Saturday, May 4, 2019

SIKU YA WAKUNGA DUNIANI KITAIFA MWAKA 2019 KUFANYIKA SIMIYU

Maadhimisho ya Siku ya Wakunga Duniani Kitaifa mwaka 2019 yanatarajiwa kufanyika  kesho katika Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi Mkoani Simiyu, ambapo Mgeni rasmi atakuwa Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto, Dkt. Faustine Ndugulile akimwakilisha Makamu wa Rais wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amewakaribisha wakunga wote hapa nchini na kuwahakikishia kuwa Mkoa umefanya maandalizi ya  kutosha ili maadhimisho hayo yaweze kufana.

"Nitumie nafasi hii kama Mkuu wa Mkoa kuwaalika familia ya Wakunga wote Tanzania ambao wameanza safari kuja kwenye shughuli yao ya Kitaifa ndani ya mkoa wetu, niwahakikishie kuwa tumefanya maandalizi ya kutosha kuhakikisha shughuli yao inaenda vizuri" alisema Mtaka

Katika hatua nyingine Mtaka amelishukuru Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Idadi ya watu Duniani (UNFPA) kuwa sehemu ya kuwezesha Maadhimisho hayo Kitaifa kufanyika Mkoani Simiyu,  pamoja na  mchango mkubwa wa Shirika hilo na wadau wengine katika sekta ya afya ndani ya Mkoa.

Naye Makamu Mwakilishi Mkaazi wa UNFPA hapa nchini, Dkt.Hashina Begum amesema Kauli Mbiu ya Siku ya Wakunga Duniani mwaka 2019 inayosema"Wakunga ni Watetezi wa Haki za Wanawake" inakumbusha umuhimu wa wakunga katika kuwatetea kina mama wakati wa ujauzito, wakati wa kujifungua na baada ya kujifungua.


Ameongeza kuwa UNFPA imeendelea kushirikiana na Serikali  katika ukarabati wa vituo 38 vya afya, wodi za wazazi  na vyumba vya upasuaji, ununuzi wa vifaa na mashine za kumwezesha Mkunga kutoa huduma ya mama na mtoto kwa urahisi na kuwajengea uwezo wakunga 90 kutoka vituo vilivyokarabatiwa kutoa huduma za dharura kwa mama na mtoto.

Naye Rais Chama Cha Wakunga Tanzania (TAMA), Feddy Mwanga amesema TAMA inafanya kazi na Mkoa wa Simiyu kutoka mwaka 2016 kuwaelimisha Wakunga, ili waweze kutoa huduma za dharura kwa mama na mtoto hususani katika vituo vya pembezoni, huku akiishukuru UNFPA kwa mchango wake kifedha na utaalamu kuwezesha mafunzo hayo.

Ameongeza kuwa Dira ya TAMA ni kuona kuwa kila mama mjamzito anayejifungua na watoto wachanga wanahudumiwa na Wakunga wataalam na wanapata huduma bora, huku akitoa wito wananchi wa Simiyu kujitokeza kwa wingi katika Maadhimisho hayo ili waweze kupata huduma za upimaji bila malipo.
MWISHO.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka(katikati) akizungumza na waandishi wa habari  ( hawapo pichani) juu ya Maadhimisho ya Siku ya Wakunga Duniani ambayo Kitaifa yatakayofanyika kesho Mei 05, 2019 Mkoani Simiyu katika uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi.
Baadhi ya waandishi wa habari wa mkoa wa Simiyu wakiwa katika Mkutano na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka(hayupo pichani) uliolenga kutoa taarifa juu ya Maadhimisho ya Siku ya Wakunga Duniani ambayo Kitaifa yatakayofanyika kesho Mei 05, 2019 Mkoani Simiyu katika uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi.
Makamu Mwakilishi Mkaazi wa UNFPA hapa nchini, Dkt.Hashina Begum(wa pili kushoto) akitoa taarifa mbele ya waandishi wa habari juu ya Maadhimisho ya Siku ya Wakunga Duniani ambayo Kitaifa yatakayofanyika kesho Mei 05, 2019 Mkoani Simiyu katika uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi.
Rais Chama Cha Wakunga Tanzania (TAMA), Feddy Mwanga(katikati) akizungumza kwa niaba ya Chama hicho mbele ya mbele ya waandishi wa habari juu ya Maadhimisho ya Siku ya Wakunga Duniani ambayo Kitaifa yatakayofanyika kesho Mei 05, 2019 Mkoani Simiyu katika Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi. 

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!