hayupo pichani)  akitangaza kuanza kwa kambi za kitaaluma za kidato cha nne mwishoni mwa mwezi huu baada ya kufunga kikao cha kutangaza na kutathmini  matokeo ya Mtihani wa Utimilifu (Mock)  kilichofanyika jana Mjini Bariadi.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!