Wednesday, January 23, 2019

Waziri wa Afya Aitaka TBA Kurejesha Fedha za Ujenzi wa Mradi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu.

Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu ameagiza Wakala wa Majengo nchini TBA kurejesha fedha ilizokabidhiwa na wizara yake kwenye ofisi za TBA mjini Bariadi ili zitumike kukamilisha mradi wa ujenzi wa hospitali ya rufaa ya mkoa wa Simiyu ambao kasi ya ujenzi wake kwa sasa hairidhishi.

Waziri Ummy ametoa kauli hiyo katika ziara yake ya siku moja mjini Bariadi, mkoani Simiyu kukagua ujenzi wa jengo litakalotumika kutoa huduma za maabara, upasuaji na mionzi na kusema kuwa serikali imejiwekea malengo ifikapo Julai  Mosi wananchi waanze kupata huduma kwani tayari fedha zote za mradi huo zimekwishalipwa.

 “Wizara tayari imeshalipa zaidi ya shilingi bilioni moja kwa TBA lakini cha ajabu wao wameleta shilingi milioni 430 tu, na matokeo yake ndio haya, ukiangalia muda tuliopewa kukamilisha kazi hii si rafiki, sasa ninawaagiza TBA walete hiyo pesa site ili kazi iendelee”.

“ Hivi jamani kwa kasi hii kweli tunaweza kuendelea kuweka matumaini kwa hawa ndugu zetu, ukiangalia mheshimiwa Rais ametupatia shilingi bilioni 2.5 tujenge jengo la mama na mtoto sasa kwa utaratibu huu wa kusuasua mnadhani tutafika kweli, mimi nadhani umefika wakati tutumie force account kwenye mradi huu, Bariadi kuna mafundi wengi wazawa wenye uwezo mkubwa wa kutufanyia kazi hii”, alisisitiza Waziri Ummy.

Kuhusu mpango wa serikali wa kuboresha huduma za rufaa katika hospitali zote za mkoa nchini, Waziri Ummy amesema wizara imedaa utaratibu ambapo kila hospitali itapata madaktari bingwa 16 katika fani 8 yaani madaktari 2 kila fani wakiwemo madaktari bingwa wa akina mama, watoto, Mishipa ya fahamu, mifupa, njia ya mkojo, dawa za usingizi na mionzi.

“ Tunataka tuwe na maabara kubwa za kisasa pamoja na jengo la mionzi kama tunalojenga hapa Simiyu katika kila hospitali ya rufaa ya mkoa, tunamshukuru sana mheshimiwa rais kwa kutupatia shilingi bilioni 3.5 kwa ajili ya ujenzi wa jengo uchunguzi, ninaomba kila mmoja wenu kwa nafasi yake ahakikishe miradi yote inayotumia fedha za serikali inatekelezwa kwa ufanisi”, aliongeza Waziri Ummy.

Akijibu maombi ya viongozi wa chama na serikali wa mkoa wa Simiyu kuhusu tatizo la usafiri kwa watumishi watakaopangiwa kufanya kazi katika hospitali ya rufaa ambayo kwa sasa haina nyumba za watumishi, Waziri Ummy amewahakikishia kuwa Wizara itaangalia uwezekano wa kuipatia hospitali hiyo basi maalumu la watumishi halikadhalika itaweka bajeti ya ujenzi wa nyumba za watumishi katika mwaka wa fedha ujao.

Akiwa katika hospitali ya wilaya ya Bariadi ya Somanda, Waziri Ummy alielezea kutoridhiswa na utaratibu wa kutoa huduma katika wodi ya wazazi na kumwagiza mganga mkuu wa mkoa kuzifanyia marekebisho kasoro zote zilizobainika ili huduma zinazotolewa ziendane ni miongozo ya wizara.

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka amemhakikishia Waziri Ummy kuwa,  mkoa utasimamia kikamilifu utakelezaji wa mradi huo na kusisitiza kuwa pale ambapo pamebainika kuwa na dosari atahakikisha zinarekebishwa ili kuongeza ufanisi katika mradi huo.
“Mhe Waziri mimi nina amini kukamilika kwa hospitali hii ni mkombozi kwa maelfu ya wananchi wetu wa mkoa wa Simiyu,  sasa wajiandae kupata huduma bora zikiwemo za bima ya afya ambazo zimeboreshwa kwa kiwango kikubwa, kwa ujumla tunaamini zitawahamasisha watu wengi zaidi kujiunga na  huduma hiyo”, alisisitiza RC Mtaka.  

Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu amekamilisha ziara yake mkoani Simiyu na Kuelekea katika mikoa ya Geita na Shinyanga.


Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu Akiongozana na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Kukagua Ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu katika eneo la Nyaumata Kilomita chache kutoka mjini Bariadi
Viongozi wa Chama na Serikali pamoja na Watumishi wa Ngazi mbalimbali kutoka mkoani Simiyu Wakisikiliza Maelekezo ya  Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu Wakati wa Ziara yake Katika Eneo la Nyaumata inapojengwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa. 
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka Akimpa Maelezo Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akipewa maelezo kuhusu Ujenzi wa Jengo jipya litakalotumika kutoa huduma za maabara, upasuaji na mionzi katika eneo la Nyaumata Wilayani Bariadi.
Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akitoa maelekezo katika eneo la ujenzi wa hospitali ya rufaa ya mkoa wa Simiyu eneo la Nyaumata Wilayani Bariadi.
Mafundi wakiendelea na Shughuli ya ujenzi wa jengo litakalotumika kutoa  huduma za maabara, upasuaji na mionzi katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Simiyu eneo la Nyaumata wilayani Bariadi.
Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu  na mwenyeji wake Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka wakielekea kukagua Jengo la hospitali ya rufaa ya Mkoa lililokamilika katika eneo la Nyaumata Wilayani Bariadi.

Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu  na mwenyeji wake Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka Mkuu Wakiwasili katika Jengo Jipya la Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu Eneo la Nyaumata, Wilayani Bariadi.
Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akipewa maelezo katika moja ya chumba cha wagonjwa katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Simiyu iliyopo eneo la Nyaumata wilayani Bariadi, kulia kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Anthony Mtaka






0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!