Thursday, February 28, 2019

DC BARIADI: WALEMAVU WATASHIRIKISHWA KATIKA FURSA ZOTE ZA KIUCHUMI

Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga amesema Serikali wilayani humo itaendelea kuhakikisha watu wenye ulemavu wanashirikishwa katika fursa za kiuchumi ili waweze kujikwamua kiuchumi na kuondokana na utegemezi.


Kiswaga ameyasema hayo wakati wa ziara ya Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia watu wenye Ulemavu, Mhe. Stella Ikupa Wilayani Bariadi, ambayo ililenga kujionea utekelezaji wa mradi wa kitalu nyumba na masuala mbalimbali ya watu wenye ulemavu.

Amesema katika mradi wa kitalu nyumba ambao utahusisha vijana 100 atahakikisha vijana wenye ulemavu wanashirikishwa kupata elimu ya ujenzi wa kitalu nyumba na kilimo cha kisasa chenye tija kupitia mradi huo ili waweze kujiajiri na kujipatia kipato.

Aidha, katika mradi wa ushonaji unaotarajiwa kuanza kutekelezwa hivi karibuni katika Halmashauri ya Mji wa Bariadi  atakahikisha sehemu ya washiriki katika miradi huo ni watu wenye ulemavu.

“Tunatarajia kuanza mradi wa ushonaji hapa Bariadi Mjini na tayari tuna vyerehani 50 kwa  hiyo tutahakikisha watu wenye ulemavu wamejumuishwa ili nao wanufaike na mradi huu ambao utawasaidia wananchi kupata kipato na Halmashauri kupata chanzo cha mapato pia” alisema Kiswaga.

Kwa upande wao watu wenye ulemavu pamoja na kuishukuru serikali kwa kushughulikia  changamoto zinazowakabili wameomba Serikali kuendelea kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa watu wenye ulemavu na kuongeza walimu wa elimu maalum.

Vile vile wameomba watu wenye ulemavu wapewe kipaumbele katika suala la ajira na mafunzo mbalimbali yakiwepo ya Jeshi la Kujenga Taifa ili nao wawe sehemu ya kutegemewa katika jamii badala ya kuwa tegemezi.

“Tunaishukuru Serikali kutusaidia kutatua changamoto mbalimbali lakini tunaendelea kuiomba iboreshe mazingira ya kujifunzia kwa watoto wenye ulemavu kwa kuongeza madarasa na wataalam wa lugha ya alama, ili nao wapate haki yao ya msingi ya elimu bora”alisema Alex Benedicto Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Wasiosikia

Akijibu baadhi ya changamoto za watu wenye ulemavu, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia watu wenye Ulemavu, Mhe. Stella Ikupa amesema Serikali imeendelea kuajiri watu wenye ulemavu katika kada mbalimbali huku akitoa wito kwa Halmashauri kuweka mikakati ya kutafuta wataalam wa lugha ya alama ili waweze kuwasaidia walemavu wasiosikia kuwasiliana.

Kuhusu miundombinu Mhe. Ikupa ametoa wito kwa taasisi zinazoendelea kujenga majengo zizingatie ujenzi wa miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu na kwa upande wa majengo ya zamani taasisi zione namna ya kufanya marekebisho madogo ili ziweze kufikika kirahisi na watu enye ulemavu katika kupata huduma.

Naibu Waziri Stella Ikupa akiwa wilayani Bariadi amezungumza na viongozi wa Serikali na watu wenye ulemavu pamoja na kutembelea mradi wa Kitalu nyumba ili kujionea utekelezaji.

MWISHO




Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia watu wenye Ulemavu, Mhe. Stella Ikupa akipokelewa na baadhi ya viongozi wa Wilaya ya Bariadi kuelekea kwenye kikao kuzungumza na viongozi hao na watu wenye ulemavu Mjini Bariadi, wakati akiwa katika ziara yake ya kikazi  Wilayani humo, Feburuari 2019.



Kiongozi wa Chama cha Watu wenye ulemavu wa kusikia, Alex Benson  akichangia hoja katika kikao cha Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia watu wenye Ulemavu, Mhe. Stella Ikupa na viongozi wa Serikali na watu wenye ulemavu Mjini Bariadi, wakati akiwa katika ziara yake ya kikazi  Wilayani humo, Feburuari 2019.

Katibu wa SHIVYAWATA Wilaya ya Bariadi, Zizi Kubilu akiwasilisha taarifa ya walemavu  kwa Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia watu wenye Ulemavu, Mhe. Stella Ikupa na viongozi wa Serikali na watu wenye ulemavu Mjini Bariadi, wakati akiwa katika ziara yake ya kikazi  Wilayani humo, Feburuari 2019.
Mkalimani wa lugha ya alama(mbele kulia) akiwatafsiria baadhi ya watu wenye ulemavu wa kusikia hotuba ya Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia watu wenye Ulemavu, Mhe. Stella Ikupa, wakati  akizungumza na  viongozi wa Serikali na watu wenye ulemavu Mjini Bariadi, alipokuwa katika ziara yake ya kikazi  Wilayani humo, Feburuari 2019.
Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga akiwasilisha taarifa ya Wilaya kuhusu watu wenye ulemavu kwa Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia watu wenye Ulemavu, Mhe. Stella Ikupa, wakati akiwa  katika ziara yake ya kikazi  Wilayani humo, Feburuari 2019.
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia watu wenye Ulemavu, Mhe. Stella Ikupa(aliyepo kwenye gari) akizungumza na viongozi wa Serikali na watu wenye ulemavu wilayani Meatu  baada ya kutembelea Kitalu nyumba kilichopo Nyakabindi , wakati akiwa katika ziara yake ya kikazi  Wilayani Bariadi, Feburuari 2019.
Baadhi ya viongozi na watu wenye ulemavu Wilaya ya Bariadi wakipewa maelezo juu kilimo kinavyofanyika katika Kitalu nyumba kilichopo Nyakabindi
Baadhi ya wakuu wa idara halmashauri ya Wilaya ya Bariadi na Mji wa Bariadi wakifuatilia kikao cha Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia watu wenye Ulemavu, Mhe. Stella Ikupa(hayupo pichani ) na viongozi wa Serikali na watu wenye ulemavu wilayani Bariadi, wakati akiwa katika ziara yake ya kikazi  Wilayani Bariadi, Feburuari 2019




0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!