Saturday, February 10, 2018

SERIKALI KUTOA CHUPA 2,000,000 ZA DAWA YA KUUWA WADUDU WANAOSHAMBULIA PAMBA SIMIYU

Serikali imewahakikishia wakulima wa pamba Mkoani Simiyu kuwa  itatoa chupa 2,000,000 za dawa ya  kuuwa wadudu wanaoshambulia zao la Pamba  ili kuwasaidia katika kukabiliana na wadudu hao.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Mhandisi Mathew Mtigumwe jana alipofanya ziara katika Wilaya ya Bariadi, Itilima na Maswa Mkoani Simiyu  kwa ajili ya kukagua mashamba ya pamba na kujionea changamoto zinazowakabili wakulima wa pamba.

Mhandisi Mtigumwe amesema lengo la Serikali lilikuwa ni kutoa chupa za dawa 1,800,000 lakini kutokana kuongezeka kwa wakulima wa zao hilo,  Serikali kupitia Bodi ya Pamba imeamua kutoa chupa 2,000,000 .

“Awali tulipanga kusambaza chupa 1,800,000 lakini mahitaji yamekuwa makubwa, kwa hiyo tutaongeza na kufikia chupa 2,000,000 na kufikia mwishoni mwa mwezi Februari chupa 1,000,000 zitakuwa zimeshafika Simiyu” alisistiza Mhandisi Mtigumwe.
Aidha, Mtigumwe alisisitiza viongozi na wataalam wa Kilimo mkoani Simiyu kusimamia ugawaji wa dawa hizo kwa wakulima na kuhakikisha zinatumika vizuri.
Aliongeza kuwa Wizara imetoa wataalam wake wasiopungua 60 kutoka makao makuu ya Wizara, Kituo cha Utafiti cha Ukirigulu na Chuo cha Kilimo Ukirigulu na kuwapeleka katika mikoa yote inayolima pamba, lengo likiwa ni kutoa elimu kwa wakulima na Maafisa Ugani juu ya matumizi sahihi ya dawa za kuua wadudu(viuadudu).
Masanja Mabula mkulima wa Pamba kutoka  Kijiji cha Mbiti Wilayani Bariadi alisema katika msimu wa mwaka 2017/2018 wakulima wamehamasika kulima pamba hivyo wanaomba Serikali iwasaidie wapate dawa ili wadhibiti wadudu waharibifu.

Awali akiwasilisha taarifa ya Mkoa, Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Ndg.Jumanne Sagini alisema Mkoa huo unahitaji chupa za dawa 1,810,839 kwa ajili ya wakulima wa pamba 309,511 ambao wamelima ekari 602,409 zikitarajiwa kuzalisha tani 421,686.3 za pamba kwa wastani wa kilo 700 kwa ekari moja.
Hadi kufikia Januari 31, 2018  Mkoa wa Simiyu umelima jumla ya hekta 241,445.2 sawa na ekari 603,613, ambazo ni asilimia 85.1 ya lengo la kulima ekari 709,296.5
Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew Mtigumwe (mwenye miwani katikati) akipewa maelezo na  mkaguzi wa pamba wilaya ya Bariadi Alfred Chagula juu ya mmea wa zao la pamba ulioshambuliwa na wadudu wakati wa ziara yake jana katika mashamba ya wakulima wilayani humo.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew Mtigumwe (wa pili kushoto), Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Ndg.Jumanne Sagini wakiangalia shamba la pamba Mkulima Emmanuel Masuke wakati walipotembelea mashamba ya wakulima jana katika Wilaya ya Bariadi, Iilima na Maswa mkoani Simiyu.
Katibu Mkuu wizara ya Kilimo Mathew Mtigumwe (mwenye miwani) akimsikiliza mkulima wa pamba Tindigwe Masuke(hayupo pichani) wa kijiji cha Mbiti wilayani Bariadi alipokuwa akiongelea juu ya uhitaji wa dawa, wakati wa ziara yake jana mkoani Simiyu.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Mhandisi Mathew Mtigumwe (mwenye miwani wa pili kushoto), akikagua shamba la pamba la Mkulima Emmanuel Masuke wakati wa ziara yake jana katika Wilaya ya Bariadi, Iilima na Maswa mkoani Simiyu.


0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!