Sunday, January 6, 2019

DKT BASHIRU AWAONYA VIONGOZI WALIOANZA KUTAFUTA UBUNGE KABLA YA WAKATI


Katibu Mkuu wa Chama cha Mpinduzi (CCM) Taifa Dkt. Bashiru Ally amewaonya baadhi ya Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri, na Wakuu wa Taasisi na Mashirika ya Umma, ambao wameanza kukaa vikao kwa ajili ya kutafuta majimbo kabla ya wakati wa Chama hicho kutangaza mchakato wa kutafuta wagombea wapya wa ubunge na udiwani.

Dkt. Bashiru ameyasema hayo Januari 05, 2019 wakati akizungumza na viongozi na wanachama wa CCM pamoja na Viongozi na watendaji wa Serikali katika wilaya ya Bariadi na Itilima wakati akiwa katika ziara yake mkoani Simiyu.

Dk Bashiru amesema ikiwa viongozi hao wataendelea kufanya hivyo atawataja hadharani na akasisitiza kuwa ni vema wakaridhika na nafasi walizopewa na Rais wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwani kushindwa kufanya hivyo ni kumdharau aliyewateua.
“Wapo wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, Makatibu tawala wa mikoa, wakurugenzi wa halmashauri, na wakuu wa taasisi na mashirika ya umma, wameanza kukaa vikao kwa ajili ya kutafuta majimbo, CCM hatujatangaza mchakato wa kutafuta wabunge au madiwani wapya, uko wakati nitawatangaza hadharani, mridhike na nafasi zenu mlizopewa na Mhe. Rais” alisema
Katika hatua nyingine Dkt. Bashiru amesema kuelekea Uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika mwaka huu 2019 Viongozi wa CCM wajipange katika kuhakikisha viongozi wa Vijiji na Mitaa wanachaguliwa katika misingi ya demokrasia kwa kuzingatia sifa zao na si fedha zao(rushwa).
“ Katika mwaka huu wa kumuenzi Mwalimu Nyerere baada ya miaka 20 tunataka kufanya mchakato wa kusimamia uchaguzi uwe tofauti, wakati wa kuteua tuzingatie sifa na tuwapime viongozi kwa maisha yao na vitendo vyao......” alisema Dkt. Bashiru.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Mhe. Benson Kilangi ameishukuru Serikali ya awamu ya tano  kwa kutoa zaidi ya shilingi bilioni 26 katika kipindi cha miaka mitatu, kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya  maendeleo.
 Naye Mbunge wa Jimbo la Itilima Mhe.Njalu Silanga, ameishukuru Serikali kwa kuboresha miundombinu ya barabara ambapo amebainisha kuwa kupitia Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) barabara katika jimbo hilo zimetengenezwa zinapitika na zipo ambazo zinaendelea kufanyiwa matengenezo.
Naye Katibu wa CCM Mkoa, Bw. Donald Magesa  akitoa taarifa ya Chama, utekelezaji wa Ilani ya CCM mkoani humo umefanyika vizuri huku akisisitiza kuwa Viongozi wa Chama na Serikali wamejipanga kwa kushirikiana na wananchi kukamilisha maboma yaliyojengwa ili kila mwanafunzi aliyefaulu darasa la saba mwaka 2018 aweze kuanza kidato cha kwanza.
Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Dkt. Bashiru Ally yuko Mkoani Simiyu kuanzia Januari 05,2019 kwa ziara ya kikazi ya siku mbili yenye lengo la kukagua utekelezaji wa Ilani ya CCM mkoani humo.
MWISHO.
 Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Dkt. Bashiru Ally akizungumza na wanachama wa CCM na wananchi katika Mji mdogo wa Lamadi, mara baada ya kuwasili Mkoani Simiyu kwa ajili ya ziara yake ya kukagua utekelezaji wa Ilani ya CCM mkoani hapa Januari 05, 2019.

Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Dkt. Bashiru Ally(kulia) akiteta jambo na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Simiyu, Mhe. Enock Yakobo wakati akiwa katika ziara yake ya kukagua utekelezaji wa Ilani ya CCM mkoani hapa Januari 05, 2019.
 Baadhi ya viongozi wa CCM mkoa wa Simiyu wakimsikiliza Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Dkt. Bashiru Ally(hayupo pichani)  katika kikao chake na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi na Serikali  mkoani Simiyu kilichofanyika Mjini Bariadi Januari 05, 2019.
Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Dkt. Bashiru Ally(wa tano kulia) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya watumishi na viongozi wa Serikali wa Mkoa wa Simiyu mara baada ya k kikao chake na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi na Serikali  mkoani Simiyu kilichofanyika Mjini Bariadi Januari 05, 2019.
Kutoka kushoto Mbunge wa Maswa Mashariki, mhe. Stanslaus Nyongo, Mbunge wa Itilima, Mhe. Njalu Silanga, Mbunge wa Meatu, Mhe. Salum Khamis na Mbunge wa Maswa Magharibi, Mhe. Mashimba Ndaki wakifuatilia kikao cha Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Dkt. Bashiru Ally na viongozi na watendaji wa Chama Cha Mapinduzi na Serikali  mkoani Simiyu kilichofanyika Mjini Bariadi Januari 05,2019 wakati wa ziara yake mkoani hapa.
Baadhi ya viongozi wa CCM wa Mkoa wa Simiyu wakicheza nyimbo za Chama wakati wakijiandaa kumpokea Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Dkt. Bashiru Ally(hayupo pichani) katika Mji mdogo wa Lamadi wilayani Busega, kwa ajili ya kuanza ziara ya siku mbili mkoani hapa Januari 05 na Januari 06 , 2019.


0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!