Wednesday, February 21, 2018

SERIKALI YAWAHAKIKISHIA WANANCHI WA ITILIMA UJENZI WA HOSPITALI YA WILAYA


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano  wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amewahakikishia wananchi  wa Itilima ujenzi wa hospitali ya wilaya itakayowawezesha kupata huduma bora zaidi za Afya wilayani humo.

Mhe.Makamu wa Rais  ameyasema   alipowasalimia wananchi wa makao makuu ya wilaya ya Itilima Lagangabilili mara baada ya kufungua Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya Itilima.

Amewapongeza viongozi wilayani  humo kwa kutatua changamoto mbalimbali za wananchi katika sekta za elimu, maji, kilimo na sekta nyingine huku akiahidi kushughulikia suala la ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ambayo ndiyo changamoto kubwa ya afya wilayani humo.

“Niwapongeze kwa mambo mbalimbali mliyopata kwenye elimu, maji, umeme na kuhusu changamoto ya afya  niwaahidi tu kuwa, hiyo ndiyo sekta ninayoisimamia mimi kama mama nitahakikisha Hospitali ya Wilaya inajengwa hapa Itilima” alisema

Aidha, akizungumza mara baada ya kufungua  jengo la utawala la halmashauri ya ITILIMA ameupongeza  uongozi wa wilaya ya Itilima kwa usimamizi mzuri wa Jengo na kuhakikisha linajengwa kwa gharama nafuu, huku akiwataka watendaji walitumie kuwatumikia wananchi katika kutatua kero zao.

Amesema Serikali imeboresha mazingira ya kazi kwa watumishi wilayani humo kwa kuwajengea jengo la kufanyia kazi na nyumba za kuishi hivyo wanapaswa kuwatumikia wananchi na watakaoshindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo hawatavumiliwa.

Wakati huo huo amewataka wananchi wa wilaya hiyo kulitumia jengo hilo kwa kupeleka masuala yao yanayopaswa kufanyiwa kazi na Serikali  kabla ya kwenda Serikali Kuu  na akaahidi kuwa Serikali itaendelea kuwapelekea watumishi wanaohitahijika.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa Itilima,   Mbunge wa Jimbo la Itilima Mhe. Njalu Silanga  ameishukuru Serikali kwa utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani humo.

“Mhe.Makamu wa Rais tunaishukuru Serikali ya awamu ya tano kwa  jinsi inavyotekeleza miradi mbalimbali, hapa tulipo tunalo tenki lenye ujazo wa lita 250,000 lenye thamani ya shilingi milioni 910, tunayo mabwawa manane kati ya hayo Bwawa la Habiya lililojengwa na Kampuni ya Serikali ya DDCA limeshaisha na tayari kwenye bajeti ya mwaka huu kuna usanifu unaendelea vijiji vinne vitapata maji “ alisema Njalu.

Akiwasilisha taarifa ya Ujenzi wa Jengo hilo la Utawala  la Halmashauri ya Wilaya ya Itilima, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Ndg. Mariano Mwanyigu amesema jengo hilo lenye vyumba 45 lililojengwa na wakala wa majengo nchini TBA , limegharimu kiasi shilingi milioni 621.

MWISHO
Makamu wa Rais Mhe.Samia Suluhu Hassan(wa pili kushoto) akikata utepe kufungua jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Itilima wakati wa Ziara yake Mkoani Simiyu, (kushoto) Mkuu wa Mkoa huo, Mhe.Anthony Mtaka
Mbunge wa Jimbo la Itilima, Mhe.Njalu Silanga akizungumza na wananchi wa Lagangabili mara baada ya Makamu wa Rais Mhe.Samia Suluhu Hassan kufungua jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Itilima wakati wa Ziara yake Mkoani Simiyu, (kushoto) Mkuu wa Mkoa huo, Mhe.Anthony Mtaka.
Makamu wa Rais Mhe.Samia Suluhu Hassan(kushoto) akizungumza jambo na viongozi wa Mkoa wa Simiyu na Wilaya ya Itilima kabla ya kufungua Jengo  la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Itilima wakati wa Ziara yake Mkoani Simiyu.
Makamu wa Rais Mhe.Samia Suluhu Hassan akizungumza na Wananchi wa Lagangabili Wilayani ya Itilima mara baada ya kufungua Jengo  la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Itilima wakati wa Ziara yake Mkoani Simiyu.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Samia Suluhu Hassan akipata maelezo juu ya Ujenzi wa Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Itilima kutoka kwa Meneja wa TBA Mkoa wa Simiyu, Mhandisi. Likimaitare Naunga  wakati wa Ziara yake Mkoani humo.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!