Monday, January 21, 2019

Viongozi wa Riadha Kanda ya Ziwa Washauriwa Kuziandaa Timu zao Mapema


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu ambaye pia ni rais wa chama cha riadha nchini Anthony Mtaka amewaagiza viongozi wa riadha kanda ya ziwa kuweka mpango mkakati endelevu wa kuwatambua na kuwaandaa kikamilifu wachezaji watakaoshiriki katika mashindano mbalimbali ndani na nje ya nchi.

Mhe Mtaka ametoa kauli hiyo katika kikao na viongozi wa vyama vya riadha kanda ya ziwa kilichofanyika mjini Bariadi ambapo amesema chama cha riadha kinakabiliwa na mashindano mbalimbali ikiwemo mbio za nyika za dunia zitakazofanyika nchini Denmark, mashindano ya Afrika yatakayofanyika nchini Morocco pamoja na mashindano ya relay yatakayofanyika nchini Japan hivyo ni muhimu maadalizi yakafanyika mapema ili kuwaandaa wachezaji kisaikolojia na hatimaye waweze kurejea na ushindi.

Adha Mhe Mtaka amesema chama hicho kimeandaa utaratibu mzuri wa kuwapata wachezaji wenye viwango ambapo yatafanyika majaribio nchi nzima ili kuwawezesha viongozi na makocha kubaini vipaji vipya ili wachezaji hao waweze kujumuishwa kwenye timu ya Taifa.

“ Naomba niwahakikishia hatuwezi kupata wachezaji wazuri kama tutakaa tunalalamika, nendeni mkafanye majaribio katika ngazi za mikoa yenu, chagueni wachezaji wazuri ambao tutakuwa na uhakika watarejea na ushindi”.

“ Binafsi ninawaahidi nitawapa msaada wowote mnaohitaji, sote tunafahamu kanda ya ziwa kuna wachezaji wazuri sana, kinachohitajika ni kuweka mfumo mzuri wa kuwatambua na ndio maana tumeamua safari hii tutakuwa na makocha watano kwenye kambi zetu za taifa ambazo tunatarajia kuziweka katika mikoa ya Arusha na Pwani, mimi ninaamini tukidhamiria kuleta mabadiliko katika mchezo huu tunaweza ”, alisisitiza Mtaka.

Kwa upande wao wajumbe wa kikao hicho akiwemo mwanariadha  mkongwe ambaye ni mchezaji wa kwanza kushiriki katika michezo ya Olympic mwaka 1964, Mzee Thomas Daniel walimweleza rais wa chama hicho kuwa ukosefu wa viwanja vyenye ubora, kutokuwepo kozi ya makocha wa ngazi ya juu, uhaba wa vifaa pamoja na kozi maalumu kwa ajili ya makocha ni miongoni mwa changamoto zinazohitaji kupatiwa majawabu ili kuongeza hamasa katika mchezo huo.

Kikao hicho cha siku moja kilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa vyama vya riadha kanda ya ziwa kutoka mikoa ya Simiyu, Mwanza, Mara na Geita.


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu na rais wa chama cha riadha nchini Anthony Mtaka akiwakaribisha wajumbe wa kikao cha kuweka mikakati ya kuboresha riadha ofisini kwake mjini Bariadi.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu ambaye pia ni rais wa chama cha riadha nchini Anthony Mtaka akiwa kwenye kikao na viongozi wa vyama vya riadha kanda ya ziwa mjini Bariadi.

Baadhi ya viongozi wa riadha kutoka mikoa ya Simiyu, Mara, Mwanza na Geita wakiwa katika kikao na rais wa chama hicho mjini Bariadi.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu na rais wa chama cha riadha nchini Anthony Mtaka akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa riadha kutoka mikoa ya Simiyu, Mara,  Geita na Mwanza mara baada ya kikao chao mjini Bariadi.


0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!