Sunday, April 12, 2020

TUSHEREKEE PASAKA TUKICHUKUA TAHADHARI DHIDI YA CORONA: RC MTAKA


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka leo ameshiriki ibada ya Pasaka katika makanisa tofauti mjini Bariadi na kuwasisitiza waumini na wananchi wote wa Mkoa wa Simiyu kutulia, kuepuka safari zisizo za lazima na kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi ya Virusi vya Corona kwa kuzingatia maelekezo yanayotolewa na Serikali.

Mtaka ameyasema hayo kwa nyakati tofauti wakati akitoa salamu za Pasaka za Mkoa aliposhiriki ibada katika Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu John, Parokia ya Mtakatifu Luka, Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Bariadi Mjini na Kanisa la Africa Inland Church of Tanzania (AICT) leo Aprili 12, 2020.

“Nimeona watu wananawa mikono utaratibu huu usiishie kwenye nyumba za ibada na maeneo ya kutolea huduma, uende mpaka nyumbani,tunapokuwa kwenye nyumba za ibada pia tuzingatie umbali katika ukaaji wetu na wakati wa kupokea huduma za kiroho: pasaka hii tutulie majumbani tuepuke safari zisizo lazima na tufuate maelekezo ya Serikali.” alisema Mtaka.

Aidha, pamoja na kuwasisitiza wananchi kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima Mtaka ametoa wito kwa jamii kuona namna ya kuwasaidia zaidi wazee, watoto  na watu wenye magonjwa yasiyoambukiza kama kisukari na shinikizo la damu kuepuka zaidi mikusanyiko hiyo ili kuwaondolea hatari ya kupata maambukizi kutokana na hali ya kinga zao za mwili.

Katika hatua nyingine Mtaka amewataka wazazi kuwasimamia watoto wao kujisomea kwa bidii kipindi hiki ambacho shule zimefungwa kutokana na tahadhari ya maambukizi ya Virusi vya Corona hususani wale wa madarasa ya Mitihani ya Kitaifa kwa kuwa mitihani hiyo bado ipo na itafanyika.

Sambamba na hayo Mtaka amewaasa wananchi wa Mkoa wa Simiyu kutunza chakula ambacho kimepatikana mwaka huu na kutokiuza kwa matumizi ambayo si ya lazima hususani katika kipindi hiki ambacho chakula kinauzwa kwa bei ya chini huku akiwasisitiza kujiunga na Bima ya Afya na Mfuko wa Afya ya Jamii ili waweze kupata unafuu katika huduma za matibabu.

Kwa upande wao viongozi wa makanisa akiwemo Paroko Msaidizi wa Parokia ya Mtakatifu John, Peter Mkunya, Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Luka, Martine Jilala, Mchungaji wa KKKT Bariadi, Greyson Kinyaha na Mchungaji wa AICT, Amosi Ndaki wamesema wametumia Maadhimisho ya Kufufuka kwa Yesu Kristo(Pasaka) kuliombea Taifa ili Mungu aliponye na Janga la Corona na kuendelea kuwakumbusha waumini kuzingatia maelekezo ya viongozi wa Serikali na wataalam wa afya.

Koga Mihama na George Lyimo ni miongoni mwa waumini waliohudhuria ibada ya pasaka wameishukuru Serikali kwa jitihada zinazoendelea kuchukuliwa kujikinga na Maambukizi ya CORONA huku wakitoa wito kwa wananchi wote kufuata maelekezo yanayotolewa na Serikali ili Maambukizi ya Virusi vya Corona yaishe nchini Tanzania.

MWISHO
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka  akizungumza na waumini wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Usharika wa Bariadi Mjini (hawapo pichani), wakati alipofika kanisani hapo kutoa salamu za Pasaka kwa waumini hao leo Aprili 12, 2020 kushoto ni Mchungaji wa Kanisa hilo, Greyson Kinyaha na kulia ni Mchungaji Sarah Kimaro.
Baadhi ya waumini wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Usharika wa Bariadi Mjini wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka  wakati alipofika kanisani hapo kutoa salamu za Pasaka kwa waumini hao leo Aprili 12, 2020.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka akipokea ekaristi takatifu katika misa takatifu Kanisa Katoliki Parokia ya Mtakatifu John Bariadi Mjini, wakati aliposhiriki katika misa hiyo na kutoa salamu za pasaka kwa waumini wa Kanisa hilo waumini hao leo Aprili 12, 2020.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka  akizungumza na waumini wa Kanisa la Africa Inland Church of Tanzania(AICT) Bariadi Mjini wakati alipofika kanisani hapo kutoa salamu za Pasaka kwa waumini hao leo Aprili 12, 2020.
Paroko Msaidizi wa Parokia ya Mtakatifu John Bariadi Mjini,Peter Mkunya akitoa mahubisri ya neno la Mungu katika misa Takatifu leo Aprili 12, 2020.
Waimbaji wa Kwaya ya Uinjilisti katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Usharika wa Bariadi Mjini wakiimba wakati wa ibada ya kwanza  leo Aprili 12, 2020 kuadhimisha Siku ya Pasaka ambapo Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka   ameshiriki katika ibada hiyo na kutoa salamu za pasaka kwa waumini na wananchi.
 Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka akinawa mikono kwa maji tiririka na sabuni mara baada ya kuwasili katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania(KKKT) Bariadi Mjini ambapo ameshiriki ibada ya Pasaka na kutoa salamu za Pasaka za Mkoa leo Aprili 12, 2020 kwa waumini wa Kanisa hilo. 


 Waimbaji wa Kwaya kutoka Kanisa la Africa Inland Church of Tanzania(AICT) Bariadi Mjini wakiimba wakati wa ibada leo Aprili 12, 2020 kuadhimisha Siku ya Pasaka ambapo Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka   ameshiriki katika ibada hiyo na kutoa salamu za pasaka za mkoa kwa waumini wa kanisa hilo.


 Mchungaji wa Kanisa la Africa Inland Church of Tanzania(AICT) Bariadi Mjini, Amosi Ndaki akitoa mahubiri ya neno la Mungu wakati wa ibada leo Aprili 12, 2020 kuadhimisha Siku ya Pasaka ambapo Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka   ameshiriki katika ibada hiyo na kutoa salamu za pasaka za mkoa kwa waumini wa kanisa hilo.


 Kwaya ya Mtakatifu Johh kutoka Parokia ya Mtakatifu John Bariadi Mjini  wakiimba wakati wa misa takatifu  leo Aprili 12, 2020 kuadhimisha Siku ya Pasaka ambapo Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka   ameshiriki katika misa hiyo na kutoa salamu za pasaka za mkoa kwa waumini wa kanisa hilo.


 Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka (mwenye suti nyeusi katikati ) akiwa katika misa na waumini wengine wa Kanisa la Mtakatifu Luka Mjini Bariadi leo Aprili 12, 2020 ambapo ametoa salamu za pasaka za mkoa kwa waumini wa Kanisa hilo.


 Baadhi ya wanakwaya na Waumini wa Kanisa la Mtakatifu Luka Mjini Bariadi wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka wakati akitoa salamu za Pasaka za Mkoa kwa waumini wa kanisa hilo leo Aprili 12, 2020. 


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka akiagana na baadhi ya viongozi waandamizi katika  Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Usharika wa Bariadi Mjini mara baada ya kushiriki katika ibada ya Pasaka kanisani hapo na kutoa salamu za pasaka za mkoa kwa  waumini leo Aprili 12, 2020.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!