Thursday, February 15, 2018

DC BARIADI AAGIZA MKANDARASI ALIYETELEKEZA MRADI AKAMATWE

Mkuu wa Wilaya ya Bariadi  Mhe. Festo Kiswaga amemuagiza Meneja wa Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) wa Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi kumtafuta  mkandarasi wa Kampuni ya LNGA na kumpeleka Polisi ili akatoe maelezo ya sababu za kutelekeza kazi ya ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilomita 28 na kukiuka masharti ya mkataba.

Kiswaga alitoa agizo hilo wakati wa zoezi la kutia saini mikataba 16 ya ujenzi wa barabara na madaraja kati ya Wakandarasi na  Mameneja wa Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA)  wa Halmashauri za Mkoa wa Simiyu., ambapo alishuhudia zoezi hilo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka.

Kiswaga amesema amekuwa akimtafuta mkandarasi huyo ili wakae pamoja kujua sababu za kutelekeza na kuchelewesha ukamilishaji wa mradi huo lakini amekuwa  akikaidi wito na maagizo ya Serikali , hivyo ipo haja afikishwe katika jeshi hilo ili aweze kutoa maelezo.

“Mhandisi alinieleza mwenendo wa kazi yake nikamwita Ofisini tukamwonya, nilienda kutembelea mradi sikumkuta nikampigia simu hapokei, hii wiki ya tatu hapokei simu yangu wala ya Mhandisi, naagiza huyu mkandarasi LNGA atafutwe apelekwe polisi ili atueleze anatekeleza mradi wa Serikali au barabara ya nyumbani kwake” alisema Kiswaga.

Meneja wa TARURA wa Halmashauri ya Bariadi Vijijini  Mhandisi. Masatu Ndango amesema amepokea maelekezo ya Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga ya kumtafuta mkandarasi LNGA, anayefanya kazi ya matengenezo ya barabara ya Mbiti-Sakwe-Itubukilo (KM 17), Sakwe-Mbiti(KM 4), Sakwe-Pugu (KM 3) na Ngulyati-Mwanzoya (KM 4) ambaye kwa mujibu wa mkataba alipaswa kukamilisha kazi Desemba 2017.

Ndango amesema Mkandarasi huyo amekuwa akikaidi maelekezo kila anapoelezwa na ameshindwa  kukamilisha mradi kwa wakati,  hivyo kwa mujibu wa mkataba ameanza kukatwa Fedha ambazo ni adhabu ya ucheleweshwaji wa mradi(Liquidated damage).

Kutokana na hali hiyo Mkuu wa Wilaya, Mhe.Festo Kiswaga amesema Wakandarasi wa aina hiyo hawana na nafasi katika Mkoa wa Simiyu na kamwe wasifikirie kuwa mkoa huo ni mahali pa kujifunzia, hivyo akawataka Wakandarasi wote 16 waliosaini mikataba ya ujenzi wa barabara na madaraja kupitia TARURA kuheshimu kazi wanazopewa na Serikali.

Aidha, amewataka Mameneja wa TARURA mkoani Simiyu kuhakikisha wanajiridhisha na uwezo wa wakandarasi wote watakaotekeleza miradi mkoani humo, ili miradi yote itekelezwe kwa wakati na ubora unaotakiwa.

Akiwasilisha taarifa kwa niaba ya Mratibu wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Mkoa wa Simiyu, Meneja wa TARURA Halmashauri ya Mji Bariadi Mhandisi.Mathias Mugolozi amesema jumla ya mikataba itakayotekelezwa ni 16 ikiwa na thamani ya shilingi 1, 830, 524,724.91, ambapo Halmashauri ya Mji ina mikataba miwili(02), Bariadi Vijijini miwili(02), Itilima miwili(02), Busega miwili(02), Meatu miwili(02) na Maswa mikataba sita(06).

Kwa upande wake Mratibu wa TARURA Mkoa wa Simiyu, Mhandisi.Peter Mosha amesema TARURA mkoa  pamoja na Mameneja wa TARURA wa Halmashauri wamejipanga na watahakikisha wanatembelea miradi yote mara kwa mara na kufanya vikao vya ndani kwa lengo la kufanya tathmini ya maendeleo ya miradi hiyo.

Naye Mkandarasi Fahmy Hemed kutoka Kampuni ya Hemed Holdings Ltd ya Mkoani Shinyanga amesema watahakikisha wanafanya kazi katika viwango vya ubora vinavyohitajika, kukamilisha kwa wakati  na kuheshimu mikataba.

Miradi hii 16 ni ya kwanza kutekelezwa Mkoani Simiyu chini ya Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA),  tangu kuanzishwa kwa Wakala huo kupitia Tangazo la Serikali la tarehe 12/05/2017 na kuzinduliwa rasmi tarehe 02/07/2017.

Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe.Festo Kiswaga akishuhudia zoezi la kutia saini mikataba 16 ya ujenzi wa barabara na madaraja kati ya Wakandarasi na  Mameneja wa Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini(TARURA) wa Halmashauri za Mkoa wa Simiyu lililofanyika jana mjini Bariadi


Mratibu wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini(TARURA) Mkoa wa Simiyu, Mhandisi.Peter Mosha akizungumza na wakandarasi wa makampuni ya ujenzi(hawapo pichani) kabla ya zoezi zoezi la kutia saini mikataba 16 ya ujenzi wa barabara na madaraja kati ya Wakandarasi hao na  Mameneja wa Wakala wa TARURA wa Halmashauri za Mkoa wa Simiyu lililofanyika jana mjini Bariadi
Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe.Festo Kiswaga akizungumza na wakandarasi wa makampuni ya ujenzi(hawapo pichani) kabla ya zoezi zoezi la kutia saini mikataba 16 ya ujenzi wa barabara na madaraja kati ya Wakandarasi hao na  Mameneja wa Wakala wa TARURA wa Halmashauri za Mkoa wa Simiyu lililofanyika jana mjini Bariadi
 Meneja wa TARURA Halmashauri ya Mji wa Bariadi, Mhandisi.Mathias Mugolozi akifafanua jambo kabla ya zoezi zoezi la kutia saini mikataba 16 ya ujenzi wa barabara na madaraja kati ya Wakandarasi hao na  Mameneja wa Wakala wa TARURA wa Halmashauri za Mkoa wa Simiyu lililofanyika jana mjini Bariadi
Mwanasheria kutoka Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini(TARURA), Bw.Speratus Boniphace akifafanua jambo,  kabla ya  zoezi la kutia saini mikataba 16 ya ujenzi wa barabara na madaraja kati ya Wakandarasi na  Mameneja wa Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini(TARURA) wa Halmashauri za Mkoa wa Simiyu lililofanyika jana mjini Bariadi
 Baadhi ya Wakandarasi wa Makampuni ya ujenzi wakifuatilia maelekezo kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe.Festo Kiswaga aliyotoa kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka, kabla ya  zoezi la kutia saini mikataba 16 ya ujenzi wa barabara na madaraja kati ya Wakandarasi na  Mameneja wa Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini(TARURA) wa Halmashauri za Mkoa wa Simiyu lililofanyika jana mjini Bariadi


0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!